Monday, October 21, 2013

MLANGONI MWA SABINA sehemu ya 33



ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA....
          Baada ya kutoa utetezi huo, jaji Aneth Mwalukwa ambaye alikuwa ni mwanamama alipanga siku ya hukumu yangu baada ya mwezi mmoja.
SASA ENDELEA.......
Kwa namna moja au nyingine nilifurahi kusikia hivyo kwani nilikuwa na shauku kubwa ya kujua hatma ya hiyo kesi yangu. Japokuwa nilikuwa najua fika ya kwamba kuokoka kwangu ilikuwa ni bahati nasibu, kitendo cha kupelekwa mahakamani na kupandishwa kizimbani mara kwa mara kilikuwa kimeshanikifu.
Niliona ni heri hukumu yangu ikitoka, hata kama nitahukumiwa kunyongwa basi nitakaa gerezani bila bughudha siku zote za kungojea kunyongwa kwangu.
Niliteremka kizimbani na kuchukuliwa na askari magereza kwa ulinzi mkali mpaka kwenye karandinga lao kama ilivyo ada. Tulikaa kidogo kuwasubiri baadhi ya mahabusu ambao kesi zao zilikuwa zinaendelea kusikilizwa. Baada ya kukamilika wote, tuliondoka mahakamani na kuelekea magereza.

                        *****************************

Mwezi mmoja ulitimia tangu siku ambayo kesi yangu ilisikiliza. Hayawi hayawi hatimaye sasa yakawa, siku ya hukumu yangu iliwadia.
Mapigo ya moyo wangu yalikuwa yakinidunda kasi kuliko kawaida. Pamoja na kwamba nilikuwa naiombea siku ya hukumu ifike, siku hiyo nilikuwa nimenyong’onyea na kuwa mpole kama shilingi mia.
Usiombe kuwekwa kizimbani kwa mara ya mwisho ukisubiri hukumu, tena hukumu yenyewe ya kesi ya mauaji! Hakika nilikuwa nipo maji siku hiyo.
Nilipandishwa kizimbani huku nikiwa nimenywea pasipo mfano. Yaani ilikuwa ni tofauti kabisa na siku zingine zote nilizofika mahakamani hapo.
Jaji alianza kusoma hukumu yangu kwa kutaja kosa lililokuwa linanikabili na kutangulia kusema kuwa adhabu ya kosa hilo ni kifo endapo mtuhumia atapatikana na hatia.
Niliposikia hivyo moyo wangu ulilipuka pu kana kwamba ilikuwa ndiyo mara ya kwanza kusikia hiyo adhabu ya mtu mwenye hatia ya kuua.
Jaji huyo aliendelea kwa kusema kuwa hakuna shaka yoyote kwa ushahidi ambao ulitolewa ya kuwa nilimuua Kishoka Mpoto siku ya tukio hilo.
“Hata katika utetezi wake mshtakiwa kashindwa kutoa maelezo sawasawa ambayo yanaweza yakailinda hoja yake kuwa hajaua. Suala la kudai kuwa shahidi aliyetoa taarifa za tukio kituoni ni mchawi au ni jini haliwezi likaaminiwa na mahakama hata siku moja kwani hakuna uchawi juu ya sheria.” Aliendelea kutema maneno jaji Aneth Mwalukwa.
Aliendelea kusema kuwa ushahidi wa picha, alama za vidole kwenye mwili wa marehemu na kwenye kisu kilichokuwa kimetumika kumuulia Kishoka vilikuwa ni vielelezo tosha kabisa kunitia hatiani.
“Japokuwa sababu au chanzo cha mtuhumiwa kumuua marehemu hakijafahamika mpaka sasa kutokana na mshtakiwa kuendelea kushikilia msimamo wa kwamba hajaua, bado haiondoi dhana ya mtuhumia kupatikana na hatia ya kuua kwa kukusudia.” Alizidi kusema jaji huyo.
“Kazi yangu ilikuwa ni kuchambua madai ya pande zote mbili, lakini upande wa utetezi umeonekana kuwa na hoja ambazo hazina mantiki kabisa, hoja za kusingizia ushirikia. Katika kusoma madai ya upande wa mshtakiwa sikuona shahidi yeyote ama ushahidi wowote ulioonyesha kuwa ni kweli mtuhumiwa hajaua zaidi ya maneno matupu ya kudai kuwa tukio liliambatana na ushirikina.” Aliunguruma mwanamama huyo.
Mpaka hapo matumaini yalikuwa yameshaniishia kabisa. Nilijua fika kuwa mwisho wa hukumu yangu ni adhabu ya kifo. Huku maelezo ya hakimu hayajafika mwisho nilianza kuhisi machozi yakinilengalenga huku pua zangu zikionekana kuloa.
Jaji aliendelea kusema kuwa jambo la shahidi aliyetoa taarifa polisi kutotokea kituoni haliwezi likaleta shaka yoyote juu yake kwani jambo muhimu ambalo ni kutoa taarifa alikuwa kashalifanya. Tena kwa kuongeza ushahidi aliamua kujitokeza mahakamani na kutoa ushahidi wa picha ambao ulionyesha hali halisi ya tukio lilivyokuwa.
“Kutofika kituoni huenda kulichangiwa na woga pamoja na kuchanganyikiwa kutokana na uzito wa tukio jenyewe ulivyokuwa.” Aliendelea kufafanua jaji huyo.
Ulikuwa ni uchambuzi ambao ulichukua karibu saa moja. Jaji Aneth Mwalukwa alihitimisha hukumu yake iliyokuwa na kurasa kadhaa kwa kueleza kuwa anakubaliana na upande wa mashtaka kuwa nilikuwa nimetenda kosa la mauaji ya kukusudia dhidi ya marehemu Kishoka Mpoto.
“Kwa mujibu wa sheria za nchi yetu mtu anayepatikana na kosa hilo, adhabu yake ni kifo. Kwa hiyo natamka kwamba mahakama hii imemtia hatiani mshtakiwa Brighton David kwa kosa la kumuua Kishoka Mpoto kwa kukusudi.
Jaji alinyamaza kidogo kisha akanitazama na akuniambia,
“Mshtakiwa Brighton David nakuhukumu adhabu ya kifo, utanyongwa kwa kitanza mpaka ufe.”
            Jaji alipomaliza kusoma hukumu yangu aligonga nyundo mezani kisha akainuka na kuondoka.
            Kwa kweli sikuweza kujizuia. Nilijikuta nikiangua kilio cha haja huku simanzi na huzuni zikitawala kwa watu wengi waliokuwa wamefika mahakamani hapo, wale waliokuwa wananijua na hata wale ambao walikuwa hawanijui.
            Wakati jaji anaondoka mahakamani askari magereza walinishusha kizimbani na kuanza kunipeleka kwenye karandinga la magereza bila hata kunipa nafasi ya kuagana na baadhi ya watu niliokuwa najuana nao.
            Kijana niliyekuwa nimemuachia kuisimamia miradi yangu alikuja mbio akitaka kuongea nami kwa mara ya mwisho, lakini bila huruma askari alinisukuma na kunitaka niingie kwenye karandinga haraka.
            Gari lililokuwa limenichukua liliondoka kwa kasi ya ajabu kuelekea gerezani
    
                          **************************
HAYA SASA, HUKUMU IMESHATLEWA! BRIGHTON ATANYONGWA KWELI AU ITAKUWAJE? ENDELEA KUFUATILIA!

No comments:

Post a Comment