Friday, December 6, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 52

Kwa wasomaji wapya....
            Brighton anajikuta akitupwa gerezani na kuhukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe baada ya kusingiziwa kumuua mpangaji wake kishoka. Hata hivyo mtu aliyemsingizia anaenda gerezani na kumtorosha huku akimwambia kuwa kuna masharti atampa baada ya kukamilisha hilo zoezi. Sasa Brighton tayari yupo uraiani.......endelea.

ILIPOISHIA TOLEO LILLOPITA...
“Tuendelee!” niliropoka mara baada ya kugutuka kutoka kwenye kuwaza kwa kina.
“Huo ulikuwa ni utangulizi tu, hivyo kama unataka kuwa mmoja kati ya matajiri wa dunia hii yakubali nitakayokuambia.” Aliongea Sharifa kisha akanyosha mkono wake kuichukua brificase iliyokuwa mezani.
SASA ENDELEA..........
            Aliifungua brificase na kuniambia niangalie. Naam! Ilikuwa imesheheni fedha za kigeni, fedha ambazo zilikuwa zimebanwa katika maburungutu. Nilijikuta nikimeza mate baada ya kuviona vitita hivyo.     
            “Kama utakubaliana na ninachoenda kusema basi matumizi yako kwa siku yatakuwa ya pesa kama hizi.” Mwanadada huyo alizidi kunitamanisha japokuwa nilikuwa sijajua atakachokitaka kutoka kwangu.
            Nilishusha pumzi huku nikiongeza umakini wa kumsikiliza. Nilizidi kuwa katika wakati mgumu kwa kujua kwamba kama nitamuendekeza sana msichana huyo basi pepo ya Mwenyezi Mungu nitakuwa nimeipa kisogo.
            Hata hivyo nilijiambia ngoja kwanza nimsikilize, uamuzi si ulikuwa ni wangu bwana, kama ningetaka kukubali basi ningekubali na kama ningetaka kukataa basi ningekataa.
            “Najua mwanzo ulikuwa ukinichukia sana, hasa hasa pale niliposimama mbele ya mahakama kutoa ushahidi juu ya kesi yako. Lakini sasa hivi hunichukii tena, hasa baada ya kukuokoa kutoka kwenye kunyongwa, uongo?”
“Ni kweli.”
“Mateso yote uliyokuwa ukiyapata tangu kifo cha marehemu kaka yako ulikuwa ukitumikia adhabu.”
            Maneno hayo yalinishtua na kunifanya nigutuke.
“Adhabu! Adhabu kwa kosa lipi? Na kosa hilo nilikuwa nimemkosea nani?” Niliuliza.
“Kosa hukutenda wewe bali ni kaka yako James.”
“Alitenda kosa gani kaka yangu?”
“Usiwe na pupa, nipo hapa kukufunulia kila kitu hivyo nitakueleza siri nzito aliyokuwa nayo kaka yako.”
            Hilo nalo lilikuwa neno; kujua kile kilichokuwa kimejificha nyuma ya pazia wakati wa uhai wa kaka James, nilizidi kuongeza umakini. Kikao chetu kilizidi kutia fora, sasa nikawa na shauku ya mambo matatu. Jambo la kwanza ni shauku ya kujua siri nzito iliyokuwepo kwa kaka James.
            Jambo la pili lilikuwa ni shauku ya kujua masharti ambayo nilikuwa nimeambiwa nitapewa wakati natoroshwa gerezani. Jambi la tatu ni shauku ya kutaka kujua madhara yatakayonipata endapo ningeshindwa kutekeleza masharti hayo.
            Sharifa alianza kunieleza habari ya kaka James. Habari ambayo iliyaamsha machungu ya moyo wangu, nikahisi maumivu makali yakipenya barabara kunako mtima wa moyo wangu.
            Kaka James alipokuwa anamalizia masomo yake ya kidato cha nne aliambiwa na rafiki yake mmoja kuwa kuna mganga wa kikongo aliyekuwa kaingia nchini. Mganga huyo alikuwa akiwatengenezea watu dawa ya kupata utajiri.
            Kutokana na tamaa za kutaka kupata utajiri, kaka James alimtaka rafiki yake huyo ampeleke kwa mganga huyo ili akatengenezewe dawa ya kuwa tajiri. Ndipo alipopelekwa.
            Alipofika kwa mganga huyo aliambiwa kuwa masharti ya kupata utajiri ni lazima uingie maagano na majini. Maagano hayo yalikuwa ni maagano ya kafara za damu huku yakiwa katika madaraja matatu.
Daraja la kwanza lilikuwa ni kuwatoa kafara wazazi wako wote pamoja na ndugu yako mmoja wa damu. Ndugu aliyetakiwa katika daraja hili ni mdogo wako, kaka yako ama dada yako. Kama wote hao huna basi mjomba ama shangazi hutakiwa. 
Baada ya hapo utajiri unaanza kwa kasi ya kawaida. Ukishakaa miaka mitano unatakiwa kutoa tena kafara ya mtoto wako wa kwanza pamoja na mama yake kama wewe ni mwanaume. Lakini kama ni mwanamke basi unatakiwa kumtoa mtoto wako wa kwanza pamoja na baba yake.
            Ukishakamilisha kafara za daraja la kwanza na la pili unatakiwa sasa kuhamia kwenye daraja la tatu ambalo kafara yake huendelea mwaka hadi mwaka. Kafara katika daraja hili ni ya mtu yeyote ama awe mfanyakazi wako au anayetumia vitu vyako mfano abiria katika magari yako, mpangaji katika nyumba yako na kadhalika.
            Masharti hayo ndiyo aliyopewa James naye akakubaliana nayo. Siku chake baada ya kuingia kwenye maagano yale ya kishetani wazazi wetu walikufa wote kwa mkupuo katika ajali ya kutisha.

HAYA SASA, MAMBO NDO YANAFIKIA PENYEWE, NINI KITATOKEA? USIKOSE TOLEO LIJALO!

No comments:

Post a Comment