Tuesday, September 17, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 16




ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA......
Niliamua kujinyamazia kwa kuhofia kupewa mikong’oto na maafande hao walioonekana kupinda kuzidi maelezo. Alama za mia moja kumi na moja zilizokuwa zimejichora kwenye mapaji ya nyuso zao kwa kukunja ndita zilikuwa zinanitisha.
SASA ENDELEA.......
            Nilitulia na kuamua kuvuta kumbukumbu mwenyewe ili niweze kung’amua kilichotokea na kuniweka matatani kiasi kile. Kumbukumbu zangu zilianza kuniijia kwa mbaali, nilijaribu kuwa makini ili niweze kuyakumbuka matukio yote yaliyokuwa yametendeka tangu asubuhi kwenye mizunguko yangu.
            Nilikumbuka jinsi nilivyoshuhudia kioja cha mwanadada wa asubuhi, mwanadada aliyekaribishwa na Kishoka akakataa kuingia ndani kisha nilipoenda kumwangalia sikumkuta. Kumbukumbu zilizidi kutiririka sasa kwenye fikira zangu, nikakumbuka jinsi nilivyoachana na kioja cha dada huyo na kuondoka zangu.
            Ratiba nzima ya mizunguko yangu nilifanikiwa kuikumbuka kwa marefu na mapana, niliendelea kukumbuka nilivyopigiwa simu na Kishoka wakati narudi nyumbani akaniambia kuwa mgeni wa asubuhi ananisubiri.
Mpaka nilipofika getini na kuongea naye dada huyo kwa njia ya simu akiniaga kuwa anaondoka kwa madai ya kuchoka kunisubiri, licha ya kumbembeleza kwa kumwambia kwamba nilikuwa getini lakini bado mwanadada huyo aligoma kunisubiri.
            Mpaka naingia ndani kwangu sikuweza hata kumuona japokuwa nilitegemea ningekutana naye. Kumbukumbu ziliendelea kutiririka mpaka nilipoingia chumbani kwangu na kumkuta Kishoka kauawa juu ya kitanda changu.
            Wakati nikitafakari la kufanya watu wawili waliingia na kuniweka chini ya ulinzi. Hapo ndipo kumbukumbu zangu zilifikia kikomo, sikukumbuka tena kilichoendelea zaidi ya kujikuta nipo kwenye mahakama ya magonjwa, sehemu ambayo magonjwa yote yanayowasumbua binadamu hushtakiwa na kutolewa hukumu, yaani namaanisha hospitalini.
            ‘Sasa nimeelewa, nitakuwa ninadhaniwa kumuua Kishoka. Muuaji atakuwa ni yule mwanamke, lakini lazima nishakiwe mimi kutokana na mazingira ya kifo chenyewe; kweli leo nimeamini kuwa akamatwaye na manyoya ndiye mwizi wa kuku.’ Nilijisemea kimoyomoyo baada ya kukumbuka mkanda wa tukio zima.
            Nilianza kujuta kumfahamu msichana huyo, nilijilaumu mno kwa kumsemesha kule ufukweni siku niliyoanza kumuona. Kama nisingemsemesha huenda yasingetokea haya, ama kweli siku zote busara huja baada ya kutenda.
            ‘Hivi tukio hili ni la kweli au naota?’ Niliendelea kuwaza.
‘Lakini hii siyo ndoto, hii ni ‘laivu’, tena ni ‘laivu’ bila chenga.’ Nilijikuta nikijijibu mwenyewe.
            Niliamua kumwachia Mungu kwani yeye ndiye mweza wa yote, yeye ndiye alikuwa anajua suluhisho la kesi iliyokuwa inanikabili, kesi ya mauaji ambayo sikuhusika nayo hata kidogo. Nilijipa matumaini kuwa maadamu sina hatia basi Mungu atakuwa na mimi.
            “Afande, kama vipi richukue maerezo maana tayari rimeshazinduka.” Alisikika afande aliyekuwa ameshikilia bunduki akimwambia mwenzake ambaye alikuwa kashika faili mkononi.
“Hamna tabu afande, hata mimi nilikuwa ninalifikiria hilo kichwani mwangu.” Alijibu afande huyo.
JE, KATIKA KUCHUKULIWA MAELEZO BRIGHTON ATASEMAJE KUHUSU KUUAWA KWA KISHOKA? ITAENDELEA........

No comments:

Post a Comment