Sunday, January 12, 2014

Simulizi: Nimekosa nini? sehemu ya 1

                                                                 NIMEKOSA NINI?


Alfajiri na mapema niliamka. Sikuamka kwa bahati mbaya muda huo bali ilikuwa ndiyo kawaida yangu kila siku. Nilikuwa nikiamka asubuhi na mapema kwa ajili ya kwenda katika mihangaiko yangu ya kila siku.
                Ingawa siku hiyo nilikuwa kwenye mtoka kisha nikachelewa sana kurudi nyumbani, sikuwa na budi ya kujidamka asubuhi na mapema ili niende kazini.
                Baada ya kupiga mswaki niliingia maliwatoni kujiswafi. Nilipomaliza nilirudi chumbani kwangu, nikauramba kama ilivyokuwa ada kila nilipokuwa naelekea kazini.
                Nilichukua suruali yangu niliyokuwa nimevaa jana yake nilipokuwa kazini ili nichukue pochi iliyokuwa kwenye mfuko wa suruali hiyo kwani humo ndiyo kulikuwa na nauli yangu ya kunipeleka kazini na kunirudisha nyumbani.
                “Umeiona pochi yangu mama Chris?” Nilimuuliza mke wangu aliyekuwa kajilaza kitandani kwa wakati huo.
“Hata sijaiona, kwani ulikuwa umeiweka wapi?” Aliuliza.
“Nakumbuka jana nimeenda nayo kazini, lakini nimeangalia kwenye suruali niliyokuwa nimevaa sijaiona.”
“Mh! Sasa itakuwa wapi?”
“Kama vipi achana nayo kwa sasa, acha niende kazini nikirudi nitakuja niitafute vizuri! Cha kufanya sasa hivi nipe shilingi elfu kumi kwa ajili ya nauli.” Niimwambia mke wangu naye akainuka na kunichukulia kwenye droo ya kitanda kisha akanipatia.
                Nilimuaga mke wangu kwa kumbusu kwenye paji la uso kisha nikamalizia kwa mwanangu kipenzi  aliyekuwa bado kalala.
“Kila la heri mume wangu, nakutakia kazi njema!” Yalikuwa ni maneno ya mke wangu kipenzi mama Chris, maneno  ambayo alikuwa akiniambia kila siku nikiwa naelekea kazini.
“Asante mama, na wewe nakutakia siku njema, utamsalimia mwanangu Chris atakapoamka.” Nilijibu huku nikichana chana nywele zangu huku nikijiangalia kwenye kioo kikubwa kilichokuwepo kwenye meza ya kujirembea iliyokuwemo humo chumbani.
                Nilipoanza  kuondoka mama Chris akanishika mkono,
“Ngoja kwanza baba wewe!”  Alitamka maneno yale wakati akiuvuta mkono wangu!
“Nini tena mama?” Nilihoji kwa lugha ya kubembeleza nikidhani kuwa labda mama Chris anataka mambo yetu yale ya mchezo wa kikubwa, maana katika kumbukumbu zangu usiku huo timu zote zilikuwa kambi kwani mwenzangu alikuwa katika sherehe zake za kila mwezi.
                “Hii tai haijakaa vizuri mume wangu, angalia na hii kola ya shati lako shingoni ilivyokaa shaghala baghala, utaenda unachekwa njia  nzima!” Aliongea wakati akinirekebisha huku tabasamu lake mwanana akilitoa.
“Nitachekwa mimi au utachekwa wewe mke wangu maana umeshindwa kunikagua wakati natoka!”
“Mimi sitachekwa  sababu sitakuwepo huko.” Aliongea mke wangu huku akihamia kwenye tai kuiweka sawa.
                Alipomaliza kuyaweka sawa mavazi yangu nilimkumbatia tena kwa mara nyingine na kumpiga mabusu motomoto kisha nikatoka zangu. Nilienda mpaka stendi kugombania daladala, si unajua tena usafiri wetu wa huku Bongo.
                Sikuchelewa kupata gari, nikapanda na kwenda kushukia posta mpya kisha nikaanza kutembea kwa miguu kuelekea ofisi yetu ilipokuwa.
                Nilipofika ofisini nilipigwa na butwaa baada ya kuwakuta watu wamejazana. Kwa haraka haraka nikaanza kuhisi kuwa kuna tukio kubwa ambalo lilikuwa limetokea. Watu walikuwa wameuzunguka mlango huku polisi wakiwa wanarandaranda.
                Maswali mia mia yakaanza kuzunguka katika akili yangu bila kupata majibu. Kwa kuwa nilikuwa tayari nipo kwenye tukio lenyewe, nilipiga moyo konde na kujiambia kuwa muda si mrefu nitakijua kilichojili.
                “Halafu linaonekana ni tukio kubwa sana, yaani mpaka polisi wamekuja!” Nilijiwazia huku nikitembea kwa tahadhari kuelekea ofisini.

