Sunday, November 17, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 42

KWA WASOMAJI WAPYA.....
            Brighton anaota ndoto ya ajabu akiwaona watu waliokufa siku nyingi kwa kujiua wakiwemo mzee Mboma, Patrick, James na Anna. Baada ya ndoto hiyo anazongwa na mwanadada Sharifa anayemsababishia kesi ya mauaji ya mpangaji wake, yaani Kishoka. Kesi inaunguruma mahakamani kisha anajikuta akihukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe kwa kosa la mauaji ya Kishoka, kosa ambalo alikuwa hajalitenda. Akiwa gerezani akisubiri tarehe za kunyongwa anakutana na Mack, jamaa aliyekuwa amenunua nyumba iliyokuwa ya marehemu James, naye Mack anaanza kumhadithia kisa kilichompelekea afungwe jela, sasa endelea...................

            Pale pale nikajishauri kuwa nimkatishe Mack kwa kumuuliza swali tena kwani kuuliza ilikuwa siyo dhambi na nilikuwa sijakatazwa. Ndipo nilipomuuliza kuwa msichana huyo alijitambulisha kwa jina gani.
            “Alisema kuwa anaitwa Sada, mwenyeji na mzaliwa wa Matopeni ila wazazi wake walikuwa wameshafariki kwa kipindi hicho.” Hilo ndilo lilikuwa jibu la Mack kwa swali nililokuwa nimemuuliza, jibu ambalo lilianza kunitoa katika hisia zangu juu ya msichana huyo.
            “Alikuwa yukoje yukoje kimuonekano?” Nilizidi kudodosa nikidhani ya kuwa huenda alikuwa kabadilisha tu majina.
“Alikuwa ni mwembamba halafu kaenda hewani kimtindo, mweupe na mwenye mwanya. Akiwa anaongea sauti yake ilikuwa nzito kiana.” Alidadavua Mack.
Jibu hilo pekee lilitosha kuitengua hoja iliyokuwa imejengeka akilini mwangu ya kwamba mwanamke huyo alikuwa ndiyo Sharifa. Nilimuacha Mack aendelee kunipa michapo labda kwa baadaye ningeweza kung’amua kitu kuhusu mwanadada huyo.
Aliendelea kunielezea. Akasema kuwa baada ya siku mbili kupita mwanamke huyo alijileta mwenyewe kwa Mack akija kumwambia anampa onyo la mwisho, kama hatahama vitendo vingefuata.
Mack alitaka sana kuumaliza mgogoro huo kwa njia ya amani akiamini kabisa kuwa yote yanawezekana kwa nguvu ya hoja. Alimsihi mwanadada huyo waende kwenye ofisi za serikali ya mtaa ili wakaliongelee shauri hilo.
Hata hivyo mwanamke huyo alimjibu kwa nyodo nyingi akisema kuwa hana muda mchafu wa kwenda kuonana na hao viongozi wa serikali za mtaa. Siyo muda peke yake, hata hadhi yake ilikuwa siyo ya kwenda kuvimbisha tumbo lake mbele ya watu kama hao aliowaita majuha.
Mack aliyapeleka majibu hayo kwa hao viongozi, nao wakamwambia ya kuwa asubiri hatua atakayochukua mwanamke huyo huku wakiahidi kuwa mstari wa mbele kumtetea.
Wiki moja baada ya hapo kioja kilitokea nyumbani kwa Mack. Wakati anatoka kwenye mihangaiko yake ya kila siku, alikutana na askari polisi waliokuwa wakimsaka kwa udi na uvumba. Walipompata walimweka chini ya ulinzi wakimwambia ametoka kuua mtaa wa Matopeni.
Alishangaa sana kusikia hivyo, akawaambia kuwa yeye hajaua. Wakamwambia kuwa ameua kwani nyumba aliyokuwa ameenda kufanya tukio hilo ilikuwa na kamera maalum za kunasa wezi na wahalifu mbalimbali.
Alipouliza kamuua nani akaambiwa kuwa kamuua mwanadada mmoja aliyekuwa akijulikana kwa jina la Sada, mwanamke aliyekuwa akiishi katika mtaa wa Matopeni.
Mack aliendelea kubisha. Askari hao wakaanza kupekua kwenye gari lake. Katika pekua pekua waliona bastola ndani ya gari la lake, kitu ambacho kilikuwa ni kigeni kabisa kwake.
Kiukweli alikuwa hana bastola na alikuwa hajawahi kumiliki siraha kama hiyo katika maisha yake, hata kule kuishika masikini wa Mungu alikuwa hajawahi. Cha ajabu sasa ilipatikana, tena ndani ya gari lake. Alizidi kuchanganyikiwa.
Askari waliendelea kueleza kuwa kwenye kamera hizo Mack alianza kuonekana tangu anafika kwenye nyumba ya Sada na zilikuwa zimerekodi tukio zima.
Kati ya askari waliokuwa wamemkamata mmoja alikuwa akimfahamu, hivyo baada ya kuiona picha yake kwenye kamera hizo akawa amemtambua.
Habari hiyo ilikuwa ni ngeni kabisa kwa Mack. Aliwaeleza askari hao kuwa yeye hakuua ingawaje kweli alikuwa katika mgogoro wa nyumba na huyo Sada. Alizidi kujitetea kuwa hata nyumbani kwake (yaani kwa Sada) alikuwa hapafahamu kwani siku moja alienda kumtafuta ili waende kwenye ofisi za serikali ya mtaa kuuongelea mgogoro wao lakini hakufanikiwa kumpata msichana huyo.
Pamoja na kujitetea kote huko, Mack aliambulia kuwekwa chini ya ulinzi na kupelekwa kwenye kituo cha polisi cha kati. Alikaa hapo kwa siku moja na nusu kisha jalada la kesi yake likapelekwa kwenye mahakama ya hakimu mkazi.

DAH! MAUZAUZA YANAHAMIA KWA MACK. HUYO SADA NI NANI NA ANAUHUSIANO WOWOTE NA SHARIFA ALIYEKUWA AKIMSUMBUA BRIGHTON? USICHOKE KUFUATLIA MWISHO WA SIKU MAJIBU YOTE UTAYAPATA. 

No comments:

Post a Comment