Friday, November 8, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 41


ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA...
Nilizidi kuchanganyikiwa kwa kuona maisha yangu yakiandamwa na mikasa, mikosi na ndege mbaya kila wakati. Kichwa kilizidi kuuma.
SASA ENDELEA.......
Maisha ya gerezani yalizidi kusonga huku nikiwa nasubiri siku yangu ya kutundikwa kwenye kitanzi ifike, siku ambayo nilikuwa sijui tarehe yake, mwezi wala mwaka wake.
Huko gerezani nilishangaa sana kumkuta jamaa mmoja ambaye nilikuwa namfahamu. Jamaa huyo ni yule niliyekuwa nimemuuzia nyumba aliyokuwa kahongwa Neila, mwanamke aliyeuliwa na James baada ya kumuonyeshea utapeli wa mapenzi na nyodo za kila aina.
Nilishangaa sana kumkuta jamaa huyo aliyekuwa anajulikana kwa jina la Mack. Alikuwa kakaa gerezani kwa muda mrefu kiasi kwani alikuwa kashapewa mpaka unyapara wa humo gerezani.
“Kulikoni tena ndugu yangu na wewe umeletwa huku?” Lilikuwa ni swali la Mack siku ya kwanza kabisa kuingia jela mara baada ya kuniona.
“Matatizo makubwa ndugu yangu, hapa nilipo sina hata hamu! Na wewe lini tena humu na kipi kilichopelekea kuletwa sehemu hii isiyofaa?” nilimuuliza nikiwa na shauku kubwa ya kujua kilichokuwa kimemsibu.
Kabla ya kunijibu aliguna kisha akavuta pumzi ndefu na kisha  kuzishusha.
“Ni stori ndefu mdogo wangu, hebu anza kwanza wewe kunieleza mkasa uliokusibu mpaka ukaletwa humu.”
Niliamua kuanza kumsimulia jinsi mambo yalivyokuwa. Nikamweleza kinaga ubaga, hatua kwa hatua tangu kipindi nahama mji tuliokuwa tunaishi na kaka James.
Wakati namsimulia alikuwa katulia tulii huku akinisikiliza kwa umakini mkubwa. Nilipomaliza nikamuachia naye aweze kufunguka. Alianza kwa kusema,
“Kisanga chako hakina tofauti sana na kile kilichonitokea mimi.” Alitulia kidogo kumeza mate.
            Nilishtuka sana baada ya kusikia hivyo. Nikawa na hamu ya kusikia mambo yalivyokuwa huko. Aliendelea kuniambia kuwa mara baada ya kumuuzia nyumba ile alihamia. Akawa anaishi pale yeye na familia yake ambayo ilikuwa na jumla ya watu watatu, yaani yeye mwenyewe, mke wake na mtoto wake mmoja.
            Kabla hajamaliza hata mwezi kuna msichana alijitokeza na kumtaka ahame pale akidai kuwa nyumba ile ni yake. Baada ya kuambiwa hivyo hakutishika kwani ushahidi wote wa kuonyesha kuwa nyumba ile ni mali yake ya halali alikuwa nao.
            Mwanadada huyo alizidi kumwandama kwa kumtisha na vitisho kedekede. Pamoja na vitisho hivyo Mack aliendelea kukaidi madai ya mwanadada huyo.
            “Huyo msichana ulikuwa unamfahamu kabla?” Nilimtwanga swali hilo nikiwa najaribu kudadisi juu ya msichana huyo.
“Hapana! Nilikuwa sijawahi hata kumuona kabla ya hapo.” Mack alinijibu kama hivyo.
“Alisema yeye ni mwenyeji wa wapi?” Niliuliza tena.
“Alidai kuwa ni mwenyeji wa palepale mjini mtaa wa Matopeni. Lakini mimi niliona ni muongo kwani Matopeni nilikuwa mwenyeji kidogo na nilikuwa sijawahi kuona sura kama yake.”
            Niliona niachane na kuuliza uliza maswali kwani yalikuwa yanakatisha uhondo wa stori yenyewe. Nikamuacha Mack aendelee kunipa michapo hatua kwa hatua.
Aliendelea kueleza kuwa baada ya kukaidi mwanamke huyo hakuchoka kumghasi akimwambia ahame katika nyumba ile.
Baada ya Mack kuona kero imezidi aliamua kulipeleka shauri hilo kwenye uongozi wa serikali za mtaa ili wamsaidie kuipata suluhu. Alipowaeleza viongozi hao walimwambia aende na mlalamikaji huyo ili wakapate kuyasikiliza malalamiko yake.
“Nikaenda kumtafuta mtaa wa Matopeni lakini sikufanikiwa kumuona. Kila niliyemuuliza alisema hamfahamu.” Alisikika Mack akiniambia.
Sikutaka kutia swali katika maelezo yake, nikachombeza tu kwa kumwambia aendelee, naye akaendelea.
“Baada ya kumkosa nilirudi nyumbani. Nikaamua kumsubiri atakapokuja nimkamatishe na kumpeleka kwenye ofisi za serikani za mtaa.”
            Huku nikimsikiliza lakini kwenye ubongo wangu kulikuwa na mjadala mzito uliokuwa ukiendelea. Suala la kulifahamu jina la msichana huyo ndiyo lilikuwa nimetawala kwenye akili yangu. Mawazo yangu yote yalikuwa yananituma kuwa piga ua galagaza yule msichana alikuwa ni Sharifa, msichana aliyenisababishia matatizo ya kupatikana na hatia ya kuua wakati sijaua.

JE, MSICHANA HUYO NI NANI NA KWA NINI ANAMSUMBUA MACK? USIKOSE TOLEO LIJALO.

No comments:

Post a Comment