ITAENDELEA........

Wednesday, January 1, 2014

Tanzia. WAZIRI WA FEDHA NCHINI TANZANIA AFARIKI DUNIA!!!

Breaking news!!!
WAZIRI WA FEDHA NCHINI TANZANIA MH DR. WILLIAM MGIMWA AFARIKI DUNIA!






Waziri wa Fedha, Dk. William Augustao Mgimwa (63) amefariki dunia.

Taarifa za hivi punde zinasema Waziri huyo wa fedha katika serikali ya awamu ya nne ya Rais Jakaya Kikwete amefariki dunia hii leo baada ya kuugua na kulazwa nchini Afrika Kusini.

Mgimwa aliyezaliwa January 20, 1950 na kuwa mbunge wa jimbo la Kalenga mkoani Iringa kupitia chama cha Mapinduzi (CCM) alikuwa amelazwa katika Hospitali ya Binafsi ya Milpark ya nchini humo.

Dk. Mgimwa alikuwa mkufunzi katika Chuo cha Benki mkoani Mwanza, kabla ya kufanikiwa kuchaguliwa kuwa Mbunge wa Jimbo la Kalenga, Mkoa wa Iringa, katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010.

Hospitali hiyo ya Milpark ndiyo imekuwa ikitumiwa na Serikali ya Tanzania kupeleka watu wanaoumwa na mtu wa karibuni zaidi kuhudumiwa katika hospitali hiyo ni marehemu Dk. Sengondo Mvungi.

HIKI NDICHO ALICHOANDIKA MBUNGE WA KIGOMA KASKAZINI ZITTO KABWE KWENYE UKURASA WAKE WA FACEBOOK MUDA MCHACHE ULIOPITA


Tanzia Waziri wa Fedha William Mgimwa, Mb

Nimepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za kifo cha Waziri wetu wa Fedha ndg. William Mgimwa.

Kwa kipindi kifupi nilichofanya naye kazi kwa karibu, kwanza kwenye Kamati ya Fedha (nikiwa mkaribishwa kama Waziri wa Fedha kivuli), kisha kwenye kamati ndogo niliyounda kuhusu miradi ya Umeme ya Mchuchuma na Liganga na Ngaka, na baadaye akiwa Waziri wa Fedha, jambo la msingi nilioona kwake ni unyenyekevu na heshima kubwa aliyonayo kwa watu wengine.

Hakusita kuomba ushauri licha ya kuwa na tofauti za kivyama na kwa kweli ni Waziri wa Fedha niliyeelewana naye zaidi kuliko wengine wote waliopita nikiwa ama Waziri Kivuli au Mwenyekiti wa Kamati za Mahesabu.


Uzalendo wake hauna mashaka na kujituma kwake katika kazi ni tabia ya kupigiwa mfano.

Mungu ameamua kumchukua mja wake na sisi wanadamu hatuna uwezo wa kupinga.


Nawapa pole sana familia yake kwa kumpoteza baba yao mpendwa. Naomba mola awape moyo wa subira katika kipindi hiki kigumu.

Nawapa pole wananchi wa Jimbo la Kalenga na Halmashauri ya Wilaya Iringa kwa kupoteza kiongozi wao.

Mola ailaze roho ya marehemu mahala pema peponi. Amina
Share this article :

Friday, December 27, 2013

HEBU CHEKA NA HII UONGEZE SIKU ZA KUISHI!

Mlevi mmoja aliingia kwenye daladala na kukaa siti ya mbele halafu akaweka begi lake kwenye siti ya pembeni kisha akapitiwa na usingizi.
Mara akaingia mlevi mwingine kwenye daladala hiyo na kulitoa begi la mlevi wa kwanza kisha akakaa.
Mlevi wa kwanza alipoamka alipeleka mikono yake alipokuwa ameliweka begi na kuanza kufungua zipi ya suruali ya mlevi wa pili akidhania ya kwamba ni zipu ya begi lake, baada ya kufungua zipu alianza kupapasa ndani ya zipu hiyo. Kwa hasira akauliza,
"nani kaweka ndizi na machungwa kwenye begi langu?"

