Monday, September 23, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 20



ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA......
Waliniamru nipande nami nikajitoma bila ya ubishi. Safari ya kuelekea mahakamani ilianza. Gari lilitoka mbio utadhani lipo katika mashindano, tulitumia takribani dakika kumi kufika mahakamani.
SASA ENDELEA.......
            Tulipofika mahakamani tuliwakuta watu kibao, baadhi yao niliwatambua, walikuwa ni wakazi wa mtaani kwetu. Nilianza kuhisi kuwa taarifa za kesi yangu zilikuwa  zimetapakaa sana huko mtaani.
            Kamera za mapaparazi nazo zilizidi kunisonga wakati naingia mahakamani. Nilijaribu kujifunika usoni ili nisipigwe picha lakini haikusaidia chochote. Nilipelekwa mpaka sehemu ya kukaa watuhumiwa wakati wanasubiri kupandishwa kizimbani.
            Mara ilisikika sauti... ‘koooort!’, sauti hiyo iliashiria kufunguliwa kwa mahakama. Watu wote walisimama ili kutoa heshima katika mahakama kama ilivovyo ada, muda mfupi waliketi na kesi zikaanza kusikilizwa.
            Kesi yangu ndiyo ilikuwa ya kwanza kutajwa. Nilipandishwa kwenye kizimba kisha nikaulizwa dini yangu. Nilipotaja dini yangu nikapewa kitabu kitakatifu cha dini husika na kuanza kuapishwa.
            Baada ya kuapishwa nilisomewa shitaka langu na kuambiwa sitakiwi kujibu chochote kwani mahakama hiyo ilikuwa haina uwezo wa kuendesha kesi ya mauaji. Baada ya hapo nilitolewa kizimbani na kurudishwa rumande nikasubiri jalada la kesi yangu lipelekwe mahakama kuu. Lakini rumande niliyopelekwa kwa mara hii haikuwa ile ya kule kituoni bali ni rumande ya magereza.
            Nilikaa mahabusu katika rumande hiyo kwa siku kadhaa nikisubiri tarehe ya kutajwa kwa kesi yangu kwa mara ya pili ambayo ilitakiwa kuhamishiwa mahakama kuu, mahakama ambayo huwa na uwezo wa kuendesha kesi za mauaji.
            Kawaida ya sheria za nchi yetu ni kwamba, mshtakiwa yeyote wa kesi ya mauaji hutafutiwa wakili na serikali kama hana uwezo wa kumlipa wakili. Wakili huyo humsaidia kusimamia kesi yake mpaka mwisho.
            Hicho ndicho kilichotokea kwenye kesi yangu hiyo. Nilitafutiwa wakili ambaye alikuwa ni wakili kutoka kwenye taasisi moja inayosimamia haki za binadamu.
            Nikiwa nasota kwenye rumande ya magereza nilipokuwa nimepelekwa baada ya kutoka mahakamani, wakili alinifuata na kuanza kujadiliana nami jinsi ya kunisaidia katika kunitetea kwenye kesi iliyokuwa ikinikabili.
            “Hebu nieleze ukweli wako wote ili nijue ni jinsi gani nitakusaidia.” Alisikika wakili Jonas Mlyanyama kwa sauti iliyokuwa imejaa upole na yenye kubembeleza.
“Kusema kweli sikuhusika kabisa na kifo cha Kishoka.”
“Ilikuwaje, hebu niambia A mpaka Z bila kuficha kitu chochote.”
            Nilianza kumweleza tukio zima lilivyokuwa. Nikamweleza jinsi msichana wa kule ufukweni nilivyokutana naye na kuweka miadi ya kunitembelea kesho yake nyumbani kwangu.
            Sikuishia hapo, niliendelea kusimulia jinsi mauzauza yalivyoanza kujitokeza kwa mwanadada huyo pale alipokuja nyumbani na kukatalia getini baada ya kwenda kuambiwa na Kishoka apite ndani. Hata Kishoka alipokuja kuniambia kuwa mgeni huyo kakataa kuingia ndani bali ananitaka niende kulekule getini, nilienda lakini sikumkuta.
            Niliendelea kumhadithia kizaazaa hicho wakili Jonas Mlyanyama huku akiwa kanisikiliza kwa makini kabisa. Hatimaye nilimaliza maelezo yangu kwa kueleza jinsi nilivyoikuta maiti ya Kishoka ikiwa imelazwa juu ya kitanda changu.
            “Nimeambiwa kwamba alama za vidole vyako zilionekana kwenye mwili wa marehemu na kwenye kisu kilichotumika kumuua marehemu, ulikigusa kisu au ile maiti?”
“Hapana wakili sikugusa chochote hapo, na ndiyo maana nakuambia kwamba kesi hii ipo kimazingara. Hata mimi nashangaa kuonekana alama za vidole vyangu.”
            Wakili Jonas Mlyanyama alivuta pumzi kisha akazishusha. Wakati natoa maelezo wakili huyo alikuwa ‘busy’ kuandika maelezo yangu kwenye kitabu alichokuwa amekuja nacho.
            Pamoja na kuwa ‘busy’ wakili huyo alionekana kuwa makini sana kunisikiliza kila nilichokuwa nakinena. Pia hakuacha kuhoji maswali pale ilipolazimu. Alikuwa na maswali mengi utadhani mgambo wa kata.
            Alinipa moyo na kuniambia kuwa kwa vile nilikuwa sijafanya kosa hilo kama nilivyokuwa nimeshtakiwa, Mungu angetusaidia na mwisho wa siku tungeibuka kidedea.
JE, WAKILI JONAS MLYANYAMA ATAFANIKIWA KUMTETEA BRIGHTON KATIKA KESI YA MAUAJI YA KISHOKA? USIKOSE TOLEO LIJALO!

No comments:

Post a Comment