Tuesday, September 3, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 3.



ILIPOISHIA........
Nilizidi kuchanganyikiwa nilipoanza kuwatambua baadhi yao, kilichokuwa kinanishangaza ni kwamba kila niliyemtambua alikuwa kashatangulia mbele ya haki tukamzika, yaani namaanisha alishakufa kitambo.

SASA ENDELEA.......
Mtu wa kwanza kumtambua alikuwa ni mzee Mboma, alionekana akitembeatembea huku uso wake ukiwa umeghubikwa na huzuni.
‘Ni mambo gani haya jamani?’ Nilibaki nikijiuliza.
Ni mwaka mmoja sasa tangu tumzike mzee Mboma. Kifo chake kiliwashtua watu wengi sana pale mtaani, na siyo mtaani kwetu peke yake; bali nchi nzima ilisikitishwa na kifo cha mzee huyo kutokana na umashuhuri wake.
Ukianza kuongelea waasisi wa chama kilichotukomboa kutoka kwenye utawala wa kikoloni hutomuacha mzee huyu. Alikuwa ni mwanasiasa mkongwe ambaye alionyesha uanaharakati wake katika kupigania uhuru wa nchi yetu na Afrika kwa ujumla.
Mzee huyo alitegemewa sana pale mtaani kwetu kwa ushauri na kusuluhisha migogoro kutokana na busara zake. Kitendawili kilijitokeza kufuatia habari za kifo chake, mpaka waleo bado hakijateguliwa.
Hakufa kwa ugonjwa wala hakuuliwa na mtu yeyote. Kwa kweli kifo chake kilizua gumzo kwenye vyombo vya habari; kujiua kwa kujinyonga bila kujulikana sababu ni fumbo tosha ambalo halijafumbuliwa mpaka sasa.
Alijinyonga mishale ya saa kumi jioni kwa kutumia kamba ya usumba palepale nyumbani kwake. Hakuacha waraka wowote kuelezea sababu zilizopelekea kuchukua uamuzi wa kujinyonga. Hata mkewe hakuwa na hili wala lile juu ya kifo chake. Watu wengi huwa hawaamini kuwa alijinyonga, lakini ukweli ndiyo huo.
Basi kitendo cha kumuona mzee Mboma katika kundi lile kilinifanya nizidi kutaharuki.
‘Kwani mtu akifa huwa anarudi tena duniani?’ Hili ndilo swali lililofuatia baada ya kuvuta kumbukumbu za mzee huyo aliyekuwa na busara sambamba na hekima mithili ya hayati baba wa taifa, mwl. Julius Kambarage Nyerere.
Sijakaa sawa nikamtambua mtu mwingine, mtu aliyekuwa muhimu sana na mhimili katika maisha yangu. Nilitamani kumkimbilia ili nikamsabahi kwa kumkumbatia. Nilijisahau kabisa kuwa awali nilishindwa kujongea japo ile hatua moja. Nilikosa jinsi baada ya kubaini kuwa hali yangu ilikuwa bado iko vilevile, viungo vya mwili wangu vyote vilikuwa havina nguvu mfano wa mtu aliyepooza.
Nilitaka kumuita lakini nikaishia kugugumia kwani sikuweza hata kukifumbua kinywa changu. Nilimung’unya mung’unya maneno utadhani bubu anayelalamika.
Kushindwa kwenda kumkumbatia ndugu yangu huyo wa damu kuliniumiza sana moyoni. Nilishindwa kupata uhakika ya kwamba na yeye alikuwa kaniona au la! Tatizo hata kuongea kwenyewe sikuweza, japo ningemuita kwa sauti natumai angenisikia.
 
ITAENDELEA..........

No comments:

Post a Comment