Unajua kilichotokea hapo ni kipi? Like hapo chini kisha nitakutumia jibu kwenye inbox.

Monday, December 23, 2013

MIRATHI YA KAKA KUANZA UPYA KWENYE PAGE YA Hakuna kulala, Mpaka kieleweke?


Hakuna kulala, Mpaka kieleweke?


kama hukubahatika kusoma matoleo ya mwanzo ya hadithi ya "MIRATHI YA KAKA" ama unataka kukumbushia utamu uliomo kwenye hadithi hiyo tamu na yenye kusisimua, bofya kwenye link hiyo hapo juu kisha uilike, utapata post za hadithi ya mirathi ya kaka kuanzia matoleo ya wanzo. pia usisahau ku-like na kutupia comment zako bada ya kumaliza kusoma! .

Wednesday, December 18, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 56


Kwa wasomaji wapya....
Brighton anajikuta akitupwa gerezani na kuhukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe baada ya kusingiziwa kumuua mpangaji wake kishoka. Hata hivyo mtu aliyemsingizia anaenda gerezani na kumtorosha huku akimwambia kuwa kuna masharti atampa baada ya kukamilisha hilo zoezi. Sasa Brighton tayari yupo uraiani na anachukuliwa na Sharifa na kupelekwa kwenye hoteli na kuanza kuambiwa jinsi utajiri wa marehemu kaka yake (yaani James) ulivyopatikana.......endelea

ILIPOISHIA TOLEO LILLOPITA...

 Mara baada ya kuongea hivyo alinikabidhi funguo za gari zilizokuwa mezani. Kufumba na kufumbua alipotea ghafla, nikabaki peke yangu kwenye chumba hicho. Niliogopa sana.

