Monday, September 16, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 14



ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA......
 ‘Wamewasha hadi taa utadhani ni chumbani kwao, hizi sasa ni dharau. Kwa nini asimpeleke chumbani kwake?’ Nilizidi kujisemea kimoyomoyo.
SASA ENDELEA.......
            ‘Lakini Kishoka huwa hana kawaida ya kuingia chumbani kwangu kama sipo, na hata kama angekuwa na kawaida hiyo asingefanya hivyo kwani alikuwa kanipigia simu muda si mrefu kunijuza kuwa kuna mgeni wangu ananisubiri nami nikamwambia nipo njiani.’ Nilizidi kuwaza huku masikio yakiwa makini kusikilizia chumbani kama kuna mihemo ama miguno ya watu wakifanya matusi.
Lakini suala la Kishoka kusahau kuufunga mlango wangu ama kuacha kwa makusudi lilikuwa haliniingii akilini hata kidogo kwani alikuwa ni mtu mwaminifu sana. Sasa aliingiwa na ibilisi gani mpaka akaamua kutofunga mlango wangu. Na kama alikuwa kafunga aliingiaje wakati funguo nilikuwa nazo na nilikuwa sina kawaida ya kuziacha? Funguo nilikuwa natembea nazo utadhani pete ya ndoa kwa mwanandoa mwaminifu!
Nilizidi kujiuliza maswali teletele huku nikiusogelea mlango. Nilipousukuma mlango nilizidi kuchanyikiwa baada ya kukiona kisu kilichokuwa kimetapakaa damu kikiambaa ambaa pale mlangoni kunako tambala la kufutia miguu.
Nililazimika kuingia kwa tahadhari kubwa wakati chumba kilikuwa ni changu, chumba ambacho nilikuwa nimeshakizoea kiasi kwamba hata liwemo giza totoro lakini swichi ya taa sitashindwa kuiwasha. Siku hiyo nilijikuta nikinyata wakati taa ilikuwa inawaka!
            Kwa mwendo wa kunyata niliuvusha mguu wangu wa kwanza pale mlangoni huku ukifuatiwa na mguu wa pili. Nilijaribu kuangaza mbele usawa wa mlango lakini sikuona chochote kigeni zaidi ya kabati langu la nguo na meza ya  kujipodolea yenye kioo kikubwa cha kuweza ujiona nusu mwili; yaani kuanzia kiunoni kwenda juu.
            Wakati huo nilikuwa sijaangalia upande wa kulia wa chumba changu, upande ambao kitanda changu cha sita kwa sita kilipokuwa, si unajua tena mambo ya mila na desturi kitanda sharti kiwe pembeni!
Niligeuka mzima mzima huku nikitupia jicho langu pale kitandani. Jicho lilipotua kitandani nilijikuta nikibaki mdomo wazi huku nikikodoa macho bila ya kupepesa.
            Lahaula! Mambo yaliyokuwa yametendeka juu ya kitanda changu ni vioja, nilishindwa kuelewa ni nani aliyefanya unyama huo usiokuwa na breki hata kidogo. Nguvu zilianza kuniishia, nikabaki nimeduwaa huku nisijue la kufanya. Sikutegemea kabisa kukuta tukio la kutisha na la umafia namna ile likiwa limetendeka kwangu, tena juu ya kitanda changu.
            Tukio jenyewe lilikuwa ni la mauaji ya kutisha, kichwa cha Kishoka kilikuwa kimetenganishwa na kiwiliwili chake. Kisu kilichokuwa mlangoni kikiwa kimetapakaa damu nadhani ndicho kilichotumika kumchinja mpangaji wangu, yaani Kishoka.
‘Chinjachinja ni nani sasa kama siyo yule mgeni wangu? Na kama ndiyo yeye, kajificha wapi sasa wakati sijamuona akitoka?’ Nilizidi kuchoka.
‘Kumbe msichana huyo ni hatari! Sioni mtu mwingine wa kufanya kitendo kama hiki zaidi yake, atakuwa ni huyohuyo!’ Nilizidi kunena kimoyomoyo huku nikiisogelea maiti ya Kishoka, maiti ambayo ilikuwa haitamaniki kutokana na  kutenganishwa kikatili, kichwa na kiwiliwili havikuwa pamoja tena.
            Wakati nikitafakari hatua ya kuchukua kwa wakati huo, nilishangaa baada ya kuona watu wawili wanaingia mpaka humo chumbani kwangu utadhani ni kwao vile, wote walikuwa na jinsia ya kiume. Sijakaa sawa wakanipiga ‘henzapu’ na kuniambia nipo chini ya ulinzi.
            Pumzi zilianza kuniishia, nikajikuta nikipumua kwa shida huku kifua changu kikianza kubana. Sijakaa sawa nikaanza kuhisi kama kizunguzungu na kuhisi kama nataka kuanguka. Mpaka hapo nilipoteza ‘network’ na kujikuta sijitambui hata kidogo.

                                    **********************
SALAAAAALEH! HAPO PATAMU KWELIKWELI NDUGU MSOMAJI, HEBU FUATILIA TOLEO LIJALO UONE NI NINI KITATOKEA.

No comments:

Post a Comment