Wednesday, October 23, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 34



ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA....
Gari lililokuwa limenichukua liliondoka kwa kasi ya ajabu kuelekea gerezani
    
                          **************************
SASA ENDELEA.......
Maisha ya jela ndiyo niliyoanza kuishi kwa wakati huo. Niligundua tofauti kubwa sana kati ya jela na mahabusu. Ukiwa mahabusu husumbuliwi kufanya kazi ama adhabu yoyote kwani unakuwa bado ni mtuhumiwa tu.
Lakini ukiwa jela unatakiwa kufanya kazi za hapa na pale zikiwa ni adhabu kwani tayari utakuwa umeshahukumiwa. Na ndiyo maana watu wengine husema jela kuna mateso.
Yote hayo ni tisa, kumi mkienda kulala, heheeeh! Kama utalemaa mithili ya kalio la kushoto basi unaweza ukawa mke wa wanaume wenzio. Huko ndiyo kuna watu waliopinda, watu wasiokuwa na dira na maisha.
Jela ni ubabe ubabe tu, unyama na mikwara ndiyo hutawala hasa kwa mtu mgeni gerezani humo. Hata hivyo kwa upande wangu hayo yote hayakutokea licha ya kuwa na muonekano wa upole.
Kilichonisaidia kutoionja adha ya ugeni wa jela ni kitu kimoja. Kuna jamaa mmoja nilimkuta humo gerezani ambaye tulikuwa tukifahamiana na kuheshimiana sana. Huyo mtu ndiyo alionekana kuwa msaada mkubwa sana kwangu kwani alikuwa kakaa humo kwa muda wa miaka miwili hivyo mikikimikiki ya huko alikuwa kashaizoiea.
Mbali na kuizoea mikiki mikiki ya humo; jamaa huyo alikuwa kashateuliwa kuwa mnyapara wa gereza. Mnyapara wa gerezani ni yule mfungwa anayewaongoza wafungwa wezake gerezani humo.
Jamaa huyo hakuwa mwingine bali ni Mack. Uhusiano wetu haukuanza siku hiyo ama siku za karibuni, ulianza miaka mingi iliyokuwa imepita. Tulikuwa tunafahamiana toka kitambo na tulikuwa tumeshafanya mambo mengi.
Baada ya kifo cha marehemu kaka James; mali zake zote nilizirithi mimi kwani ndiyo nilikuwa ndugu yake wa pekee. Ikumbukwe kuwa mimi na marehemu James tulizaliwa tumbo moja ila baba zetu ni tofauti.
Yeye ndiye alikuwa kifungua mimba katika tumbo la mama yetu. Mama yetu alipata ujauzito kwa bahati mbaya wakati anasoma elimu ya sekondari.
Baada ya kupewa ujauzito alilazimika kukatisha masomo ili aulee huo ujauzito hivyo akashindwa kuendelea na elimu na kujikuta akiishia kidato cha tatu.
Jamaa aliyekuwa amempa ujauzito alikimbia na kupotelea pasipojulikana kwa kuogopa kushtakiwa na wazazi wa mama yetu kwa kumrubuni na kumkatisha masomo mtoto wao.
Si wazazi peke yao waliokuwa wakila sahani moja na wanaume waliobainika kuwapa mimba watoto wao, hata serikali ilikuwa ipo mstari wa mbele kuhakikisha wanafikishwa mbele ya sheria.  
Tangu siku hiyo jamaa huyo alipotea kabisa na hakuonekana tena kama walivyopotea wadudu aina ya nzige. Nadhani waliozaliwa siku za nyuma kidogo wanakumbuka miaka ile ya uvamizi wa nzige katika mashamba ya wakulima.
Nzige ni wadudu hatari sana ambao hutembea katika kundi kubwa na wakivamia shambani mwako basi wanakula mimea yote iliyomo shambani humo. Usiombe shamba lako livamiwe na wadudu kama hao kwani wanakula hadi mashina ya mimea ya shamba wanalolivamia.