                        **************************   
SASA ENDELEA..........
Asubuhi ilifika, ilikuwa ni asubuhi ya kwanza kuiona nikiwa uraiani baada ya kukaa rumande na hatimaye gerezani kwa miaka mingi. Niliamkia kwenye hoteli hiyo hiyo niliyokuwa nimepelekwa na Sharifa jana yake.
Mara baada ya kuamka nilitupia jicho langu kitandani kuiangalia brificase iliyokuwa imejaa mapesa niliyokuwa nimeachiwa na Sharifa. Niliiona imetulia. Nikajiinua kisha nikaifungua na kuiona minoti imejaa tele.
Nilipoangalia mezani niliziona funguo za gari niliyokuwa nimeachiwa. Kwa bahati nzuri chumba nilichokuwa kilikuwa kipo upande tuliokuwa tumeegesha gari. Nikaamua kuchungulia nje ili kujiridhisha kama gari hilo lilikuwepo kweli. Nikaliona limetulia.
Wazo nililokuwa nalo usiku wakati Sharifa hajaondoka ni kukataa katakata kufuata masharti yote niliyokuwa nikishinikizwa kuyafanya; masharti ya kuoa mwanamke kisha akishanizalia mtoto nimtoe kafara pamoja na mtoto aliyemzaa, na baada ya hapo niwe natoa kafara mtu mmoja kila mwaka ambaye ni mfanyakazi wangu ama mteja wangu wa aina yoyote ile.
Hata hivyo baada ya Sharifa kunishika kichwani muda mfupi kabla ya kuyeyuka ghafla wazo hilo nalo liliyeyuka kabisa kichwani mwangu. Nikaanza kujiona kama mtu anayechezea shilingi kwenye tundu la msala.
Nililipima jambo hilo usiku kucha kwa mapana na marefu, nikaona hakuna sababu yoyote ya kulipiga teke debe la bahati kama hilo. Kitu kilichonipa moyo ni kwamba sikutakiwa kumtoa kafara ndugu yangu yeyote wa karibu zaidi ya mke ambaye nitamuoa kwa ajili hiyo pamoja mtoto nitakayemzaa kwa ajili hiyo.
Nikaona ni bora nikubaliane na shinikizo la Sharifa ili nitengeneze maisha yangu, niwe mmoja kati ya matajiri wakubwa nchini na duniani pia. Moyo wangu uliridhia kabisa kutajirika kwa njia hiyo, njia ya nguvu za giza na ya kishetani huku nikiwa tayari kuendelea kuteketeza watu kila mwaka kwa kuwatoa kafara ili nizidi kuulinda utajiri wangu huo.
Pesa nilizokuwa nimeachiwa na Sharifa zilizidi kunipa jeuri, jeuri ya kwenda kununua nyumba sehemu yoyote katika nchi hiyo. Jambo la kuendelea kuishi kwenye mji huo sikuwa nalo kabisa akilini mwangu, hivyo nikaamua kuondoka asubuhi hiyo kwenda mji mwingine uliokuwa mbali na mji huo.
Niliinuka na kwenda maliwatoni kujimwagia maji mwilini mwangu. Nilipotoka nilivaa nguo zangu kisha nikainua simu ya mezani iliyokuwemo hotelini humo kuangiza kifungua kinywa.
Haukupia muda sana mlango ukagongwa, nami nilifungua na kumuona dada aliyekuwa amebeba trei (chano) iliyokuwa imesheheni mazagazaga kwa ajili ya kifungua kinywa.
Kabla hajaondoka nilichukua noti moja iliyokuwa na rangi ya kaki na kumpa ikiwa ni malipo ya kifungua kinywa hicho.
“Haina haja ya kulipa maana kila kitu kimelipiwa.” Aliniambia mwanadada huyo.
Hata hivyo ili kumuonyesha kuwa nilikuwa ni bilionea mtarajiwa kwa wakati huo, nilimwambia achukue tu hiyo pesa kwani nilikuwa nimeshaitoa kwenye mahesabu. Naye bila kuvunga aliipokea, si alikuwa kapewa!
“Samahani dada yangu kama nitakukwaza, ningependa kulijua jina lako.” Nilijikuta namchombeza zikiwa ni harakati za kutaka kutangaza nia katika suala zima la mapenzi.
Bila kinyongo wala malingo msichana huyo alinionyesha jina lake kwenye kitambulisho chake cha kazi alichokuwa amekining’iniza shingoni.
Nililisoma jina na kujikuta naachia tabasamu.
“Kumbe unaitwa Anna, jina lako lina historia ndefu sana katika maisha yangu.”
“Historia gani tena kaka yangu?”
“Kwanza mama yangu mzazi alikuwa akiitwa jina hilo, pili kuna msichana ambaye nilitokea kumpenda kupita kiasi naye alikuwa akiitwa Anna, ni jina muhimu sana katika maisha yangu.”
“Kumbe! Basi na mimi naitwa hivyo!”
“Natabiri na wewe utakuwa na historia ndefu sana katika maisha yangu,”
“Yaweza kuwa!” Aliongea Anna na kuanza kunipa mgongo ili aondoke.
Bila kufikiri wala kuwaza nilijikuta naropoka kumuomba namba ya simu ama mawasiliano yoyote. Pale pale alinitolea kadi yake ya biashara (business card) iliyokuwa na kila aina ya mawasiliano aliyokuwa akitumia.
“Asante sana mrembo!”
“Usijali!” Alimalizia maneno hayo huku akifungua mlango na kuondoka zake.
Taratiibu kabisa nilijongea kwenye kimeza kilipokuwepo chano cha mapochopocho ya chakula cha asubuhi. Pasipo kuvunga nilikaa na kuanza kujichana kwa raha zangu. Kilikuwa ni kifungua kinywa cha haja, waswahili wa siku hizi wanakwambia ‘msosi draft’ulioenda shule.
Muda mfupi baada ya kumaliza kushambulia kifungua kinywa niliondoka kwa mwendo wa madaha mpaka kwenye mchuma wangu huku nikiwa nimening’iniza kibrificase changu mithili ya kibosile ama fisadi aliyefutuka tumbo kwa kuchakachua fedha za umma.
Mpaka nafika nje sikumuona Anna, nilitamani sana japo tupungiane mkono wa kuagana ili nimringishie gari langu la kifahari, lakini haikuwezekana. Nadhani alikuwa kwenye majukumu yake mengine hotelini hapo.

JE, BRIGHTON ATAMUONA TENA ANNA? NA KAMA ATAMUONA ATAMWAMBIA NINI? FUATILIA TOLEO LIJALO!

Sunday, December 15, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 55

Kwa wasomaji wapya....
Brighton anajikuta akitupwa gerezani na kuhukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe baada ya kusingiziwa kumuua mpangaji wake kishoka. Hata hivyo mtu aliyemsingizia anaenda gerezani na kumtorosha huku akimwambia kuwa kuna masharti atampa baada ya kukamilisha hilo zoezi. Sasa Brighton tayari yupo uraiani na anachukuliwa na Sharifa na kupelekwa kwenye hoteli na kuanza kuambiwa jinsi utajiri wa marehemu kaka yake (yaani James) ulivyopatikana.......endelea

ILIPOISHIA TOLEO LILLOPITA...
Wakati nikiwa katika lindi la mawazo niligutushwa na sauti ya Sharifa. Alianza kwa kuniita jina langu.
“Brighton!”
“Naam!” Nami nilimwitikia.

