Thursday, October 10, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 27




ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA....
“Yangu macho na masikio siku hiyo, lakini mimi nimeshamnyanyulia mikono huyo ibilisi. Nashangaa sijui kwa nini kaniandama sana na kunisababishia ndege mbaya katia maisha yangu, kanipotezea dira ya maisha kabisa, isitoshe hata hatima yangu haijulikani.” Nilijikuta nikiongea kwa uchungu huku nikionyesha kukata tamaa kwa hali zote.
SASA ENDELEA.......
            “Tatizo lako wewe ni mwepesi mno wa kukata tamaa. Hebu hakikisha unapambana mpaka dakika ya mwisho.”
“Nitapambana vipi kaka wakati hali ninavyoiona inazidi kuelekea kubaya tu. Hebu jiulize hizo alama za vidole vyangu zimeonekanaje kwenye mwili wa marehemu na kwenye kisu wakati sikuwahi hata kugusa?”
“Huenda ulishika bila kijielewa kutokana na kuchanganyikiwa na tukio.”
“Hakuna kitu kama hicho kaka, mimi hata nichanganyikiwe vipi lakini huwa najielewa.”
“Basi yote hayo tumwachie Mungu, yeye ndiye atakayeamua kuwa tushindwe au tushinde hii kesi.”
“Mimi nahisi hata Mungu kashanipa kisogo, haya siyo matatizo ya kwanza kwangu, walianza wazazi wangu wakafariki, kipenzi changu Ana naye akanitoka kimzahamzaha. Haikuishia hapo tu, kaka James ambaye alikuwa ndiyo nguzo yangu ya pekee iliyokuwa imebakia, naye akafariki dunia, tena kifo cha ghafla ghafla tu.” Nilijikuta nikimshtakia Mungu kwa wakili huku machozi yakianza kunibubujika kwenye mifereji ya mashavu yangu.
            Ndipo mlango ulipofunguliwa kisha askari magereza akaingia na kumtaka wakili aondoke kwani muda wa kuendelea kuongea na mimi ulikuwa umefikia kikomo.
            Wakili aliniaga na kuniambia atakuja kunipa taarifa pale tarehe ya kesi yangu itakapopangwa. Aliondoka na kuniacha nikifutafuta machozi ambayo yalikuwa yameshaanza kukolea kutokana na kuyaamsha machungu yaliyokuwa yamejilaza moyoni; machungu ya kuondokewa na watu wangu muhimu katika hii dunia ambao ni wazazi wangu, kaka James na kipenzi changu Anna.
            Mawazo juu ya msichana huyo ambaye nilikuwa nimembatiza jina la Ibilisi yalianza kuzunguka kunako kichwa changu. Hata hivyo sikuweza kupata jibu ni kwa nini msichana huyo alikuwa ameniandama kiasi kile.
            Niliendelea na maisha ya gerezani ingawa nilikuwa ni mahabusu. Mpaka muda huo nilikuwa bado sijayazoea kabisa maisha ya huko, ilikuwa ni ngumu sana kwangu kuyazoea maisha ya huko.
Siku moja kabla ya kesi yangu kuendelea wakili alikuja kunipa taarifa. Hata hivyo alipokuja aliniambia habari nyingine ambayo ilizidi kunichanganya zaidi.
Alisema kuwa siku aliyotoka kuongea na mimi kwenye hospitali ya magereza alikutana na msichana aliyekuwa akitusumbua katika kesi hiyo. Msichana aliyekuwa amenisingizika kuwa nimeua wakati sijaua.
MH! HAYA SASA, WAKILI WA BRIGHTON ANAKUTANA NA YULE  MSICHANA HATARI. JE, ATAAMBIWA NINI? USIKOSE TOLEO LIJALO!

No comments:

Post a Comment