Thursday, October 24, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 35



ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA....
Mpaka anafikishwa hospitali mama yangu alikuwa hajielewi hata kidogo. Alikuwa kaumia vibaya sana

                        ************************
SASA ENDELEA.......
Taarifa za ajali ziliwafikia wazazi wa mama majira ya mchana, walipigiwa simu na mwalimu mkuu wa shule aliyokuwa akisoma mama na kuambiwa kuwa mtoto wao kapata ajali katika moja ya basi lililokuwa likienda mji jirani muda mchache baada ya kutoka mjini hapo.
Walishangaa sana kusikia habari hiyo, wakaanza kujiuliza mtoto wao alikuwa kapanda gari hilo kuelekea wapi! Walipojaribu kumuuliza mwalimu kuwa labda alikuwa na taarifa na hiyo safari naye aliruka kimanga na kudai hana ajualo.
Hapo ndiyo wazazi walizidi kuchekecha akili wakijiuliza kuwa mtoto wao alikuwa anasafiri kuenda wapi na ni kwa nini aondoke bila ya kuaga ama kutoa taarifa?
Hata hivyo hilo halikuwa la kujadili sana kwa wakati huo, kilichokuwa cha msingi kwa wakati huo ni kwenda hospitali kumuona mtoto wao, hata hayo maswali yao yote yangeweza kupata majibu hukohuko kwa kumuuliza mwenyewe.
“Au labda alikuaga wewe lakini unanificha tu?” Ilikuwa ni sauti ya babu yangu akimuuliza mkewe wakati gari yao inachoma mafuta kuelekea hospitali aliyokuwa kalazwa mama.   
“Aka! Mimi sijui chochote kuhusu safari hiyo, atakuwa kajiamulia mwenyewe.”
“Maana nyie wanawake wakati mwingine huwa mnakula njama na watoto wenu hasa hasa watoto wa kike.”
“Mimi siwezi nikafanya ujinga kama huo.”
            Mara baada ya maongezi hayo ukimwa ulitawala katika safari hiyo. Hawakuchukua muda wakawa wamefika kwenye hospitali ambayo majeruhi na maiti waliopatikana katika ajali ya asubuhi walikuwa wamehifadhiwa.
            Wakaanza kumtafuta mtoto wao kwenye wodi walizokuwa wameweka majeruhi. Kwa bahati nzuri hawakuhangaika sana wakawa wamemuona, ila alikuwa bado hajazinduka.
            Fahamu zilimrudia muda wa usiku, akashangaa kujiona yupo hospitali huku akiwa na majeraha mwili mzima. Hata hivyo tukio zima alilikumbuka mara baada ya kuvuta kumbukumbu. Ndipo akakumbuka kuwa  alikuwa akitoroka kwa kuogopa kugundulika nyumbani ya kuwa ni mjamzito.
            Akili yake ikamtuma kuwa huo ndiyo ulikuwa ni muda muafaka wa kuomba radhi kwa wazazi wake kwani hata zile hasira za baba yake zisingewaka sana juu yake kwa vile alikuwa anaumwa na yupo hospitali. Alijua fika mpaka kuja kupata nafuu baba yake atakuwa kashapunguza hasira kama siyo kuisha kabisa na hapo asingekipata kichapo cha paka mwizi.
Kesho yake asubuhi baba na mama yake walikuwa wameshafika hospitali hapo kumjulia hali. Kwa wakati huo hali yake ilikuwa inaendelea vizuri ingawaje alikuwa bado ana maumivu makali.
Ndipo alipopata fursa ya kuwaeleza wazazi wake kinaga ubaga juu ya tatizo lililokuwa likimsumbua kiasi kwamba mpaka akachukua uamuzi wa kutoroka nyumbani.
“Huyo bwege aliyekupa ujauzito huo ni nani na yuko wapi?” Lilikuwa ni swali la baba yake baada ya kusikia hivyo.
“Kashakimbia, hicho nacho ndicho kimechangia kunifanya nichukue uamuzi huo kwani ana wiki mbili sasa hayupo.” Alijibu mama yangu kwa shida.
“Jamani, mimi sioni sababu yoyote ya kuanza kuyajadili mambo haya huku hospitali, haya mambo ni ya kuyajadili tukiwa nyumbani.” Aliingilia kati bibi yangu.
            Hata hivyo mama alikuwa na hofu kwamba maelezo hayo akiyatoa wakiwa nyumbani yanaweza yakaupandisha ‘mzuka’ wa baba yake na kuanza kumshushia kichapo. Lakini alipiga moyo konde na kusema litakalokuwa na liwe. Kizuri zaidi alikuwa tayari kashatoa utangulizi wa jambo hivyo hasira za baba yake zisingekuwa nyingi sana.
            Baada ya wiki moja mama yangu aliruhusiwa kutoka hospitali, afya yake ilikuwa inaimarika vizuri ingawaje majeraha mengine yalikuwa hayajapona ikiwemo mkono wake ambao ulikuwa umevunjika hivyo alikuwa kawekewa ‘p.o.p’
            Siku hiyo hiyo alipofika nyumbani hakutaka kulaza damu, aliianzisha tena mada kwa kuwaomba msamaha wazazi wake kwa kile kilichokuwa kimejitokeza.
            Suala hilo liliongelewa na kufikia muafaka, akawa ameambiwa asiwe na wasiwasi kwani kuteleza si kuanguka.
“Usiwe na wasiwasi mwanangu mimi na mama yako tumeshakusamehe, ila ole wake huyo mpumbavu aliyejifanya rijali apatikane, hapo ndiyo atajua kuwa kumbe koti huwa halichomekewi, atajuta kuzaliwa.” Mzee wa kazi alimalizia kuongea kisha akaondoka zake.
            Mama aliendelea kuilea mimba yake akiwa nyumbani. Mpaka miezi tisa ilipoada ndipo alipojifungua mtoto wa kiume ambaye ndiyo alikuwa kifungua mimba wake, huyo hakuwa mwingine bali ni kaka James.
            Kuzaliwa kwa kaka James ndiyo kulikuwa hivyo. Wakati huo mimi nilikuwa bado sijafikiriwa hata kuiona hii dunia. Nilikuwa bado nipo mbinguni nikicheza na kufurahia tu na malaika.
ITAENDELEA......

No comments:

Post a Comment