SASA ENDELEA..........
“Usiwaze sana kwani kazi nzito ilishafanywa na kaka yako, unachotakiwa wewe ni kuikamilisha tu na utakuwa bilionea wa kuogopeka.” Alinyamaza kidogo kisha akaendelea.
“Daraja la kwanza utakuwa umeshalivuka kwani wazazi wa James ni wazazi wako, pia kufa kwake kutachukua nafasi ya ndugu wa karibu, kafara ambayo ilikuwa utolewe wewe. Kitakachohitajika kwako ni kuoa mke kisha mkishazaa mtoto unamtoa kafara akifuatiwa na mama yake, hapo utakuwa tayari umeshakamilisha daraja la pili.” Alipozi kidogo.
Wakati wote huo nilikuwa nimemsikiliza kwa makini. Baada ya kupozi kidogo aliendelea kuniambia kuwa nikishaimaliza daraja la pili lile lililokuwa linafuata ni mteremko. Daraja hilo ambalo ni daraja la tatu lilikuwa ni kumtoa kafara mtu mmoja kila mwaka, mtu huyo anaweza kuwa ni mfanya kazi wako ama ni mteja wako. Hiyo hatua ndiyo ilikuwa ni nyepesi kuliko zote kwani pale unamtoa mtu ambaye siyo ndugu wa karibu.
Hata hivyo bado ulikuwa ni mzigo mzito moyoni mwangu. Dhambi ya kuua nilikuwa naichukia na nilikuwa sitegemei kabisa kuitenda katika maisha yangu.
Nilivuta kumbukumbu ya maneno ya marehemu kipenzi changu Anna aliyoniambia kwenye ile ndoto niliyoota, ndoto ya kutisha. Katika maneno yake alinisisitiza sana nisiue wala kujiua kwani adhabu yake huwa ni kubwa mno.
Alinisisitiza nizidi kutenda mema huku nikiongeza upendo kwa watu wote wanaonizunguka ili siku zangu zikiisha duniani nikapumzike kwa amani na siyo kwa mateso.
Sasa mwanamke aliyekuwa mbele yangu alikuwa ananishawishi nianze kuua kwa ajili ya kupata utajiri, tena siyo kuua mara moja bali ni kuua kila mwaka mpaka pale maisha yangu yatakapofika kikomo duniani. Niliogopa sana.
Kibaya zaidi jambo lilikuwa limekaa kwenye njia panda, kama nisingefanya hivyo basi ningeuliwa mimi. Kweli maisha ni matamu sana mithili ya asali mwitu japokuwa ni mafupi zaidi ya watu wa Uturuki.
Hapo ndipo nilizidi kuumiza kichwa. Lakini kumbukumbu ya maneno ya marehemu Anna ilionekana kunipa nguvu. Nikajisemea kimoyomoyo kuwa ni bora nife kuliko kubeba dhambi mbaya na nzito kama hiyo, dhambi ya kuua.
Nikiwa katika kuwaza wazo lilinijia, nikaliona linafaa kulifanyia kazi. Nikataka kufumbua kinywa changu ili nieleze msimamo wangu juu ya jambo lililokuwa lipo mbele yangu. Kabla sijaongea chochote nilimuona Sharifa akisimama na kuniwekea mkono wake kichwani. Mwili wote ulisisimka, nikajihisi kama nimepigwa shoti ya umeme.
Alipotoa mkono wake juu ya kichwa changu aliniambia gari tuliyokuwa tumeenda nayo hotelini hapo imekuwa yangu kuanzia wakati huo. Pia akaniambia pesa zote zilizokuwemo kwenye brificase iliyokuwa mezani zote ni zangu.
Mara baada ya kuongea hivyo alinikabidhi funguo za gari zilizokuwa mezani. Kufumba na kufumbua alipotea ghafla, nikabaki peke yangu kwenye chumba hicho. Niliogopa sana.

                        **************************   

ITAENDELEA..........  

