Kwa wasomaji wapya....
Brighton anajikuta akitupwa
gerezani na kuhukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe baada ya kusingiziwa
kumuua mpangaji wake kishoka. Hata hivyo mtu aliyemsingizia anaenda gerezani na
kumtorosha huku akimwambia kuwa kuna masharti atampa baada ya kukamilisha hilo
zoezi. Sasa Brighton tayari yupo uraiani na anachukuliwa na Sharifa na
kupelekwa kwenye hoteli na kuanza kuambiwa jinsi utajiri wa marehemu kaka yake
(yaani James) ulivyopatikana.......endelea
ILIPOISHIA TOLEO LILLOPITA...
Mara baada ya
kuongea hivyo alinikabidhi funguo za gari zilizokuwa mezani. Kufumba na
kufumbua alipotea ghafla, nikabaki peke yangu kwenye chumba hicho. Niliogopa
sana.
**************************
SASA ENDELEA..........
Asubuhi ilifika,
ilikuwa ni asubuhi ya kwanza kuiona nikiwa uraiani baada ya kukaa rumande na
hatimaye gerezani kwa miaka mingi. Niliamkia kwenye hoteli hiyo hiyo niliyokuwa
nimepelekwa na Sharifa jana yake.
Mara baada ya kuamka
nilitupia jicho langu kitandani kuiangalia brificase iliyokuwa imejaa mapesa
niliyokuwa nimeachiwa na Sharifa. Niliiona imetulia. Nikajiinua kisha
nikaifungua na kuiona minoti imejaa tele.
Nilipoangalia mezani
niliziona funguo za gari niliyokuwa nimeachiwa. Kwa bahati nzuri chumba
nilichokuwa kilikuwa kipo upande tuliokuwa tumeegesha gari. Nikaamua
kuchungulia nje ili kujiridhisha kama gari hilo lilikuwepo kweli. Nikaliona
limetulia.
Wazo nililokuwa nalo
usiku wakati Sharifa hajaondoka ni kukataa katakata kufuata masharti yote
niliyokuwa nikishinikizwa kuyafanya; masharti ya kuoa mwanamke kisha
akishanizalia mtoto nimtoe kafara pamoja na mtoto aliyemzaa, na baada ya hapo
niwe natoa kafara mtu mmoja kila mwaka ambaye ni mfanyakazi wangu ama mteja
wangu wa aina yoyote ile.
Hata hivyo baada ya
Sharifa kunishika kichwani muda mfupi kabla ya kuyeyuka ghafla wazo hilo nalo
liliyeyuka kabisa kichwani mwangu. Nikaanza kujiona kama mtu anayechezea
shilingi kwenye tundu la msala.
Nililipima jambo hilo
usiku kucha kwa mapana na marefu, nikaona hakuna sababu yoyote ya kulipiga teke
debe la bahati kama hilo. Kitu kilichonipa moyo ni kwamba sikutakiwa kumtoa
kafara ndugu yangu yeyote wa karibu zaidi ya mke ambaye nitamuoa kwa ajili hiyo
pamoja mtoto nitakayemzaa kwa ajili hiyo.
Nikaona ni bora
nikubaliane na shinikizo la Sharifa ili nitengeneze maisha yangu, niwe mmoja
kati ya matajiri wakubwa nchini na duniani pia. Moyo wangu uliridhia kabisa
kutajirika kwa njia hiyo, njia ya nguvu za giza na ya kishetani huku nikiwa
tayari kuendelea kuteketeza watu kila mwaka kwa kuwatoa kafara ili nizidi
kuulinda utajiri wangu huo.
Pesa nilizokuwa
nimeachiwa na Sharifa zilizidi kunipa jeuri, jeuri ya kwenda kununua nyumba
sehemu yoyote katika nchi hiyo. Jambo la kuendelea kuishi kwenye mji huo sikuwa
nalo kabisa akilini mwangu, hivyo nikaamua kuondoka asubuhi hiyo kwenda mji
mwingine uliokuwa mbali na mji huo.
