Sunday, December 15, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 55

Kwa wasomaji wapya....
Brighton anajikuta akitupwa gerezani na kuhukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe baada ya kusingiziwa kumuua mpangaji wake kishoka. Hata hivyo mtu aliyemsingizia anaenda gerezani na kumtorosha huku akimwambia kuwa kuna masharti atampa baada ya kukamilisha hilo zoezi. Sasa Brighton tayari yupo uraiani na anachukuliwa na Sharifa na kupelekwa kwenye hoteli na kuanza kuambiwa jinsi utajiri wa marehemu kaka yake (yaani James) ulivyopatikana.......endelea

ILIPOISHIA TOLEO LILLOPITA...
Wakati nikiwa katika lindi la mawazo niligutushwa na sauti ya Sharifa. Alianza kwa kuniita jina langu.
“Brighton!”
“Naam!” Nami nilimwitikia.

SASA ENDELEA..........
“Usiwaze sana kwani kazi nzito ilishafanywa na kaka yako, unachotakiwa wewe ni kuikamilisha tu na utakuwa bilionea wa kuogopeka.” Alinyamaza kidogo kisha akaendelea.
“Daraja la kwanza utakuwa umeshalivuka kwani wazazi wa James ni wazazi wako, pia kufa kwake kutachukua nafasi ya ndugu wa karibu, kafara ambayo ilikuwa utolewe wewe. Kitakachohitajika kwako ni kuoa mke kisha mkishazaa mtoto unamtoa kafara akifuatiwa na mama yake, hapo utakuwa tayari umeshakamilisha daraja la pili.” Alipozi kidogo.
Wakati wote huo nilikuwa nimemsikiliza kwa makini. Baada ya kupozi kidogo aliendelea kuniambia kuwa nikishaimaliza daraja la pili lile lililokuwa linafuata ni mteremko. Daraja hilo ambalo ni daraja la tatu lilikuwa ni kumtoa kafara mtu mmoja kila mwaka, mtu huyo anaweza kuwa ni mfanya kazi wako ama ni mteja wako. Hiyo hatua ndiyo ilikuwa ni nyepesi kuliko zote kwani pale unamtoa mtu ambaye siyo ndugu wa karibu.
Hata hivyo bado ulikuwa ni mzigo mzito moyoni mwangu. Dhambi ya kuua nilikuwa naichukia na nilikuwa sitegemei kabisa kuitenda katika maisha yangu.
Nilivuta kumbukumbu ya maneno ya marehemu kipenzi changu Anna aliyoniambia kwenye ile ndoto niliyoota, ndoto ya kutisha. Katika maneno yake alinisisitiza sana nisiue wala kujiua kwani adhabu yake huwa ni kubwa mno.
Alinisisitiza nizidi kutenda mema huku nikiongeza upendo kwa watu wote wanaonizunguka ili siku zangu zikiisha duniani nikapumzike kwa amani na siyo kwa mateso.
Sasa mwanamke aliyekuwa mbele yangu alikuwa ananishawishi nianze kuua kwa ajili ya kupata utajiri, tena siyo kuua mara moja bali ni kuua kila mwaka mpaka pale maisha yangu yatakapofika kikomo duniani. Niliogopa sana.
Kibaya zaidi jambo lilikuwa limekaa kwenye njia panda, kama nisingefanya hivyo basi ningeuliwa mimi. Kweli maisha ni matamu sana mithili ya asali mwitu japokuwa ni mafupi zaidi ya watu wa Uturuki.
Hapo ndipo nilizidi kuumiza kichwa. Lakini kumbukumbu ya maneno ya marehemu Anna ilionekana kunipa nguvu. Nikajisemea kimoyomoyo kuwa ni bora nife kuliko kubeba dhambi mbaya na nzito kama hiyo, dhambi ya kuua.
Nikiwa katika kuwaza wazo lilinijia, nikaliona linafaa kulifanyia kazi. Nikataka kufumbua kinywa changu ili nieleze msimamo wangu juu ya jambo lililokuwa lipo mbele yangu. Kabla sijaongea chochote nilimuona Sharifa akisimama na kuniwekea mkono wake kichwani. Mwili wote ulisisimka, nikajihisi kama nimepigwa shoti ya umeme.
Alipotoa mkono wake juu ya kichwa changu aliniambia gari tuliyokuwa tumeenda nayo hotelini hapo imekuwa yangu kuanzia wakati huo. Pia akaniambia pesa zote zilizokuwemo kwenye brificase iliyokuwa mezani zote ni zangu.
Mara baada ya kuongea hivyo alinikabidhi funguo za gari zilizokuwa mezani. Kufumba na kufumbua alipotea ghafla, nikabaki peke yangu kwenye chumba hicho. Niliogopa sana.

                        **************************   

ITAENDELEA..........  

No comments:

Post a Comment