Wednesday, November 27, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 48


            Brighton anaota ndoto ya ajabu akiwaona watu waliokufa siku nyingi kwa kujiua wakiwemo mzee Mboma, Patrick, James na Anna. Baada ya ndoto hiyo anazongwa na mwanadada Sharifa anayemsababishia kesi ya mauaji ya mpangaji wake, yaani Kishoka. Kesi inaunguruma mahakamani kisha anajikuta akihukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe kwa kosa la mauaji ya Kishoka, kosa ambalo alikuwa hajalitenda. Akiwa gerezani akisubiri tarehe za kunyongwa anakutana na Mack, jamaa aliyekuwa amenunua nyumba iliyokuwa ya marehemu James, naye Mack anaanza kumhadithia kisa kilichompelekea afungwe jela.
Kwa kusimuliwa na Mack, Brighton anayasikia mengi kuhusu mali alizokuwa amerithi kutoka kwa marehemu kaka yake kwa kila aliyekuwa amemuuzia aliishia kupatwa na matatizo akiwemo Mack mwenyewe. Hatimaye siku ya kunyongwa inafika kweli, hata hivyo anajikuta anakolewa kimiujiza na msichana aliyemsingizia kuua, yaani Sharifa, anatolewa gerezani na kuwa huru kabisa.
Anaporudi kwake anakuta nyumba yake ishauzwa na mtu aliyekuwa amemwachia.  Sasa endelea...................

Hata hivyo nilijishauri mwenyewe kuwa kama ningeenda kwenye nyumba hiyo basi ningeonekana kwa watu wengi, na hofu yangu ilikuwa ni kuvuja kwa siri ya kutoroka gerezani.
            Nilijua fika dunia haina siri na walimwengu hawana dogo. Kitendo cha kuniona tu basi wangeanza kuhoji kutaka kujua kulikoni. Watu wengi walikuwa wanajua fika kuwa mimi nilihukumiwa kifo, sasa kuonekana pale mtaani kungeweza kuzua gumzo na kuniletea matatizo mengine tena, huenda ningejikuta nakamatwa na vyombo vya dola.
            Hata wakati naenda kwenye nyumba yangu hiyo nilienda kwa kujificha ficha sana ili nisionekane kwa watu wa mtaa ule. Lengo langu lilikuwa ni kwamba nifike kwa Mapara na kumwambia tufanye mipango ya kuhama mji huo kinyemera na kuenda katika mji mwingine ambao ingekuwa vigumu watu kunishtukia.
            Akili yangu ilikuwa imenituma kuuza kila kitu kisha kutimkia mji wa mbali ambako ningeweza kuishi kwa raha zangu bila kushtukiwa mpango wangu wa kutoroka jela.
            Sasa kitendo cha kuambiwa Mapara hakuwa anaishi hapo tena kiliichokesha akili yangu mara dufu. Nikawa nawaza cha kufanya bila kupata majibu.
            Jamaa baada ya kuniona nimekaa kimya kirefu nikiwaza kwa kina huku nikipiga miayo mfululizo isiyo na idadi; aliamua kuzama ndani kisha akafunga geti ‘paa!’ Nilibaki pale nje peke yangu nikiwaza na kuwazua bila kupata muafaka wa mawazo yangu.
            Hatimaye niliamua kuchukua maamuzi ya hatari kwani sikuwa na jinsi.
‘Potelea mbali kifo hakina breki, ngoja niende hapo hapo alipokuwa kapanga Mapara ili nikajaribu kuulizia kama bado kapanga hapo au la!’ Nilijishauri na kuanza kuondoka.
            Kwa jinsi nilivyokuwa nimekonda ilikuwa ni vigumu sana kwa mtu yeyote aliyekuwa akinifahamu kugundua kwa haraka kuwa ndiyo mimi. Ukizingatia miaka mingi sikuwepo mtaani hapo na pia watu walikuwa wameshanifuta hata katika fikra zao kutokana na hukumu niliyokuwa nimepewa, yaani hukumu ya kunyongwa; basi niliweza kupishana nao kama vile hatujuani.
            Nilienda moja kwa moja mpaka kwenye nyumba alimokuwa kapanga Mapara. Nikaingia mpaka ndani ya nyumba hiyo. Moja kwa moja nilienda mpaka kwenye chumba alichokuwa akikaa.
            Nilipogonga ilisikika sauti ya mwanamke ikiniitikia.
‘Huyu jamaa kashavuta jiko nini?’ yalikuwa ni mawazo yangu baada ya kuisikia sauti ya mwanadada huyo.
            Mara mwanamke mrembo alifungua mlango na kutoka kidogo kisha akasimama mlangoni kwa mtindo wa kuegemea mlango. Alikuwa ndani ya kanga tu lakini kanga hizo zilikuwa ni mbili, ya kwanza ilikuwa imeanzia kifuani kuyafunika maziwa na ya pili ilikuwa imeanzia kiunoni.
            Nilimsabahi naye akaitikia. Kilichofuata baada ya salamu ni kumuuliza habari za Mapara.
“Mh! Mapara, mbona simfahamu?” Alijibu mwanamama huyo aliyekuwa na uzuri wa shani.
            Baada ya kujibiwa hivyo moyo wangu ulishtuka utadhani umepigwa shoti ya umeme. Tumbo likawa joto kwani dalili za mambo kuzidi kuniwia ugumu zilikuwa zinajidhihirisha waziwazi. Wahenga walisema dalili ya mvua ni mawingu, pia mwanzo wa ngoma siku zote huwa ni lele.
            “Kwani wewe siyo mpangaji wa siku nyingi hapa?” Nilimhoji  mama huyo.
“Ndiyo sina siku nyingi hapa, nina miezi kama mitano hivi tangu kuhamia kwenye hiki chumba.”
“Ndiyo maana, kwa maana Mapara alikuwa kapanga kwenye chumba hikihiki na  ni muda mrefu umepita tangu nifike kumsabahi.”
“Labda muulize kaka wa kwenye chumba  kinachofuata kwani huwa nasikia yeye ndiyo mkongwe zaidi hapa.”
“Sawa, asante kwa msaada wako.”
“Wala usijali, karibu tena.”
“Nimekaribia.” Nilijibu kisha nikaondoka kwa hatua za taratibu kabisa mpaka kwenye chumba kilichofuata.
            Kwa adabu zote nilianza kuugonga mlango. Sikujibiwa chochote. Mle ndani kulikuwa na mdundo wa redio uliokuwa ukikita kwa sauti utadhani ni ukumbi wa disko.
            Niliamua kugonga tena kwa kuamini kuwa labda nilipogonga kwa mara ya kwanza hawakusikia kutokana na makelele ya redio. Tena safari hii nililazimika kuukaza mkono ili kuwafanya waliokuwemo humo ndani wanisikie.

JE, HICHO CHUMBA ANAISHI NANI? NA JE, BRIGHTON ATAPATA UFUMBUZI WA MASWALI YAKE? USIKOSE KUSOMA TOLEO LIJALO.    

No comments:

Post a Comment