Monday, September 30, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 22



ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA....
Vijana hao niliwafananisha na mazuzu ambao mishipa ya fikra ilishakatika kichwani mwao. Rumande siyo sehemu ya kukimbilia kama una akili yako timamu.

                                    *************************
SASA ENDELEA.......            
Watu walikuwa wamefurika  kusikiliza kesi mbalimbali zilizokuwa zikiunguruma katika mahakama kuu ikiwemo kesi yangu. Kesi nyingi zilizokuwa zikitajwa siku hiyo zilikuwa ni za mauaji.
            Wakati huo nilikuwa nipo kwenye kizimba cha washtakiwa nikiapishwa. Mara baada ya kuapishwa, kesi ilisomwa.
            “Ni kweli au si kweli?” Lilikuwa ni swali la mwendesha mashitaka Charles Ngonyani ambaye alikuwa ni wakili wa serikari.
            Hata hivyo wakili wangu bwana Jonas Mlyanyama aliniambia nikane, nami nikatikisa kichwa kukataa kisha nikasema,
“si kweli”
            Baada ya hapo kesi iliahirishwa tena kwa muda wa wiki moja ili upande wa mashtaka uanze kupeleka mashahidi wake.
            Nilirudishwa tena gerezani nikiwa bado mahabusu. Mpaka hapo nilikuwa nimeshaipata freshi ya kwenda na kurudi mahakamani, kesi yenyewe ilikuwa haijaanza hata kusomwa.
            Niliendelea kukaa rumande mpaka siku ya kesi yangu ikawadia tena. Siku ilipofika kama kawaida karandinga la magereza lilitusomba mpaka mahakamani mahabusu ambao kesi zetu zilikuwa zinasomwa siku hiyo.
            Shahidi aliyeanza kutoa ushahidi kutoka upande wa mashitaka alikuwa ni Sajenti Bakari Mlongo ambaye ndiye alikuwa amelibeba jukumu la kuipeleleza kesi yangu.
            Huku akiongozwa na wakili wa serikali, Sajenti Bakari Mlongo alieleza kuwa siku ya tukio akiwa kazini kwake kwenye kituo cha polisi cha kati alipigiwa simu kupitia simu ya kazini na mwanamke mmoja ambaye alijitambulisha kuwa ni ndugu yake na Kishoka.
“Baada ya mpigaji kujitambulisha hivyo aliwaambia nini?” Aliuliza wakili wa serikali bwana Charles Ngonyani.
“Mtu huyo alieleza kuwa kuna mauaji ya kutisha yaliyokuwa yamefanyika kwenye nyumba ya bwana Brighton David.” Alisikika Sajenti Mlongo akijibu.
“Mtu huyo alieleza kuwa nani kauawa?”
“Ndiyo alieleza. Alisema kuwa aliyekuwa ameuawa ni ndugu yake aitwaye kishoka.”       
Sajenti Mlongo aliendelea kueleza kuwa baada ya kuambiwa hivyo alitoka yeye na askari wengine wanne na kuelekea kunako eneo la tukio.
“Mlifika mpaka eneo la tukio?”
“Ndiyo tulifika.”
“Ikawaje?”
“Kwanza tulilikuta geti la ngome ya nyumba hiyo lipo wazi, tulipofika kwenye mlango wa kuingilia wa nyumba ya mtuhumiwa tuliuona uko wazi. Ndipo tulipoingia kwa tahadhari kubwa. Hata hivyo pale ukumbini hakukuwa na mtu zaidi ya runinga iliyokuwa imewashwa.”
“Baada ya kuona hapana mtu sebuleni mlichukua uamzi gani?”
“Tulijaribu kuangaza na kubaini kuwa mlango wa chumba kimojawapo kwenye hiyo nyumba  ulikuwa wazi na taa ilikuwa ikiwaka. Ndipo mimi na afande mmoja tuliingia kwenye chumba hicho.”
“Endelea kuieleza mahakama mlichokikuta baada ya kuingia kwenye chumba hicho!”
“Tulimkuta mtuhumiwa ambaye ni bwana Brighton akizunguka zunguka humo chumbani huku mwili wa Kishoka ukiwa kitandani huku kichwa kikiwa mbali na kiwiliwili chake. Vile vile kisu ambacho tulishuku kutumika katika kutekeleza mauaji hayo kilikuwa kikiambaa ambaa sakafuni.”
“Baada ya kuona hivyo mlichukua uamuzi gani?”
“Tulimuweka chini ya ulinzi mtuhumiwa, lakini kabla hatujamfunga pingu alianguka ghafla na kupoteza fahamu.” Aliongea Sajenti Mlongo.
“Huyo mtuhumiwa mliyemkamata siku hiyo ukimuona unaweza kumtambua?” Aliuliza wakili Charles Ngonyani.
“Ndiyo ninaweza.”
“Hebu ionyeshe mahakama tukufu mtu huyo kama yumo humu!”
“Yule pale kwenye kizimba.” Sajenti Mlongo aliongea huku akinisonta pale nilipokuwa.
            Wakili wa serikali bwana Charles Ngonyani alimtazama hakimu na kumwambia,
“Nimemaliza!” aliongea na kwenda kuketi.
KESI HII ITAISHAJE? USIKOSE SEHEMU YA 23!

No comments:

Post a Comment