Saturday, November 23, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 46

            
Brighton anaota ndoto ya ajabu akiwaona watu waliokufa siku nyingi kwa kujiua wakiwemo mzee Mboma, Patrick, James na Anna. Baada ya ndoto hiyo anazongwa na mwanadada Sharifa anayemsababishia kesi ya mauaji ya mpangaji wake, yaani Kishoka. Kesi inaunguruma mahakamani kisha anajikuta akihukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe kwa kosa la mauaji ya Kishoka, kosa ambalo alikuwa hajalitenda. Akiwa gerezani akisubiri tarehe za kunyongwa anakutana na Mack, jamaa aliyekuwa amenunua nyumba iliyokuwa ya marehemu James, naye Mack anaanza kumhadithia kisa kilichompelekea afungwe jela.
Kwa kusimuliwa na Mack, Brighton anayasikia mengi kuhusu mali alizokuwa amerithi kutoka kwa marehemu kaka yake kwa kila aliyekuwa amemuuzia aliishia kupatwa na matatizo akiwemo Mack mwenyewe. Hatimaye siku ya kunyongwa inafika kweli, hata hivyo anajikuta anakolewa kimiujiza na msichana aliyemsingizia kuua, yaani Sharifa, anatolewa gerezani na kuwa huru kabisa.  Sasa endelea...................

             Mlango wa chumba kile ulikuwa umefungwa. Nilishangaa kuona tunapenye kwenye ukuta kama vile tunapita sehemu yenye uwazi.
            Tuliendelea kutembea kwa hatua za madaha huku akiwa amenishika mkono. Tulitokezea mpaka nje ya jengo tulilokuwemo. Tukaendelea kutembea kuelekea kwenye lango kuu la kuingilia kwenye magereza hiyo.
            Niliweza kuwashuhudia askari magereza wakizunguka zunguka na wengine wakiwasimamia wafungwa waliokuwa wanafanya kazi kwenye ngome ya gereza hilo.
            Katika fikra zangu nilijua kuwa kila mtu anatuona, nikaona nimuulize Sharifa,
“mbona tunatoka kwa kujiamini hivi? Hao askari wakituona si tutapata tabu?”
“Hapa hatuoni mtu yoyote hata tupite palepale aliposimama, labda ngoja nikupe mfano kwa ofisa yule tunayekutana naye.” Alinijibu huku akinionyesha ofisa mmoja tuliyekuwa tunakutana naye.
            Alipomsogelea alimwasha kibao cha haja. Ofisa huyo aliishia kujipapasa tu na hakujua alikuwa kapigwa na nani. Nilianza kucheka kwa kicheko cha chinichini baada ya kukishuhudia hicho kisanga.
            “Hata ukicheka kwa sauti hamna atakayekusikia. Usiwe na wasiwasi upo kwenye mikono salama kabisa.” Aliniambia baada ya kuniona nacheka kwa chinichini.
            Tulitembea mpaka tukafika kwenye geti kubwa. Tulipita bila ya kubughudhiwa na mtu yeyote. Tulipofika nje akaniambia niende mpaka nyumbani kwangu halafu mambo mengine tutayaongea hapo baadaye.
            Nilipojaribu kumuuliza kuwa yeye anaelekea wapi kwa wakati huo aliniambia sipaswi kujua. Nilimuaga na kumshukuru kwa kuniokoa na adhabu iliyokuwa inanikabili kisha nikaanza mdogomdogo kuchapa lapa kuelekea nyumbani kwangu.
            Wakati namuaga alikuwa kasimama barabarani. Nilitembea kidogo kisha nikageuka nyuma kumwangalia. Lahaula! Sikumuona tena.
            Akili yangu ilibaki kuwa na kazi ya ziada japo kuwa nilikuwa nimetoka jela na nimenusurika na adhabu ya kunyongwa. Kikubwa kilichokuwa kinaniumiza akili ni hayo masharti yake. Mpaka muda huo nilikuwa sijajua ni masharti gani atanipa. Kilikuwa ni kitendawili kigumu sana akilini mwangu.
            Nilifuata barabara nikitembea kwa miguu kwani mifuko yangu ilikuwa imetoboka, yaani sikuwa hata na shilingi. Njiani nilikoma na moshi wa magari. Sikuwa na cha kufanya zaidi ya kuyakenulia meno magari yote yaliyokuwa yakinipita kwa vile sikuwa na nauli.
            Safari ya kutoka lilipokuwa gereza nililokuwa nimefungwa mpaka nyumbani kwangu ni mwendo wa masaa mawili kwa miguu. Kibaya zaidi mambo ya kuombana lifti hayakuwepo kabisa katika mji huo. Niliendelea na ‘ba funika ba funua’ mpaka nikafika.
            Nilifika mpaka kwenye geti la fensi ya nyumba yangu, nikajaribu kulisukuma lakini likawa gumu. Kwa kuwa kulikuwa na swichi ya kengele wala sikuhangaika. Nilipeleka mkono wangu panapo swichi, nikabofya kistaarabu kisha nikakaa pembeni kusubiri majibu.
            Punde si punde geti lilifunguliwa. Akatokea jamaa mmoja akiwa kifua wazi.
“Karibu!” Alisikika jamaa huyo akiniambia.
“Asante! Habari yako kaka?”
“Nzuri! Sijui nikusaidie nini?” Alihoji swali hilo ambalo lilinifanya nimshangae.
            ‘Hivi huyu hajui ya kuwa mimi ndiyo mwenye nyumba hii? Au anavyoniona nimekondeana namna hii basi anajua kuwa mimi ni kapuku?’ Niliwaza huku nikiwa ninamwangali jamaa huyo pasipo kummaliza. .
            “Ndugu, sema shida yako nina mambo kibao ya kufanya huko ndani, ila kama unakuja kupiga kibomu kwa mheshimiwa kasafiri, tena hayupo kabisa ndani ya nchi hii.” Alizidi kueleza jamaa huyo.
            Maelezo hayo yalinishtua na kunifanya nianze kupatwa na wasi wasi fulani. Niliyekuwa nimemkabidhi nyumba pamoja na miradi yangu yote alikuwa ni kijana tu kama mimi. Sasa nilizidi kuumiza kichwa uheshimiwa umetoka wapi kwa kijana kama huyo!

AISEEEH, KWA BRIGHTON SASA PANAITWA KWA MHESHIMIWA, HUYO MHESHIMIWA NI NANI? PIA SHARIFA KAPOTELEA WAPI? JE, NA MAISHA YA BRIGHTON YATAKUWAJE BAADA YA KUTOKA JELA? USIKOSE TOLEO LIJALO!

No comments:

Post a Comment