Monday, October 28, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 37



ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA...
Mpaka namaliza kidato cha sita alikuwa ni tajiri wa kuogopeka mji mzima. Alikuwa na magari mawili ya kifahari na nyumba mbili za kifahari.
SASA ENDELEA.......
Tulihamia kwenye nyumba moja na kuanza kuishi pale. Mambo yalizidi kuwa safi kwa kaka James. Nilizidi kupata wasiwasi kwa jinsi utajiri wake ulivyokuwa ukiongezeka kila kukicha.
Kati ya miradi mikubwa aliyokuwa nayo ni pamoja na kampuni ya usafirishaji ambayo ilikuwa na malori ya kusafirisha mizigo ndani na nje ya nchi. Ilikuwa ni kampuni kubwa iliyokuwa imeajiri wafanyakazi wengi mno.
                       
************************
           
            Mahusiano ya kimapenzi kati ya kaka James na mwanadada Neila yalizidi kupamba moto. Hapo awali mimi nilikuwa sijui chochote kuhusu uhusiano huo kwani alikuwa hajanitambulisha.
            Ilifikia kipindi akanitambulisha rasmi na kuniambia Neila ndiye alikuwa tashtiti wake, nyonga mkalia ini kama wasemavyo watu waliobobea kwenye mahaba.
            Sikuwa na pingamizi juu ya uhusiano wao ila niliwasisitiza tu watangulize uaminifu mbele pamoja na upendo wa dhati kwa ujumla.
            Mapenzi yao yaliendelea kukolea kila siku iliyoenda kwa Mungu. Hapo ndipo Naila alianza katabia ka kudai makuu ikiwemo kukabidhiwa nyumba kununuliwa gari zuri la kifahari pamoja na kufunguliwa akaunti yenye hale nyingi.
Hayo yote hayakuwa tatizo kwa kaka James maana pesa ilikuwa chekwa. Kila alichotaka mtoto wa watu alitimiziwa, mpaka nikaanza kumuonea wivu kwani alizidi mno kumpiga ‘kibomu’ kaka yangu. Naye James kwa kutaka kumkoleza mwanadada huyo hakuona ajabu kuvitoa vimilioni kwa ajili yake.
            Siku chache baada ya kaka James kumkamilishia mambo hayo; mwanamke huyo alibadilika ghafla na kuanza kufanya vimbwanga vilivyokuwa vikileta kichefuchefu mbele ya James.
            Tabia ya mwanamke huyo ilizidi kuwa mbaya, akawa anamletea kiburi kaka yangu huku akimpa masharti mengimengi ikiwa ni pamoja na kuwa anatoa taarifa akitaka kwenda kwake.
            Siku moja kaka James alienda kwa mwanamke huyo bila taarifa. Alichokikuta huko hakuamini kwa macho yake kwani alikikuta kidume kimejilaza kitandani kikiwa na mwanamke huyo huku wakiwa kwenye pozi la kimahaba.
            Ghadhabu zilimjaa sana kaka James baada ya kuyashuhudia yale mambo.
“Nini hicho unafanya mpenzi wangu?” Alisikika James kwa sauti ya kitetemeshi akionyesha ni jinsi gani hasira ilivyokuwa imepanda.
“Nani mpenzi wako?” Aliuliza mwanamke huyo kwa jeuri na nyodo za kila aina.
Kauli hiyo ilizidi kuipandisha hasira ya James. Hapo ndiyo alipojua ya kwamba mwanamke huyo ni nyoka ndumilakuwili mwenye sumu kali.
“Sikia nikwambie James; kama kusoma hujui basi jaribu hata kuangalia picha! Wewe ni zilipendwa ndugu yangu, tangu lini mavi ya kale yakanuka?. Mwanaume mwenyewe upo kianalojia utarandana vipi na mimi nipo kidigitali zaidi? Sasa nakutangazia rasmi leo kuwa sikupendi na sikuhitaji, na huyu unayemuona hapa ndiye mwanaume ninayempenda kwa dhati ambaye anastahili kuniona. Upo hapo? Hii ndiyo habari ya mjini babu wee!” Alizidi kutamba mwanamke huyo kisha akamalizia kicheko cha kishambenga,
“Heheheeeyah!”
“Kefle! Unajifanya mjanja na kuniona bwege mimi, sasa anza kusali sala zako za mwisho kwani uhai wako naukatisha sasa hivi?” Alidakia James kwa sauti ya juu iliyowashitua Neila na jamaa yake aliyekuwemo humo ndani.
Siyo sauti ya juu pekee iliyowafanya waduwae bali ni pamoja kitu alichokuwa amekishika mkononi. Kitu hicho hakikuwa kingine bali ni kidubwasha mithili ya kipaja cha kuku kilichoundwa kwa madini shaba. Alikuwa ameshika bastola.
Mwanamke yule alianza kutetemeka na kuanza kuomba msamaha kwa James, kwa bahati mbaya alikuwa amechelewa! Bila ya huruma James alikitekenya kitufe cha kufyatulia risasi kisha akamtwanga mwanamke huyo ya kichwa.
Huku akiwa anatweta kwa hasira aliisukuma risasi nyingine ambayo ilimpata yule jamaa aliyekuwa akijaribu kulamba asali kwenye mzinga wa James.
Risasi hiyo nayo ilimpata barabara kijana huyo, ikapenya kupitia kwenye paji lake la uso na kumfanya naye aanguke chini. Hakuchukua muda akawa amerudisha jezi ya kuendelea kuishi kwa mwenyezi Mungu, ikawa ni kwa heri mwalimu!
Mpaka hapo dhambi ya mauaji ya watu wawili kwa mpigo ilianza kumtafuna kaka James. Hofu na woga vilitanda katika moyo wake, akaanza kuona kesi ya mauaji ya watu wawili ilikuwa inamkabili.
Baada ya kuwaza kidogo alikumbuka kuwa bastola yake ilikuwa imebakiza risasi moja ndani. Ndipo alipoamua kujimaliza na yeye kwa kujipiga risasi.
ITAENDELEA....

No comments:

Post a Comment