Monday, October 7, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 25




ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA....
Jaji aliiahirisha kesi na kutaja tarehe nyingine ambayo ingeendelea kusikilizwa. Nilitolewa kizimbani na kupelekwa kwenye karandinga la magereza tayari kabisa kwa kurudishwa mahabusu.        
SASA ENDELEA.......
Ilikuwa ni kesi iliyonipa wakati mgumu sana kwa kipindi chote nilichokuwa mahabusu nikisubiri hatima yake. Kila wakati nilikuwa siishi kuwa na wasiwasi mithili ya mbuzi wa shughuli.
            Wasiwasi pamoja na kuwaza huko kulizidi kuifanya afya yangu izidi kuwa mgogoro zaidi ya vile ilivyokuwa awali. Niliiona kesi inapelekwa polepole sana, nikawa natamani bora nihukumiwe ili nijue moja, kama kusubiri kunyongwa ama kuponea kwenye wokovu wa ngamia kupenya kwenye tundu la sindano.
            Pamoja na maneno ya wakili wangu bwana Jonas Mlyanyama ya kunitia moyo na kunihakikishia kuibuka kidedea katika kesi hiyo, bado nilikuwa naona kama ananikebehi na kunipa faraja za kijinga kwa vile niliamini kabisa kuwa hata yeye alikuwa anauona ugumu wa kesi yangu ulivyokuwa.
            Kibaya zaidi sikuwa hata na shahidi ambaye angesimama kizimbani na kujaribu kunitetea. Kesi yenyewe ilikuwa imejaa utata mtupu. Hata wewe mpenzi msomaji uliona wapi alama za vidole zionekane kwenye kitu ambacho hukuwahi hata kukishika? Huo ni utata, kama siyo kubambikiwa basi ni kiini macho.
            Tarehe ya kusikilizwa tena kesi yangu iliwadia. Siku hiyo tena upande wa mashitaka ulitakiwa kupeleka mashahidi wake wawili. Shahidi wa kwanza kupanda kizimbani kutoa ushahidi alikuwa ni Daktari aliyeufanyia uchunguzi mwili wa marehemu Kishoka.
            Akiwa kizimbani huku akiongozwa na mwendesha mashitaka, daktari huyo alieleza jinsi alivyoupokea mwili wa marehemu Kishoka na kuufanyia uchunguzi. Baada ya hapo alitoa maelezo ya ripoti ya postimotam kabla ya kuwasilisha nakala ya ripoti hiyo kwa Jaji.
            Wakili wangu hakuwa na maswali mengi sana ya kumuuliza shahidi huyu hivyo hakutumia muda mrefu sana kumhoji alipokuwa kwenye kizimba cha kutolea ushahidi.
            Ripoti ya daktari huyo ilikiri kuwa kweli Kishoka aliuawa kwa kukatwa na kitu chenye ncha kali mpaka akapoteza uhai wake.
            Baada ya shahidi huyo kutoa ushahidi, upande wa mashitaka ulitakiwa kupeleka shahidi mwingine. Shahidi aliyekuwa ameandaliwa ni mmoja wa askari waliokuwa wamekuja nyumbani kwangu kuja kunikamata baada ya kupewa taarifa za kifo cha Kishoka.
            Nilimuona mwendesha mashtaka ambaye ni wakili wa serikali akisimama na kumwambia jaji kuwa shahidi aliyetakiwa kupanda kizimbani haonekani na huku alikuwepo wakati mahakama inaanza.
            “Hata hivyo kuna shahidi mwingine kajitokeza ambaye ni muhimu sana katika kesi hii. Mtu mwenyewe ni yule mwanamke aliyetoa taarifa za awali kituo cha polisi kuhusiana na kifo cha Kishoka.” Nilimsikia mwendesha mashtaka akimwambia jaji.
            Moyo ulinilipuka puu baada ya kusikia kauli hiyo. Tumbo langu likachemka ghafla huku maswali mia mia nikijiuliza ya kuwa huyo mtu aliyetoa taarifa kituoni akinisingizia kuua ni nani.
            Hata hivyo kwa upande mwingine nilifurahi ili nimuone mtu huyo mwenye moyo wa kinyama na roho ya kishetani kwa kunisakizia kwesi ya mauaji ilhali sikuua.
            Baada ya jaji kuruhusu shahidi huyo apande kizimbani, nilimuona dada mmoja akiinuka na kuanza kutembea mwendo wa maringo kuelekea kwenye kizimba cha kutolea ushahidi.
            Kitendo cha kumuona mwanadada huyo kilinifanya nianze kuhisi kupumua kwa shida huku mwili wangu ukianza kuishiwa nguvu. Pumzi zilizidi kubana, ghafla nilijiona nikianguka mzima mzima huku macho yangu yakipoteza upeo wa kuona. Kabla sijafika chini niliacha kujitambua na kupoteza fahamu ghafla.

No comments:

Post a Comment