Thursday, December 12, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 54


Kwa wasomaji wapya....
            Brighton anajikuta akitupwa gerezani na kuhukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe baada ya kusingiziwa kumuua mpangaji wake kishoka. Hata hivyo mtu aliyemsingizia anaenda gerezani na kumtorosha huku akimwambia kuwa kuna masharti atampa baada ya kukamilisha hilo zoezi. Sasa Brighton tayari yupo uraiani na anachukuliwa na Sharifa na kupelekwa kwenye hoteli na kuanza kuambiwa jinsi utajiri wa marehemu kaka yake (yaani James) ulivyopatikana.......endelea.
ILIPOISHIA TOLEO LILLOPITA...
Hayo ndiyo mambo yaliyosababisha kifo cha wazazi wangu pamoja na kaka yangu. Tamaa ya kaka yangu kupata mali nyingi kwa njia ya mkato ndiyo iliyagharimu maisha yake na ya wazazi wetu kwa ujumla. Habari hiyo yote mimi nilikuwa siijui ila Sharifa ndiye aliyekuja kuning’amua.

SASA ENDELEA..........

Pamoja na maelezo hayo kuhusu kifo cha kaka James nilikuwa bado na maswali mengi sana kichwani mwangu. Maswali menyewe ni pamoja na yeye Sharifa anahusika vipi na kafara hiyo ama ana uhusiano upi na mganga wa kaka James?
Pia swali jingine lililokuwa limetanda kwenye ubongo wangu ni kwamba mimi kosa langu lilikuwa ni lipi hapo wakati aliyefanya maagano na mganga ni kaka yangu tu? Sikuwa na majibu yake ila niliamini kuwa maswali hayo yangejibika kwa Sharifa.
Sikusita kumuuliza kwani mpaka wakati huo nilikuwa nimemzoea na kumuona kama alikuwa ni mtu wa kawaida wakati alikuwa si wa kawaida.
Nilianza na kutaka kujua hao wataalamu hasa ni kina nani na wanapatikana wapi? Swali lilijibiwa. Nikaambiwa kuwa wataalamu ni wale viumbe waliokuwa wamemuweka mganga huyo ili aweze kufanya mawasilo nao katika kumpatia mtu utajiri aombapo. Sikutaka kuendelea tena kudodosa juu ya swali hilo kwani tayari niling’amua kuwa wataalamu hao ni majini ama pepo wachafu.
Nikahamia kwenye swali la pili ambalo ni kutaka kujua Sharifa anahusikanaje na huyo mganga. Alichonijibu wala sikukitila shaka, nikaachana na swali hilo mara baada ya kupewa jibu.
“Na wewe una shirika gani na yule mganga?”
“Ni mmoja kati ya wataalamu wake. Na mimi ndiye nilichaguliwa kuhakikisha James anaaga dunia pamoja na kukuandama wewe ili tukutie adabu, na ukiwa mgumu wa kuelewa utamfuata kaka yako aliko.”
            Sikutaka hata kuendelea kudodosa kwani majibu yenyewe yalikuwa yanajitosheleza. Tangu mwanzo wa kuniandama mpaka kunitoa jela nilikuwa nimeshabaini kuwa Sharifa hakuwa kiumbe wa kawaida. Alikuwa ni jini.
            Hofu ilizidi kujengeka alipotamka kauli ya kwamba hata mimi nikileta za kuleta atanitia adabu ya kumfuata kaka James alikokuwa. Tafsiri ya maneno hayo ilikuwa ni kwamba ataniua kwani James hakuwa Marekani wala Dubai bali alikuwa kuzimu.
            “Kosa langu hapo mimi ni lipi mpaka uniandame hivi?”
“Mirathi ya kaka yako.” Alijibu kwa mkato kisha akafunga bakuli lake, yaani namanisha akanyamaza kimya.
            Bado kichwa changu kilikuwa na maswali ya kumhoji Sharifa. Mirathi ya kaka ilikuwa imefanya nini? Nilizidi kuwaza kabla sijalitupia swali hilo kwa Sharifa.
            Nilipomuuliza alinijibu kuwa mali ya aina hiyo huwa haitakiwi kurithiwa na mtu yeyote yule. Nilifanya kosa kubwa sana kurithi mali alizokuwa ameziacha kaka James wakati zilikuwa ni za maagano.
            Mpaka hapo niliweza kuelewa kiini cha matatizo yangu. Nilijikuta nikianza kujuta kurithi hizo mali pamoja na kuzaliwa pia. Niliweza kubashiri hatari iliyokuwa inaninyemelea mbele yangu huku chanzo chote kikiwa ni mirathi ya kaka James.
            “Kumbe chanzo cha misukosuko yote hii ni hicho, sasa utanisaidiaje ili nijinasue kwenye hili balaa?” Niliamua kumuuliza hivyo ili nijue hatima yangu.
“Dawa ya hapo ni moja tu”
“Ipi hiyo?”
“Kufanya yale yote tunayokutaka uyafanye, zaidi ya hapo anza kujihesabu kuwa ni marehemu mtarajiwa.”
            Hakuna anayependa kufa jamani. Sikujua nifanye nini ili kujinasua kwenye urimbo niliokuwa nimenasa. Kuendelea kuishi nako nilikuwa bado nakutamani. Sasa nilizidi kuwa katika wakati mgumu.
            Maelezo ya mwanadada huyo hayakuwa na chembe ya utani ndani yake hata kidogo. Alichokuwa anakisema alikuwa anakimaanisha. Uwezo wa kufanya hivyo alikuwa nao.
            Tulibaki tukiwa tumetumbuliana macho, mimi nikiwaza yangu kutokana na uzito wa jambo ulivyokuwa. Nilikuwa najiona dhahiri ninavyodumbukia kwenye shimo lenye kina kirefu nisiloweza kutoka tena.
            Wakati nikiwa katika lindi la mawazo niligutushwa na sauti ya Sharifa. Alianza kwa kuniita jina langu.
“Brighton!”
“Naam!” Nami nilimwitikia.

“JE,  SHARIFA ATAMWAMBIA NINI BRIGHTON? Tukutane kwenye toleo lijalo.

No comments:

Post a Comment