Friday, November 22, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 45

KWA WASOMAJI WAPYA.....
            Brighton anaota ndoto ya ajabu akiwaona watu waliokufa siku nyingi kwa kujiua wakiwemo mzee Mboma, Patrick, James na Anna. Baada ya ndoto hiyo anazongwa na mwanadada Sharifa anayemsababishia kesi ya mauaji ya mpangaji wake, yaani Kishoka. Kesi inaunguruma mahakamani kisha anajikuta akihukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe kwa kosa la mauaji ya Kishoka, kosa ambalo alikuwa hajalitenda. Akiwa gerezani akisubiri tarehe za kunyongwa anakutana na Mack, jamaa aliyekuwa amenunua nyumba iliyokuwa ya marehemu James, naye Mack anaanza kumhadithia kisa kilichompelekea afungwe jela.
Kwa kusimuliwa na Mack, Brighton anayasikia mengi kuhusu mali alizokuwa amerithi kutoka kwa marehemu kaka yake kwa kila aliyekuwa amemuuzia aliishia kupatwa na matatizo akiwemo Mack mwenyewe. Hatima siku ya kunyongwa inafika kweli, anaambiwa akafanyishwe maungamo kwa mtumishi wa Mungu. Je, atanyongwa kweli? Sasa endelea...................

            Mara baada ya kuketi mwanamke huyo aliinua kichwa chake, mbona nilizidi kuchoka! Niliweza kumtambua barabara. Huwezi amini ndugu msomaji mwanamke huyo alikuwa ni Sharifa, mwanadada aliyenisingizia kuwa nimeua kisha akaonyesha ushahidi wa picha na kunifanya nihukuniwe kunyongwa.
            Baada ya kumuona hasira zilinijaa ghafla, nikasema potelea pote lolote na liwe, hakuna cha maungamo wala nini. Moyo wa kulipa kisasi ulinijaa mtoto wa kiume, nikatamani nimraruwe mle mle kwenye chumba hicho ili hata kama ninanyongwa na yeye awe ameshakufa.
            Hata hivyo nilipiga moyo konde na kujishauri nitulize munkari na kuzizuia papara zangu ili nimsikilize ananiambia nini.
            Aliniangalia kisha akaachia bonge la tabasamu. Hapo ndiyo niliweza kuuona uzuri wake ulivyokuwa wa shani, mtoto masharah alikuwa kamili kila idara.
            Hata hivyo sikutishika na tabasamu lake hilo kwani nilijua wazi kuwa tabasamu hilo lilikuwa ni la kinafiki. Nikazidi “kumlia buyu” nikisubiri aanzishe yeye mjadala.
Alikuwa katupia suti ya kike rangi nyeusi huku macho yake yakipendezeshwa na miwani midogo iliyokuwa imemkaa kisawasawa.
“Sharifa, leo hii wewe ndiyo mtumishi wa Mungu?” Niliamua kumuuliza bila woga baada ya ukimya mrefu kidogo kutawala.
“Tulia Brighton na unisikilize kwa makini.” Sauti nyororo ya msichana huyo ilipenya kupitia kwenye ngoma za masikio yangu, sauti ambayo ilinikumbusha ufukweni siku niliyoanza kabisa kukutana naye.
            “Hivi unajua ni kwa nini matatizo yote hayo yamekuaandama?” Alinihoji huku nami nikiwa makini kumsikiliza.
“Sijui labda uniambie wewe kwa maana umeonekana kuyasakama sana maisha yangu.” Nilijibu kwa mkato na kukaa kimya.
“Chanzo cha matatizo hayo yote ni mirathi ya kaka yako James.”
“Mirathi ya kaka yangu James! Imefanya nini?”
“Ujio wangu siyo kuja kujadili chanzo cha matatizo yako, ila nilikuwa nakutaarifu tu ili ukae unajua.”
“Kwa hiyo umekuja kufanya nini?” Nilizidi kumtwanga maswali bila woga wowote.
            “Lengo la mimi kuwa hapa ni kuja kukuokoa na adhadu ya kunyongwa kama utakuwa tayari kutekeleza masharti nitakayokuambia.”
“Masharti yapi hayo?” Nilihohoji huku hisia za wokovu wa chupuchupu nikizitazamia.
            Hata hivyo kazi ilikuwa kwenye hayo masharti. Ingawa alikuwa hajaniambia ila nilihisi yangekuwa magumu mno.
“Huhitaji kuyajua kwa sasa hayo masharti, kama upo tayari nikuokoe sema.” Aliongea Sharifa na kuzidi kuniweka katika wakati mgumu.
            Akili yangu ilikuwa ikizunguka kama korona kwa wakati huo huku nikiwaza na kuwazua ni uamuzi gani nichukue, lipi nishike na lipi niache.
            Kibaya zaidi nilikuwa sijaambiwa masharti nitakayopewa, hapo ndiyo nilizidi kuchanganyikiwa. Kuendelea kuishi nako nilikuwa bado nakutamani, isitoshe kufa kwa kunyongwa nako kulikuwa kukinitisha.
            ‘Hii ni bahati ya mtende nisiiachie Brighton mimi. Hayo masharti nitahangaika nayo mbele kwa mbele, kikubwa ni kwamba niwe nimeokoka na adhabu ya kunyongwa. Yakienda kunishinda si nakataa tu, atanifanya nini wakati gerezani tayari kashanitoa?’ Niliwaza kimoyomoyo huku nikionekana kuukubali msaada wa Sharifa.
            Nilitulia kidogo kama nawaza kitu fulani kwa kina, ghafla niligutushwa na sauti ya Sharifa iliyokuwa ikiniambia nifanye maamuzi yangu haraka kwani nilikuwa namchelewesha.
            “Sawa nimekubali niokoe” Nilijikuta najiropokea tu wala nilikuwa sijakamilisha sawasawa.
            Baada ya kuongea hivyo nilimuona Sharifa akitoa tena tabasamu lake la ukweli, tambasamu ambalo nilikuwa nikilifurahia kila alipolitoa. Aliinuka kwenye kiti alichokuwa amekaa kisha kitabu alichokuwa nacho mkononi akakitumbukiza kwenye mkoba wake aliokuwa nao. Akaja upande niliokuwa nimekaa, akaniambia nami niinuke. Nilipoinuka akanishika mkono na kuniambia tuondoke zetu.

HEHEEEH! MAKUBWA.MIRATHI YA JAMES INAMSABABISHIAJE MATATIZO BRIGHTON? PIA WATAFANIKIWA KWELI KUTOKA KWENYE NGOME YA MAGEREZA? NA KAMA WAKITOKA NI MASHARTI YAPI SHARIFA ATAMPA BRIGHTON? USIKOSE TOLEO LIJALO.

No comments:

Post a Comment