Tuesday, November 19, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 43

KWA WASOMAJI WAPYA.....
            Brighton anaota ndoto ya ajabu akiwaona watu waliokufa siku nyingi kwa kujiua wakiwemo mzee Mboma, Patrick, James na Anna. Baada ya ndoto hiyo anazongwa na mwanadada Sharifa anayemsababishia kesi ya mauaji ya mpangaji wake, yaani Kishoka. Kesi inaunguruma mahakamani kisha anajikuta akihukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe kwa kosa la mauaji ya Kishoka, kosa ambalo alikuwa hajalitenda. Akiwa gerezani akisubiri tarehe za kunyongwa anakutana na Mack, jamaa aliyekuwa amenunua nyumba iliyokuwa ya marehemu James, naye Mack anaanza kumhadithia kisa kilichompelekea afungwe jela.
Kwa kusimuliwa na Mack, Brighton anayasikia mengi kuhusu mali alizokuwa amerithi kutoka kwa marehemu kaka yake kwa kila aliyekuwa amemuuzia aliishia kupatwa na matatizo akiwemo Mack mwenyewe.  sasa endelea...................

Alipopandishwa kizimbani kwa mara ya kwanza alisomewa mashtaka kisha akatakiwa kutojibu chochote kwani mahakama hiyo ilikuwa haina uwezo wa kusikiliza kesi kama hiyo, yaani kesi ya mauaji.
Aliendelea kukaa rumande wakati taratibu za upelelezi wa kesi yake zikiwa bado hazijakamilika. Jalada lake lilipokamilika kesi yake ilihamishiwa kwenye mahaka kuu.
Kesi iliendelea kurindima. Kitu kilichomuacha hoi Mack ni yule shahidi namba moja wa kesi hiyo ambaye alijitambulisha kuwa ni mume  wake na Sada, yaani mwanadada aliyekuwa ameuawa.
Mack alishangaa kumuona shahidi huyo ndiye jamaa aliyekuwa ameuliwa na kaka James kwa kupigwa risasi baada ya kumkuta na Neila ambaye alikuwa ni mpenzi wake (yaani kaka James). Kijasho chembamba kilianza kumtoka.
Jamaa alitoa ushahidi wake akidai kuwa siku ya tukio alikuwepo na alimshuhudia Mack wakati anafanya mauaji.
Kilichozidi kumchanganya Mack na ndiyo hicho hicho kilichokuwa kinazifanya kesi zetu ziwe mapacha ni ushahidi wa ule mkanda uliorekodiwa na kamera maalum za nyumba hiyo ukionyesha mwanzo mpaka mwisho wa tukio.
Mack hakuua. Tena maskini wa Mungu alikuwa haijui hata hiyo nyumba aliyokuwa akiishi mwanamke huyo. Ni sawa kweli alikuwa na wenyeji kidogo kwenye mtaa wa Matopeni, lakini alipokuwa akikaa Sada alikuwa hapajui na ndiyo maana alichemsha kumpata siku alipoenda kumtafuta.
Yale yale kama yaliyotokea kwangu, kuonekana alama za vidole vyangu kwenye mwili wa Kishoka na kwenye kisu wakati sikuwahi hata kuvigusa. Tena hiyo ni tisa, kumi kuonekana picha zangu kwenye kamera nikimchinja Kishoka wakati sikuhusika abadani!
Mwisho wa siku Mack alihukumiwa kunyongwa mpaka afe kwa kosa la kumuua Sada kwa kukusudia. Hivyo ndivyo stori ilivyoenda kwa mujibu wa maelezo yake.
Nilivuta pumzi ndeefu kisha nikaishusha baada ya kumaliza kusimuliwa simulizi hiyo na Mack mwenyewe.
“Mbona kama kuna zengwe fulani hivi kwenye mirathi ya kaka James? Maana mambo yanayotokea siyaelewielewi!” Nilitamka maneno hayo nikimwambia Mack.
