Wednesday, October 9, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 26



ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA....
Pumzi zilizidi kubana, ghafla nilijiona nikianguka mzima mzima huku macho yangu yakipoteza upeo wa kuona. Kabla sijafika chini niliacha kujitambua na kupoteza fahamu ghafla.
SASA ENDELEA.......


            “Brighton, unajisikiaje?” Ilikuwa ni sauti ya wakili wangu bwana Jonas Mlyanyama aliyekuwa kaketi pembeni mwa kitanda nilichokuwa nimelala.
“Mh! Wakili, hapa nipo wapi?” Nilijikuta nikiuliza swali na siyo kutoa jibu baada ya kumfahamu mtu niliyekuwa naongea naye.
“Hapa upo kwenye hospitali ya magereza, ulianguka ghafla leo asubuhi wakati ukiwa kizimbani.” Alinijibu bwana Mlyanyama.
            Baada ya kuniambia hivyo kumbukumbu zilinijia kwa kinagaubaga. Hapo ndiyo nilikumbuka tukio zima lilivyokuwa, hata hivyo nikapata shauku kubwa ya kumuuliza wakili wangu jinsi mambo yalivyokuwa kule mahakamani.
            Wakati mimi ninashauku hiyo, yeye naye alikuwa na shauku ya kujua ni kitu gani kilinifanya nipoteze fahamu nilipokuwa pale kizimbani. Kila mmoja akawa na hamu ya kusikia maelezo kutoka kwa mwenzake.
            Nilishusha pumzi ndeefu kisha nikamwambia bwana Mlyanyama,
“hivi nilianguka mpaka chini kabisa?”
“Ndiyo! Kwani ilikuwaje?”
“Kaka, ni mambo ya ajabu niliyoyaona mle mahakamani!”
“Mambo gani hayo?” Aliniuliza wakili huyo kwa upole kabisa huku akikaa mkao wa kula kisikia kilichonifanya nianguke na kuzua gumzo mahakamani hapo.
            Ndipo nilipoamua kumpasulia kile nichokuwa nimekiona mahakamani.
“Yule msichana aliyeinuka kutoa ushahidi ndiyo muuaji kaka.” Nilimwambia wakili wangu kwa sauti ya kunong’ona.
“Muuaji ki vipi?” Naye alihoji kwani somo lilikuwa bado halijamwingia akilini.
“Yule ndiyo msichana mwenye mauzauza niliyekusimulia.”
“Yule uliyeonana naye ufukweni kisha kesho yake akawa anagonga geti lakini mkienda kumfungulia mnakosa?” Alizidi kuhoji wakili Jonas Mlyanyama.
“Haswaah! Wala hjakosea kaka. Sasa kitendo cha kumuona msichana huyo moyo wangu ulishtuka ghafla mpaka nikaanza kujihisi napata shida kupumua. Baada ya hapo sikujitambua tena.”
            Mpaka hapo wakili wangu akawa ameshakifahamu kilichonifanya nizirai huku nikiwa kwenye kizimba. Nilipotupia jicho kwa wakili Mlyanyama nilimuona kajishika tama huku akionekana kuwaza kwa kina, baada ya hapo akashusha pumzi ndeefu iliyoashiria mtu kuchoka ama kukata tamaa.
            “Kwa kweli hii kesi inautata sana. Tangu niwe wakili sijawahi kukutana na kesi yenye kizaazaa kiasi hiki. Pamoja na kukaa katika kazi hii kwa miaka zaidi ya kumi na mitano hii ndiyo mala ya kwanza kukumbana na kesi ngumu kama hii. Ama kweli hii ni kali, tena ni kali ya karne.” Alisikika bwana Jonas Mlyanyama.
“Ehe, baada ya kuanguka nini kiliendelea?” Nikazidi kudodosa.
“Kesi yako imeahirishwa, itapangwa tena pale afya yako itakapoimarika.”
“Na yule mwanamke alielekea wapi baada ya hapo?”
“Hata sikumfuatilia.” Alinijibu na kuonekana tena kuzama kwenye lindi la mawazo.
“ Sasa subiri nikaandae hoja za kisheria za kuja kumkabili siku ya kusikilizwa tena kesi yako, labda asije.”
“Yule ni mchawi kaka sidhani kama utamuweza.”
“Pamoja na uchawi wake hapa kagonga mwamba.” Aliongea Mlyanyama huku akijipigapiga kifuani kuonyesha kujigamba fulani hivi.
            “Yangu macho na masikio siku hiyo, lakini mimi nimeshamnyanyulia mikono huyo ibilisi. Nashangaa sijui kwa nini kaniandama sana na kunisababishia ndege mbaya katia maisha yangu, kanipotezea dira ya maisha kabisa, isitoshe hata hatima yangu haijulikani.” Nilijikuta nikiongea kwa uchungu huku nikionyesha kukata tamaa kwa hali zote.
ITAENDELEA.....

No comments:

Post a Comment