Sasa mwanaume aliyekuwa amempa ujauzito mama yetu na kumsababisha kukatisha masomo alipotea mithili ya wadudu hao.
Hakuonekana kabisa wala hazikusikika fununu zake hata kidogo. Kutokana na hiyo hali; mpaka wa leo haijulikani kama jamaa huyo bado yungali hai ama kashakumbwa na mauti.
Mama aliiingia katika wakati mgumu sana baada ya kubebeshwa huo ujauzito. Kilichokuwa kinamfanya apate tumbo joto ni jinsi baba yake alivyokuwa mkali na katili kupindukia, yaani marehemu babu.
Babu yangu huyo alikuwa ni mkali kama simba. Sijui kutokana na ujeshi wake aliokuwa nao, maana alikuwa mbogo kupita maelezo. Alikuwa hataki kabisa ‘Ujinga jazz bend’ katika familia yake.
Sasa ujauzito huo ulimfanya mama yangu azidi kuchanganyikiwa, kibaya zaidi hata aliyekuwa amempa huo ujauzito alikuwa kashakimbia na kutokusikika hata zile fununu zake.
Alichoamua ni kutoroka na kuenda asikokujua kwani aliona hata akienda kwa ndugu wengine baba yake angempata, na hapo ndiyo angelionja joto la jiwe.
Hakutaka kujiua wala kuitoa hiyo mimba kwani alikuwa akiijua vyema dhambi iliyopo kwa binadamu anayejiua ama anayeua. Hayo yote alikuwa ameyaweka akilini tangu utotoni alipokuwa akipewa mafundisho ya dini.
Mama yangu alilelewa katika maadili ya kidini sana japokuwa alikuja kuanguka dhambini na kurubuniwa na kamjamaa kalikokuja kumpa ujauzito.
Huku ujauzito aliokuwa nao ukiwa na miezi mitatu, mama aliamua kutorokea katika mji jirani ili kujiepusha na hasira za baba yake. Kwa mtazamo wake alihisi suluhu ya hiyo kashfa ni kulala mbele.
Alfajiri na mapema alitoka nyumbani kama anaenda shule akiwa na sare zake za shule huku nguo zingine akiwa ameziweka kwenye mfuko wake wa kubebea vitabu vya shule.
Kwa vile ilikuwa bado asubuhi sana, hakuna mtu yeyote  aliyemuona kwa pale nyumbani wakati anatoka. Alitembea mpaka kwenye stendi ya mabasi, akakata tiketi ya basi lililokuwa linaondoka muda si mrefu.
Wakati huo alikuwa tayari kashazivua sare za shule na kuvaa nguo zake za nyumbani alizokuwa ameziweka kwenye mfuko wa kubebea vitabu vyake vya shule.
Baada ya robo saa alikuwa tayari kajikausha kunako viti vya basi hilo huku likichanja mbuga kwa mwendo wa kasi.
Mambo yaligeuka kuwa si mambo mara baada ya basi hilo kuupa mgongo mji huo. Liligongana uso kwa uso na lori la mafuta na kusababisha ajari mbaya sana.
Basi hilo lilipiga mweleka na kubingirika mpaka mara tatu, likawa nyang’anyang’a kutokana na ajari hiyo.
Ilikuwa ni ajari mbaya sana na ya kutisha ambapo watu kumi na sita walipoteza maisha papo hapo, watu ishirini walikuwa ni mahututi na watu kumi na tano wakijeruhiwa ila siyo sana. Kati ya wale mahututi na mama yangu naye alikuwa ni mmoja wao.
Haukupita muda sana magari ya kubeba wangonjwa (ambulance) yakawa pale kubeba wahanga wa ajari hiyo pamoja na maiti na kuwapeleka katika hospitali ya jeshi iliyokuwa karibu kabisa na sehemu ilipokuwa imetokea ajari hiyo.
Mpaka anafikishwa hospitali mama yangu alikuwa hajielewi hata kidogo. Alikuwa kaumia vibaya sana

                        ************************
ITAENDELEA.....!

No comments:

Post a Comment