“Na hayo matatizo siyo kwetu sisi peke yetu tu, takribani watu wote uliowauzia mali za huyo marehemu kaka yako wamepatwa na matatizo!” Alisikika Mack na kuzidi kunipa mpasuko wa moyo.
            Sasa moyo wangu haukuwa na amani tena. Niliishiwa nguvu mithili ya mtu anapoletewa msiba wa mtu ampendaye kwa dhati. Hata hivyo hamu ya kutaka kujua kilichojiri kwa wateja wangu hao ilizidi kunifukuta.
            “Mungu wangu! Ni matatizo gani yaliyowapata?” Nilijikuta nikiuliza kwa mshangao mkubwa.
“Yule jamaa uliyemuuzia ile kampuni ya usafirishaji hayupo tena duniani.”
“Wewe! Kunesa alishafariki? Ilikuwaje?” Nilijikuta nikizidi kuchanganyikiwa huku nikiuliza maswali dabodabo.
            Mack alianza kunieleza yaliyojiri huko moja baada ya jingine. Alianza na habari za huyo Kunesa, jamaa niliyekuwa nimemuuzia kampuni ya usafirishaji niliyokuwa nimerithi kutoka kwa kaka yangu.
            Alinieleza jinsi kifo cha Kunesa kilivyokuwa. Japokuwa hata yeye hakuwepo huko wakati kifo hicho kinatokea ila alisimuliwa na baadhi ya ndugu na jamaa zake waliokuwa wakienda kumuona pale gerezani.
            Alieleza kuwa Kunesa alikutwa kafa kwenye ofisi yake. Alikuwa kachinjwa huku kichwa kikiwa mbali na kiwiliwili chake. Aliyefanya tukio hilo hajajulikana mpaka wa leo.
            Nilipouliza watu wengine waliokumbwa na matatizo nikaambiwa ni wale jamaa waliokuwa wameyanunua yale magari. Waliyakuta magari yanawaka moto yenyewe kwa nyakati tofauti na chanzo cha moto huo wala hakikujulikana. Habari hizo zilizidi kunipa wasiwasi mkubwa juu ya mali za kaka James. Nikazida kujiuliza kulikoni kuhusu hizo mali.
            Walionunua maduka walifilisika wote, maduka yaliisha na kubakia matupu kabisa. Nilianza kuwaza endapo watu hao wangeamua kunitafuta sijui wangenifanya nini!
            “Na wewe umefikaje kwenye gereza hili wakati hata huko mahakama kuu ipo pamoja na magereza ya kutosha kabisa.” Niliona nimuulize Mack swali hilo lililokuwa linanitatiza tangu nilipomuona tu.
“Afya yangu ilianza kuwa mgogoro mara baada ya kufungwa. Ndipo daktari wa hospitali ya gereza hilo akashauri kwamba nihamishiwe gereza jingine akidai kuwa hali ya hewa ya pale ilikuwa imenikataa. Ndipo nilipoletwa huku.”
            Kwa kweli zilikuwa ni habari nzito za kutisha na kusikitisha. Nilianza kujiona kuwa ni muuaji kwani mtu kama Kunesa nilihisi kuwa nina mchango mkubwa mno juu ya kifo chake, ukizingatia nilimbembeleza kuinunua hiyo kampuni baada ya kukosa mtu wa kuinunua.
            Hiyo ilikuwa ni siku ya kwanza kukutana na Mack, siku ambayo ndiyo kwanza nilikuwa nimetoka mahakamani kuhukumiwa.

                        ***************************

DUH! HIZO MALI ZA URITHI WA BRIGHTON KUTOKA KWA KAKA YAKE ZINA NINI? MBONA KILA ALIYEZINUNUA ANAPATA MATATIZO? USIACHE KUFUATILIA SIKU SI NYINGI UTALIPATA JIBU!

No comments:

Post a Comment