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 55

Kwa wasomaji wapya....
Brighton anajikuta akitupwa gerezani na kuhukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe baada ya kusingiziwa kumuua mpangaji wake kishoka. Hata hivyo mtu aliyemsingizia anaenda gerezani na kumtorosha huku akimwambia kuwa kuna masharti atampa baada ya kukamilisha hilo zoezi. Sasa Brighton tayari yupo uraiani na anachukuliwa na Sharifa na kupelekwa kwenye hoteli na kuanza kuambiwa jinsi utajiri wa marehemu kaka yake (yaani James) ulivyopatikana.......endelea

ILIPOISHIA TOLEO LILLOPITA...
Wakati nikiwa katika lindi la mawazo niligutushwa na sauti ya Sharifa. Alianza kwa kuniita jina langu.
“Brighton!”
“Naam!” Nami nilimwitikia.

SASA ENDELEA..........
“Usiwaze sana kwani kazi nzito ilishafanywa na kaka yako, unachotakiwa wewe ni kuikamilisha tu na utakuwa bilionea wa kuogopeka.” Alinyamaza kidogo kisha akaendelea.
“Daraja la kwanza utakuwa umeshalivuka kwani wazazi wa James ni wazazi wako, pia kufa kwake kutachukua nafasi ya ndugu wa karibu, kafara ambayo ilikuwa utolewe wewe. Kitakachohitajika kwako ni kuoa mke kisha mkishazaa mtoto unamtoa kafara akifuatiwa na mama yake, hapo utakuwa tayari umeshakamilisha daraja la pili.” Alipozi kidogo.
Wakati wote huo nilikuwa nimemsikiliza kwa makini. Baada ya kupozi kidogo aliendelea kuniambia kuwa nikishaimaliza daraja la pili lile lililokuwa linafuata ni mteremko. Daraja hilo ambalo ni daraja la tatu lilikuwa ni kumtoa kafara mtu mmoja kila mwaka, mtu huyo anaweza kuwa ni mfanya kazi wako ama ni mteja wako. Hiyo hatua ndiyo ilikuwa ni nyepesi kuliko zote kwani pale unamtoa mtu ambaye siyo ndugu wa karibu.
Hata hivyo bado ulikuwa ni mzigo mzito moyoni mwangu. Dhambi ya kuua nilikuwa naichukia na nilikuwa sitegemei kabisa kuitenda katika maisha yangu.
Nilivuta kumbukumbu ya maneno ya marehemu kipenzi changu Anna aliyoniambia kwenye ile ndoto niliyoota, ndoto ya kutisha. Katika maneno yake alinisisitiza sana nisiue wala kujiua kwani adhabu yake huwa ni kubwa mno.
Alinisisitiza nizidi kutenda mema huku nikiongeza upendo kwa watu wote wanaonizunguka ili siku zangu zikiisha duniani nikapumzike kwa amani na siyo kwa mateso.
Sasa mwanamke aliyekuwa mbele yangu alikuwa ananishawishi nianze kuua kwa ajili ya kupata utajiri, tena siyo kuua mara moja bali ni kuua kila mwaka mpaka pale maisha yangu yatakapofika kikomo duniani. Niliogopa sana.
Kibaya zaidi jambo lilikuwa limekaa kwenye njia panda, kama nisingefanya hivyo basi ningeuliwa mimi. Kweli maisha ni matamu sana mithili ya asali mwitu japokuwa ni mafupi zaidi ya watu wa Uturuki.
Hapo ndipo nilizidi kuumiza kichwa. Lakini kumbukumbu ya maneno ya marehemu Anna ilionekana kunipa nguvu. Nikajisemea kimoyomoyo kuwa ni bora nife kuliko kubeba dhambi mbaya na nzito kama hiyo, dhambi ya kuua.
Nikiwa katika kuwaza wazo lilinijia, nikaliona linafaa kulifanyia kazi. Nikataka kufumbua kinywa changu ili nieleze msimamo wangu juu ya jambo lililokuwa lipo mbele yangu. Kabla sijaongea chochote nilimuona Sharifa akisimama na kuniwekea mkono wake kichwani. Mwili wote ulisisimka, nikajihisi kama nimepigwa shoti ya umeme.
Alipotoa mkono wake juu ya kichwa changu aliniambia gari tuliyokuwa tumeenda nayo hotelini hapo imekuwa yangu kuanzia wakati huo. Pia akaniambia pesa zote zilizokuwemo kwenye brificase iliyokuwa mezani zote ni zangu.
Mara baada ya kuongea hivyo alinikabidhi funguo za gari zilizokuwa mezani. Kufumba na kufumbua alipotea ghafla, nikabaki peke yangu kwenye chumba hicho. Niliogopa sana.

                        **************************   

ITAENDELEA..........