Thursday, November 21, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 44

KWA WASOMAJI WAPYA.....
            Brighton anaota ndoto ya ajabu akiwaona watu waliokufa siku nyingi kwa kujiua wakiwemo mzee Mboma, Patrick, James na Anna. Baada ya ndoto hiyo anazongwa na mwanadada Sharifa anayemsababishia kesi ya mauaji ya mpangaji wake, yaani Kishoka. Kesi inaunguruma mahakamani kisha anajikuta akihukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe kwa kosa la mauaji ya Kishoka, kosa ambalo alikuwa hajalitenda. Akiwa gerezani akisubiri tarehe za kunyongwa anakutana na Mack, jamaa aliyekuwa amenunua nyumba iliyokuwa ya marehemu James, naye Mack anaanza kumhadithia kisa kilichompelekea afungwe jela.
Kwa kusimuliwa na Mack, Brighton anayasikia mengi kuhusu mali alizokuwa amerithi kutoka kwa marehemu kaka yake kwa kila aliyekuwa amemuuzia aliishia kupatwa na matatizo akiwemo Mack mwenyewe.  sasa endelea...................

             Suala la kuandika barua kwa rais ndiyo lilikuwa limetawala katika kichwa changu. Hiyo ndiyo fursa pekeee iliyokuwa imebakia ya kujaribu kujitetea, si unajua tena mfa maji haishi kutapatapa.
            Rais anao uwezo wa kumsamehe mfungwa wa mauaji endapo ataandika barua kuelezea ambavyo haki haikutendeka katika hukumu yake kwa mujibu wa sheria za nchi yetu naye akajiridhisha na sababu hizo.
            Wazo hilo alinipa Mack, akaniambia unaweza ukamwandikia barua rais na kumweleza jinsi mazingira ya kesi yako yalivyokuwa. Kama akiridhika na maelezo yako anaweza akakuachia ukawa huru.
            Wazo hilo nililiafiki na kulipokea kwa mikono miwili. Nikaandika barua na kuikabidhi kwa mhusika gerezani hapo ambaye alifanya harakati za kuipeleka kwa mheshimiwa rais. Nilijipa matumaini kuwa huenda mheshimiwa ataridhika na malalamiko yangu na kuniachia huru.
            Siku zilizidi kukatika bila kupata majibu yoyote. Miaka kadhaa ilipita nikiwa gerezani kusubiri siku za adhabu yangu ya kunyongwa. Ilibidi nikubaliane na hali halisi ya kwamba kifo changu kitakuwa cha kupigwa kitanzi.
            Hayawi hayawi hatimaye yalikuwa. Siku moja nikiwa sina hili wala lile niliitwa na kuambiwa masaa yangu yalikuwa yanahesabika. Yaani namaanisha siku yangu ya kupigwa kitanzi ilikuwa ndiyo hiyo.
            Nilipelekwa kwenye chumba kimoja ambako niliambiwa nitakutana na mtumishi wa Mungu ili anihubiri na kuniombea pia. Kama ningetaka kutubu dhambi zangu huo ndiyo ulikuwa ni muda muafaka.
Nilijikuta mwili ukinyong’onyea ghafla kwa hofu ya kifo. Usiombe kuijua siku na saa unayokufa.
            Wakati naukanyaga mlango wa chumba hicho nilimuona mwanamke aliyekuwa kainama chini akisomasoma kitabu. Niliambiwa huyo ndiye mtumishi wa Mungu na nilipewa masaa kadhaa ya kuongea naye kabla sijapelekwa kwenye chumba cha kunyongea.
            Mwanamke huyo alionekana kuwa bado yungali msichana. Hata hivyo mpaka nakaa nilikuwa bado sijaiona sura yake kutokana na sababu kuu mbili; sababu ya kwanza ni kutokana na yeye kuwa ‘busy’ na kusoma kitabu na sababu ya pili ni kutokana na machozi kunifumba macho kwani nilikuwa nikilia kilio cha kimya kimya. Hicho huitwa kilio cha ng’ombe; kilio cha kutoa machozi bila ya kutoa sauti.

HAYA SASA, HAYAWI HAYAWI MWISHO YAMEKUWA, KWELI  BRIGHTON ATANYONGWA? USIKOSE TOLEO LIJALO! 

No comments:

Post a Comment