Monday, December 9, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 53

Kwa wasomaji wapya....
            Brighton anajikuta akitupwa gerezani na kuhukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe baada ya kusingiziwa kumuua mpangaji wake kishoka. Hata hivyo mtu aliyemsingizia anaenda gerezani na kumtorosha huku akimwambia kuwa kuna masharti atampa baada ya kukamilisha hilo zoezi. Sasa Brighton tayari yupo uraiani.......endelea.
ILIPOISHIA TOLEO LILLOPITA...
Masharti hayo ndiyo aliyopewa James naye akakubaliana nayo. Siku chake baada ya kuingia kwenye maagano yale ya kishetani wazazi wetu walikufa wote kwa mkupuo katika ajali ya kutisha.
SASA ENDELEA..........
            Habari hii ndiyo iliyonitonesha majeraha yaliyokuwa yamejengeka ndani ya moyo wangu mithili ya donda ndugu. Kuanzia hapo nilianza kumchukia James na kumuona ni shetani mkubwa ambaye alikuwa anastahili kutupwa kwenye moto wa jehanamu.
            Nilijikuta nahukumu wakati maandiko ya Mungu yanatuambia tusikuhumu ili na sisi tusije tukahukumiwa. Niliumia sana nilipoambiwa hiyo habari.
            ‘Ndiyo maana mambo ya kaka James yalianza kuwa safi mara baada ya vifo vya wazazi wetu.’ Niliwaza.
            Wakati huo huo nikakumbuka swali, nikaona nimuulize huyo huyo Sharifa kwani hata yeye alikuwa ni mdau wa kafara hizo.
“Umesema kafara ya daraja la kwanza inahusisha wazazi wote wawili na ndugu mmoja wa damu, mbona sasa baba yangu alikufa wakati hakuwa baba wa kumzaa James?”
“Kwa kuwa alikuwa kamuoa mama mzazi wa James na pia alikuwa na mapenzi ya baba kwake, basi kafara yake ilifana.” Alijibu Sharifa.
            Akaendelea kunieleza kosa la James lilikuja kutokea baada ya kutakiwa kutoa kafara nyingine ili kukamilisha kafara za kwenye daraja la kwanza. Hapo alitakiwa ndugu yake wa karibu; mdogo mtu, kaka mtu, shangazi ama mjomba.
Kwa bahati mbaya sana ndugu wa damu aliyekuwa yu ngali hai nilikuwa ni mimi peke yangu. Aliamua kukaidi kunitoa kafara kutokana na mambo mawili.
Jambo la kwanza ni upendo uliokuwepo baina yangu na yeye. Kusema kweli kaka James alikuwa ananipenda kupita kiasi, na ndiyo maana hakuwa tayari kunitoa kafara.
Jambo lingine lililomsababisha kaka James agome kunitoa kafara ni kwamba hapakuwa na ndungu mwingine wa karibu zaidi yangu mimi. Kama angenitoa kafara basi angebaki bila ndugu wa karibu katika dunia hii. Sasa kubaki bila ndugu wa karibu lilikuwa ni jambo gumu sana kwake.
Nadhani hata wewe mpenzi msomaji usingepata fursa ya kusimuliwa simulizi hii nzuri iliyojaa vitisho vya lejaleja na yenye kusisimua kwani ningekuwa tayari nimeshalala mauti.
Baada ya kuona kunitoa kafara haiwezekani, James aliacha kabisa kwenda kwa mganga aliyekuwa amemfanyia dawa ya kumpa utajiri huo wakati alitakiwa awe anaenda mara moja kwa mwezi kufanya ibada. Muda wa kukamilisha kafara ya daraja la kwanza ulipita huku akiwa hajakamilisha, akaongezwa muda wa ziada nao ukawa umepita.
Mganga alipoona James kapuuzia agano hilo aliamua kumripoti kwa wataalamu wake ambao ndiyo waliokuwa wanamwezesha kufanya uganga huo.
Wataalamu hao walikasirishwa sana na kitendo  chake cha kujifanya mjanja na mwenye akili kuzidi wao waliokuwa wamempa maagizo yale. Ndipo walipoamua kumtoa duniani kwa staili ya kujiua mwenyewe ili akaonekane ana dhambi hata mbele za mwenyezi Mungu.    
Japo kabla ya kutoa adhabu hiyo walitoa muda wa kutosha kwake wakitegemea labda angejirudi na kukamilisha agano lao, siku zilizidi kwenda bila ya mabadiliko yoyote ya kutaka kujirudi kwa James.
Tena alipoona kakaa muda mrefu bila kupatwa na matatizo yoyote ilhali alikuwa hajakamilisha kutoa kafara alijua kuwa huenda zile zote zilikuwa ni danganya toto tu na vitisho visivyokuwa na misingi yoyote. Baada ya muda wa nyongeza kuisha uhai wa James ukawa ni halali ya wataalamu hao.
Hayo ndiyo mambo yaliyosababisha kifo cha wazazi wangu pamoja na kaka yangu. Tamaa ya kaka yangu kupata mali nyingi kwa njia ya mkato ndiyo iliyagharimu maisha yake na ya wazazi wetu kwa ujumla. Habari hiyo yote mimi nilikuwa siijui ila Sharifa ndiye aliyekuja kuning’amua.
NINI KITAFUATIA? USIKOSE TOLEO LIJALO!!!


No comments:

Post a Comment