Saturday, October 26, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 36

ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA....
Kuzaliwa kwa kaka James ndiyo kulikuwa hivyo. Wakati huo mimi nilikuwa bado sijafikiriwa hata kuiona hii dunia. Nilikuwa bado nipo mbinguni nikicheza na kufurahia tu na malaika.
SASA ENDELEA.......
Baada ya kujifungua mama yangu hakupata tena nafasi ya kuendelea na masomo ya sekondari kwani huo mfumo umekuja miaka ya hivi karibuni. Zamani ukinasa huku bado unasoma basi hiyo ndiyo nitolee tena.
Haikuwa kama siku hizi ambapo msichana akipata mimba yungali anasoma anaruhusiwa kwenda kuilea mimba kisha akishajifungua anaendelea na masomo. Miaka ile haikuwa hivyo.
Hata hivyo mama yangu alikuja kujiunga na ualimu wa UPE enzi zile rais wa kwanza wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania hayati Mwl. Julias Kambarage Nyerere alipotangaza elimu ya UPE.
Kwa wale wenzangu na mimi ambao wamezaliwa juzijuzi  kuelekea kwenye mfumo wa digitali, maana ya UPE ni mpango ulioanzishwa na aliyekuwa rais wa kipindi hicho hayati Baba wa taifa Mwl. Nyerere ambao ulitaka kila mtoto wa kitanzania asome elimu ya shule ya msingi.
Hapo ndipo ulipotokea upungufu mkubwa wa walimu wa shule za msingi kiasi kwamba walimu waliokuwa wametoka vyuoni wakawa hawakidhi mahitaji.
Ndipo serikali ilipotangaza nafasi za ualimu hata kwa wale waliokuwa wameishia njiani na kushindwa kumaliza kidato cha nne pamoja na wale waliokuwa wamemaliza darasa ya saba nao walichukuliwa na kupewa jukumu ya kuwa walimu.
Kati ya hao walimu wa UPE na mama yangu naye alibahatika kuwamo. Akawa amepangiwa shule ya kufundisha.
Ilipita miaka kadhaa. Huku akiwa mwalimu alipata mume na kumuoa. Ndipo nilipozaliwa mimi.
Wakati huo kaka James alikuwa akiishi na wazazi wake na mama, yaani namaanisha kwa bibi na babu. Mpaka walipokuja kufariki ndipo alipochukuliwa na mama na kukaa pamoja katika familia moja.
Baba yangu alimchukulia kaka James kama alivyokuwa akinichukulia mimi, yaani alimlea kama mwanae wa kumzaa wakati alikuwa ni baba yake wa kufikia.
Hapakuwa na ukambo ukambo hapo, baba yangu alikuwa kapenda boga pamoja na maua yake. Alikuwa tofauti kabisa na baadhi ya wanaume ama wanawake wengine wanaowachukia watoto wa kambo.
Kama zawadi alituletea wote bila ya upendeleo, kama adhabu alitoa bila ya kupendelea, kama ni mapenzi basi alitupatia mapenzi mema wote wawili.
Kaka James hakuwahi kuwa na upweke kwa kulelewa na baba wa kambo. Alikuwa akithaminiwa kama kawaida, hakika maisha yake yalikuwa ni ya furaha siku zote.
Nadhani upendo tuliokuwa tukiupata kutoka kwa baba na mama ndiyo ulioimarisha uhusiano wetu na udugu wetu uliokuwa wa kushibana kama vile mapacha.
Hata hivyo furaha yetu ilikuja kubadilika na kuwa majonzi pale wazazi wetu walipokuja kupata ajari mbaya ya gari na kupoteza maisha papo hapo. Vifo vya wazazi wetu kwa mkupuo vilichimba donda kumbwa mno moyoni mwangu.
Usiombe ndugu msomaji kuwapoteza wazazi wako kwa wakati mmoja, maumivu yake ni zaidi ya msumari wa moto ukandamizwapo kwenye kidonda kinachoelekea kupona.
Tukio hilo huwa sipendi hata kulielezea kwani huwa linaibua machungu makubwa mno ndani ya moyo wangu. Yaani wee acha tu. Kama ukitaka nianze kububujikwa na machozi basi nikumbushie tukio hilo tu, aisee! Bora niachane na hizo habari kwani zitanifanya nishindwe hata kuendelea kukuhadithia yanayohusu mirathi ya kaka.
Wakati wazazi wetu wanatutoka mimi nilikuwa nipo darasa la tatu na kaka James alikuwa ndiyo kahitimu kidato cha nne.
Mara baada tu ya wazazi wetu kufariki kaka James alitaka tugawane mali tulizokuwa tumeachiwa. Kwa kuwa mimi nilikuwa mdogo sana, sikuwa na la kuamua wala kushauri zaidi ya kuwa kama bendera nikifata maamuzi ya kaka yangu.
Tuligawana mali zote huku nyumba akiniachia mimi. Hata hivyo tuliendelea kuishi hapo wote licha ya nyumba kuwa mikononi mwangu. Baadhi ya mali  nilizokuwa nimegawiwa kutoka kwenye mirathi hiyo tuliziuza ili zinisaidie katika masomo.
Kaka James yeye aliuza kila kitu, lakini hakutaka tena kuendelea na shule badala yake alianza kufanya biashara huku akiwa na mtaji wa kutosha kutokana na kuuza mirathi yake yote.
 Nilifanikiwa kusoma mpaka kidato cha sita huku kaka yangu yeye akiishia kidato cha nne tu. Lakini mpaka namaliza shule mwenzangu alikuwa kashakuwa tajiri huku biashara zake zikishamiri vizuri.
Kasi ya kupata utajiri kwa kaka James ilikuwa kubwa sana mpaka nikaanza kushangaa. Nilipojaribu kumuuliza kaka James kulikoni naye aliniiambia ni baraka kutoka kwa Mungu. Hilo ndilo lilikuwa jibu lake pindi nilipomuuliza kuhusu utajiri huo aliokuwa akiupata kwa kasi.
Mpaka namaliza kidato cha sita alikuwa ni tajiri wa kuogopeka mji mzima. Alikuwa na magari mawili ya kifahari na nyumba mbili za kifahari.

ITAENDELEA......

2 comments:

  1. This comment has been removed by the author.

    ReplyDelete
  2. Nilifanikiwa kusoma mpaka kidato cha sita huku kaka yangu yeye akiishia kidato cha nne tu.NowMing Lakini mpaka namaliza shule mwenzangu alikuwa kashakuwa tajiri huku biashara zake zikishamiri vizuri.

    ReplyDelete