Tuesday, October 15, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 30



ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA....
“Haya bwana wewe wasema, mimi nitapeleka taarifa kama ulivyotaka.” Alimalizia mjumbe huyo na kuondoka zake.
SASA ENDELEA.......
            Siku ayami zilipita, ukakaribia kuisha mwezi bila kupata taarifa zozote za kuendelea kwa kesi yangu kutoka mahakamani. Kadri siku zilivyozidi kwenda nilizidi kuingiwa na ujasiri wa kuja kukabiliana na mwanamke huyo siku tutakayokuwa kizimbani. Tena nikawa na shauku kubwa ya kumbana na kumhoji maswali, ukizingatia kauzoefu kakuhoji maswali nilikuwa nimeshaanza kukapatapata.
            Nilijikuta napania kumkaba maswali ya kufa mtu mwanadada yule. Japokuwa nilijua fika kuwa uwezekano wa kuwa bubu kama ilivyokuwa kwa wakili Mlyanyama ulikuwepo. Lakini sikujali kutokana na kuchoka na vimbwanga vya mwanamke huyo.
            Nikiwa mahabusu nilizidi kujipanga kwa maswali ya kwenda kumkabili huku pointi zangu nikizipangilia kiuanasheria. Nikawa nimeandaa maswali mithili ya gwiji la mawakili.
            Siku moja nikiwa sina hili wala lile nilipewa taarifa kuwa kesi yangu ingesikilizwa tena wiki moja mbele. Niliingojea kwa hamu siku hiyo huku nikiamini kuja kuushangaza umati wa watu wote watakaohudhuria siku hiyo mahakamani kwa kuuliza maswali yenye mantiki na yaliyosimama kisheria.
            Wiki moja haikukawia, nilitinga ndani ya kizimba cha mshtakiwa huku upande wa mashtaka ukimpandisha mwanadada Sharifa kuendelea kutoa ushahidi.
“Kwa vile shahidi alitoa maelezo siku tuliyomalizia kusikiliza kesi hii, sasa upande wa utetezi utaendelea kumuuliza maswali.” Ilikuwa ni sauti ya jaji.
            Bila kuchelewa wala kuzubaa nikakohoa kidogo kuisafisha sauti yangu, na baada ya hapo nikamfakamia kwa maswali shahidi huyo.
“Ulisema jina lako unaitwa nani vile?”
“Sharifa.”
“Sharifa unaweza ukaeleza mbele ya mahakama ulikuwa na uhusiano gani na Kishoka?”
“Ni ndugu yangu.”
“Ndugu yako kivipi?”
“Kaka yangu!”
“Kabla ya hii kesi mimi ulikuwa unanifahamu?”
“Ndiyo!”
“Ulikuwa unanifahamu ki vipi?”
“Nilikuwa nakufahamu kama mmiliki wa nyumba alipokuwa amepanga kaka yangu.”
“Siku ya tukio ilikuwa ni mara yako ya ngapi kufika hapo kwangu?”
“Ilikuwa ni mara ya kwanza?”
“Sasa mimi ulinijulia wapi wakati ilikuwa ni mara yako ya kwanza kuja kwangu?”
“Nilikujulia mitaani.”
“Wakati unaniona mitaani nilikuwa na nani?”
“Ulikuwa peke yako?”
“Sasa ukajuaje kuwa mimi ni mwenye nyumba wa pale anapoishi kaka yako?”
“Nilijua tu!”
“Sharifa, nikikuambia kuwa wewe unajaribu kutunga uongo uwe ukweli nitakuwa nadanganya?”
“Ndiyo utakuwa unadanganya.”
“Ngoja nikwambie kitu, mimi Kishoka nilikuwa namjua kuliko mtu mwingie hapa, siri zake zote alikuwa akiniambia, na kati ya siri alizoniambia ni kwamba hana ndugu hata mmoja katika nchi, sasa wewe unadai kuwa ni ndugu yake kutoka wapi?”
“Labda alikudanganya, lakini mimi ni ndugu yake.” Alijibu Sharifa.
“Wewe unajishughulisha na nini?”
“Mimi ni fundi cherehani!”
“Siyo mpiga picha?”
“Siyo!”
“Siyo mwandishi wa habari?”
“Siyo!”
“Na wala siyo mtalii?”
“Nimekwambia mimi ni fundi cherehani?” Alitamka Sharifa kwa ukali.
“Usiwe mkali Sharifa. Sasa ilikuwaje siku hiyo utembee na kamera? Au ulikuwa unajua kwamba ukifika kwa Kishoka utakuta tukio kama hilo upige picha za ushahidi?”
“Mimi huwa na kawaida ya kutembea na kamera ili kuchukua matukio muhimu pale inapobidi.”
            “Tulipoonana na wewe kule ufukweni siku moja kabla ya tukio la kuuawa kwa Kishoka ulikuwa na kamera?”
“Sijawahi kuonana na wewe ufukweni?”
“Kwa nini kesho yake asubuhi ulikuwa unatusumbua na Kishoka ukigonga geti na kupotea kimiujiza?”
“Sikuwa mimi?”
“Alikuwa nani?”
“Mimi sijui.”
ITAENDELEA.......

No comments:

Post a Comment