Sunday, October 6, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 24



ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA....
Sajenti Bakari Mlongo alionekana kuwa na kigugumizi hatimaye akaganda mithili ya cd kongwe iliyochakaa. Wakili wangu bwana Jonas Mlyanyama alimwambia hakimu hana la zaidi la kumuuliza shahidi huyo.
SASA ENDELEA.......            
            Hatimaye shahidi wa pili kutoa ushahidi aliwadia. Shahidi aliyefuatia alikuwa ni Sajenti Majaliwa Mbogo, askari ambaye yupo katika kitengo cha kupima alama za vidole ambaye pia alikuwa ameambatana na kikosi kilichokuja kwangu siku ya tukio.
            Sajenti Mbogo baada ya kuapishwa alikumbushwa saa na siku ya tukio na mwendesha mashtaka bwana Charles Ngonyani.
            Sajenti Mbogo alieleza kuwa siku hiyo alikuwa kwenye kituo chake cha kazi kama ilivyo ada. Ndipo alipopata wito kutoka kwa mkuu wa kituo hicho na kuambiwa kuna mauaji yametokea kwenye nyumba yangu.   
“Tueleze ilikuwaje baada ya kuambiwa hivyo na mkuu wako wa kituo.”
“Agizo lililokuwa limetolewa pale ni kwenda kunako eneo la tukio, na ndicho kilichofuata.”
“Mlipofika eneo la tukio mlikuta nini?” Mwendesha mashitaka aliendelea kuuliza maswali ya kuweza kumuongoza shahidi huyo aendelee kutoa ushahidi.
            Maelezo ya Sajenti Mbogo hayakutofautiana sana na yale ya shahidi aliyekuwa ametangulia. Mwisho shahidi huyo alieleza jinsi matokeo ya vipimo vya alama za vidole yalivyonihusisha kuwa nilimuua Kishoka.
            Hatimaye mwendesha mashitaka alimaliza kutoa muongozo kwa shahidi huyo kisha akamwambia mheshimiwa Jaji kuwa amemaliza na akaenda kuketi.
            Wakili wangu aliinuka tena na kusogea kwenye kizimba ambacho shahidi huyo alikuwa amesimama. Alipofika akaanza kumuuliza maswali kama ilivyoada.
“Natumaini wewe upo kwenye kitengo cha kupiga picha na kupima alama za vidole kwa muda mrefu katika jeshi la polisi?”
“ Ndiyo.”
“Kama mimi nikishika kitu kisha mkaja kupima alama zangu za vidole si zitaonekana?”
“Ndiyo.”
“Nikiiambia mahakama kwamba mteja wangu alishika mwili wa marehemu pamoja na kisu baada ya kukuta tukio limeshatokea chumbani kwake kwa kutokujua madhara yake ama kutokana na kuchanganyikiwa unaweza ukakubaliana na mimi?”
“Hapana sitakubaliana na wewe.”
“Kwa nini?”
“Kwa sababu hatukuona alama za vidole vya mtu mwingine zaidi.”
“Mimi nitaiambia mahakama tukufu kwamba mteja wangu alishika sehemu hiyo hiyo aliyokuwa ameshika muuaji na ndiyo maana hazikuonekana alama za mtu mwingine.?”
“Haiwezekani, siyo rahisi kumshika mtu mpaka kumuua usimguse sehemu kubwa ya mwili. Ingekuwa mtuhumiwa aliyepo kizimbani hajafanya hilo tukio basi alama za vidole za mtu wa kwanza zingetapakaa mwili mzima wa marehemu.”
“Je, mtu kama kavaa ‘groves’ mikononi alama zake huonekana akishika sehemu?”
“Hapana.”
“Basi muuaji alikuwa kavaa groves wakati anaua na ndo maana alama za vidole hazikuonekana!”
“Hapana, muuaji ni yule pale kizimbani maana ndiyo tulimkuta eneo la tukio.”
“Shahidi aliyekutangulia amesema kwamba mtu aliyetoa taarifa za awali juu ya kifo cha kishoka hakujitokeza hata kidogo zaidi ya kupiga simu tu kituoni, unaweza kuniambia kwa nini hakutaka kujitokeza?”
“Kwa kweli siwezi kujua.”
“Nikikwambia kuwa hajajitokeza kwa kuwa alikuwa ni mharifu na huenda aliogopa kuja kuumbuka utakubaliana na mimi?”
“Hapo siwezi kusema chochote kwa sababu sijui sababu zilizomfanya asijitokeze kituoni.”
“Basi huyo akipatikana na kufanyia mahojiano kikamilifu huenda akawa na maelezo ya kutosha kuwasaidia katika upelelezi wa kesi hii na huenda mtambaini muuaji halali wa Kishoka na siyo mteja wangu.” Aliunguruma bwana Mlyanyama.
            Mpaka hapo Sajenti Majaliwa Mbogo hakuwa na la kuongea. Wakili wangu alimtazama jaji na kumwambia kamaliza maswali ya kumuuliza shahidi huyo. Baada ya kusema hivyo akaenda kuketi.
            Jaji aliiahirisha kesi na kutaja tarehe nyingine ambayo ingeendelea kusikilizwa. Nilitolewa kizimbani na kupelekwa kwenye karandinga la magereza tayari kabisa kwa kurudishwa mahabusu.
JE, KESI HII ITAISHAJE? USIKOSE TOLEO LIJALO!

No comments:

Post a Comment