Niliinuka na kwenda
maliwatoni kujimwagia maji mwilini mwangu. Nilipotoka nilivaa nguo zangu kisha
nikainua simu ya mezani iliyokuwemo hotelini humo kuangiza kifungua kinywa.
Haukupia muda sana
mlango ukagongwa, nami nilifungua na kumuona dada aliyekuwa amebeba trei
(chano) iliyokuwa imesheheni mazagazaga kwa ajili ya kifungua kinywa.
Kabla hajaondoka
nilichukua noti moja iliyokuwa na rangi ya kaki na kumpa ikiwa ni malipo ya
kifungua kinywa hicho.
“Haina haja ya kulipa maana kila kitu
kimelipiwa.” Aliniambia mwanadada huyo.
Hata hivyo ili
kumuonyesha kuwa nilikuwa ni bilionea mtarajiwa kwa wakati huo, nilimwambia
achukue tu hiyo pesa kwani nilikuwa nimeshaitoa kwenye mahesabu. Naye bila kuvunga
aliipokea, si alikuwa kapewa!
“Samahani dada yangu
kama nitakukwaza, ningependa kulijua jina lako.” Nilijikuta namchombeza zikiwa
ni harakati za kutaka kutangaza nia katika suala zima la mapenzi.
Bila kinyongo wala
malingo msichana huyo alinionyesha jina lake kwenye kitambulisho chake cha kazi
alichokuwa amekining’iniza shingoni.
Nililisoma jina na
kujikuta naachia tabasamu.
“Kumbe unaitwa Anna, jina lako lina historia
ndefu sana katika maisha yangu.”
“Historia gani tena kaka yangu?”
“Kwanza mama yangu mzazi alikuwa akiitwa jina
hilo, pili kuna msichana ambaye nilitokea kumpenda kupita kiasi naye alikuwa
akiitwa Anna, ni jina muhimu sana katika maisha yangu.”
“Kumbe! Basi na mimi naitwa hivyo!”
“Natabiri na wewe utakuwa na historia ndefu
sana katika maisha yangu,”
“Yaweza kuwa!” Aliongea Anna na kuanza kunipa
mgongo ili aondoke.
Bila kufikiri wala
kuwaza nilijikuta naropoka kumuomba namba ya simu ama mawasiliano yoyote. Pale
pale alinitolea kadi yake ya biashara (business card) iliyokuwa na kila aina ya
mawasiliano aliyokuwa akitumia.
“Asante sana mrembo!”
“Usijali!” Alimalizia maneno hayo huku
akifungua mlango na kuondoka zake.
Taratiibu kabisa
nilijongea kwenye kimeza kilipokuwepo chano cha mapochopocho ya chakula cha
asubuhi. Pasipo kuvunga nilikaa na kuanza kujichana kwa raha zangu. Kilikuwa ni
kifungua kinywa cha haja, waswahili wa siku hizi wanakwambia ‘msosi
draft’ulioenda shule.
Muda mfupi baada ya
kumaliza kushambulia kifungua kinywa niliondoka kwa mwendo wa madaha mpaka
kwenye mchuma wangu huku nikiwa nimening’iniza kibrificase changu mithili ya
kibosile ama fisadi aliyefutuka tumbo kwa kuchakachua fedha za umma.
Mpaka nafika nje
sikumuona Anna, nilitamani sana japo tupungiane mkono wa kuagana ili
nimringishie gari langu la kifahari, lakini haikuwezekana. Nadhani alikuwa
kwenye majukumu yake mengine hotelini hapo.
JE, BRIGHTON ATAMUONA TENA ANNA? NA
KAMA ATAMUONA ATAMWAMBIA NINI? FUATILIA TOLEO LIJALO!
No comments:
Post a Comment