Wednesday, December 4, 2013

MIRATHI YA KAKA toleo la 51

ILIPOISHIA TOLEO LILLOPITA...
Alirudi ndani haraka huku akiwa na hasira kisha akaufunga mlango kwa kuukomea ili kumkomoa mtu aliyekuwa akileta ubishi pale mlangoni. Sikutaka kumuuliza chochote kwani kama ningeongea basi sauti yangu ingesikika na kisha mpango wetu kubumbuluka.
SASA ENDELEA..........
Alijitupia kitandani huku akimlaumu mwanamke huyo kwa kuwa mbishi bila sababu. Huku akiwa bado analalama, tuliuona mlango ukifunguka licha ya kukomea wakati anaufunga.
 Pamoja na ubabe aliokuwa nao Benja alijikuta akinywea baada ya kuona mlango unafunguka. Hakuendelea tena kubwabwaja badala yake alibaki mdomo wazi huku hofu na woga vikimjaa.
Baada ya mlango kufunguka msichana aliyekuwa anabishana na Benja mlangoni aliingia mpaka chumbani. Kumbe alikuwa ni Sharifa, msichana aliyekuwa kanisababishia kufungwa kisha kuniokoa dakika chache kabla ya kunyongwa kitanzini.
Sasa nilikuwa nimeshaanza kumzoea msichana huyo.
“Ooh! Sharifa, kumbe ni wewe, samahani kwa yote yaliyojitokeza kwani mwenzio nalazimika kuishi kama digidigi.” Nilimwambia huku nikimlaki kwa kumkumbatia.
            Wakati huo Benja alikuwa aking’aang’aa sharubu tu, nikamtambulisha kwa Sharifa huku tukiwa bado tumekumbatiana. Alishusha pumzi kwa nguvu na kurudi katika hali yake ya kawaida.
            “Mbona unaishi kwa woga na wasiwasi hivi?” Sharifa alinitwanga swali hilo.
“Naogopa kugundulika kuwa nimetoroka jela, maana jambo hilo tulilifanya tu kwa uwezo wako ila ni la hatari mno.” Nilijibu vile.
“Wasiwasi wako tu. Hakuna mtu yeyote atakayekuuliza juu ya hilo hata kama uende gerezani hapo hapo.” Aliongea tena Sharifa kunitoa wasiwasi.
            Hata hivyo maneno yake sikuyasadiki hata kidogo ila nilikubali ili yaishe. Nilipomuomba tukae japo pale kwenye godoro ili anisaidie ushauri juu ya suala lililokuwa linaumiza kichwa changu  alikataa. Akasema alikuwa amekuja kunichukua ili tuende kumalizia maongezi yetu tuliyokuwa tumeyabakisha kule gerezani kabla ya kutoroka.
            Nilipomuuliza tunaenda kuongelea wapi aliniambia anajua yeye, nilichokuwa natakiwa kufanya ni kumfuata kokote ambako ataniambia tuende.
            Nilimuaga Benja kisha tukaondoka na Sharifa. Sikuwa na nijualo juu ya safari hiyo.  Tulipotoka nje ya nyumba alimokuwa kapanga Benja tuliingia kwenye gari moja la kifahari ambalo alikuwa amekuja nalo msichana huyo. Safari ya kuelekea nisikokujua ilianza huku dreva akiwa ni yeye.
            Baada kama ya nusu saa tulikuwa tupo kwenye hoteli moja mashuhuri sana mjini hapo. Hoteli hiyo ilikuwa siyo ngeni kwangu japokuwa nilikuwa sijawahi kuingia ndani zaidi ya kuliona jengo lake kwa nje nikiwa napita karibu nayo.
            Wakati tunashuka kwenye gari hiyo mara baada ya kufika hotelini hapo, Sharifa alichukua ‘brificase’ na kushuka nayo akiwa kaishikilia mkononi.
            Sikuelewa kama tayari alikuwa kashalipia chumba au vipi kwa sababu tulipapita mapokezi bila kusimama, tukaenda moja kwa moja kwenye lift. Tulipofika lift ikatupandisha mpaka ghorofa ya saba, tukatembea kwenye korido mpaka kwenye chumba namba 138.
            Tulipofika kwenye chumba hicho Sharifa alifungua mlango kwa kadi maalumu nao ukafunguka kisha tukazama ndani. Chumba kilikuwa matawi ya juu kweli kweli, kila huduma inayopatikana kwenye vyumba vya hoteli kubwa kubwa basi hata humo ilikuwepo.
            Kimawazo nilikuwa mbali sana wakati huo. Akili yangu ilikuwa inazunguka kuwaza ni masharti gani nitapewa na msichana huyo ikiwa ni malipo ya kuniokoa kutoka kwenye kunyongwa kwa kitanzi.
            Mwili wangu ulikuwa umezizima mithili ya mtu aliyetota kwa kunyeshewa mvua. Nilikuwa mdogo kama pilton.
            Tulipoingia tulikaa kwenye sofa za nguvu, ndipo mazungumzo yetu yalipoanza.
“Brighton mwana wa David!” Sharifa alichokoza mada kwa kuanza kuniita.
“Naam!” Niliitikia na kukaa kimya kusikilizia kitachachoongewa.
“Bila shaka unapenda sana kuwa tajiri, maana umekuwa ni mtu mwenye kujituma na kujishughulisha ukiwa na lengo la kuusaka utajiri! Kweli ama si kweli?”
“Ni kweli, lakini utajiri ninaopenda mimi ni ule wa kuupata kwa njia za halali zenye kumpendeza Mungu.”
            Baada ya kujibu hivyo nilimuona Sharifa akiangua kicheko cha dharau kisha akaendelea kusema,
“hayo ni mawazo finyu ambayo hayataleta tija katika maisha yako. Utajiri hauji kwa njia za halali hata siku moja na Mungu hawezi akakuletea utajiri. Tangu lini kitu haramu kikaja kwa njia halali?”
            Kauli hiyo iliniacha njiapanda kidogo. Ikanifanya nirejee kwenye mafundisho ya dini niliyoyapata nikiwa bado kinda wakati huo, mafundisho yaliyozungumzia matajiri wa kale ambao miongoni mwao ni kina Ibrahim na kina Ayubu, mbona wao walikuwa ni wacha Mungu wazuri tu?
            Nikakumbuka tena maneno ya Yesu kristo alipokuwa akiwaambia wanafunzi wake kuwa ni vigumu kwa tajiri kuingia kwenye ufalme wa Mungu kuliko hata kwa ngamia kupenya katika tundu la sindano.
‘Je, maneno haya huenda ndiyo yanaashiria anachokisema Sharifa?’ nilimalizia tafakuli yangu kisha nikatoa jibu kuwa si matajiri wote wanaoupata utajiri kwa njia za mkato.
            “Tuendelee!” niliropoka mara baada ya kugutuka kutoka kwenye kuwaza kwa kina.
“Huo ulikuwa ni utangulizi tu, hivyo kama unataka kuwa mmoja kati ya matajiri wa dunia hii yakubali nitakayokuambia.” Aliongea Sharifa kisha akanyosha mkono wake kuichukua brificase iliyokuwa mezani.

JE, NI MAMBO GANI BRIGHTON ATAAMBIWA NA SHARIFA AMBAYO YATAMFANYA AWE TAJIRI? USIKOSE TOLEO LIJALO!

No comments:

Post a Comment