Friday, September 6, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 5



ILIPOISHIA........
Kumuona tena huyo jamaa ndiyo kulinifanya nitabasamu kwani nilikumbuka visa na vituko alivyokuwa akivifanya kipindi cha uhai wake.

SASA ENDELEA.......
Jamaa huyu ni Patrick, Patrick Chibehe; kijana wa kihehe aliyetia fora kwa madeni pale mtaani kwetu. Walipokusanyika watu watano basi watatu au wanne walikuwa wakimdai.
Ulevi wake wa pombe ya kienyeji ijulikanayo kama mabonge ndiyo uliomfanya awe na madeni lukuki. Wakati mwingine alidiriki kuuza hata nguo alizokuwa amevaa kisha kubaki kifua wazi au kubaki na kaputura tu ili apate pesa ya kununulia pombe.
Vituko alivyokuwa navyo wakati wa uhai wake ndivyo vilivyonifanya niachie tabasamu likifuatiwa na kutikisa kichwa. Nilikumbuka jinsi alivyotuingiza mjini kwa kutuuzia TV moja watu watatu tofauti.
Kumbukumbu zilizidi kunijia jinsi kijana huyu alivyopoteza uhai wake kimzaha mzaha. Aliamua kujinyonga kwa kutumia mkanda wa suruali yake baada ya kuambiwa kuwa wadai wake tumemshitaki kituo cha polisi. Aliona njia pekee ya kujiokoa na hilo janga ni kujinyonga.
Kwa kweli nilishindwa kabisa kuamini kwa hicho nilichokuwa nakiona, nikabaki nikijiuliza kwa nini kila niliyemtambua katika kundi hilo alishakufa. Nilianza kufikiria kuwa labda hata wale wengine ambao nilikuwa siwatambui katika hilo kundi walikuwa wameshakufa.
‘Kwa hali kama hii huenda hata wazazi wangu nitawaona.’ Wazo hilo lilinijia baada ya kuwaona mzee Mboma, kaka James pamoja na Patrick.
Niliendelea kukodoa macho walipokuwa watu hao, nikazidi kuumia kutokana na vilio walivyokuwa wakivitoa. Nikazidi kujiuliza;
‘Watu husema kuwa mtu akifa huenda kupumzika kwa amani, mbona sasa hawa wanalia?’ Nilikosa jibu kabisa.
Nilikomaa kuangaza angaza nikijipa moyo ya kwamba huenda nitamtambua mtu mwingine, hasahasa shauku yangu ilikuwa ipo kwa wazazi wangu waliofariki kitambo nikiwa bado nipo darasa la tatu. Pamoja na kukodoa kwangu macho niliambulia kapa, sikufanikiwa kuwaona baba yanga na mama yangu katika kundi hilo.
Katika harakati za kuhangaika kutafuta mtu mwingine ambaye ningeweza kumfahamu kutoka kwenye hilo kundi, nilimuona mtu ambaye aliamsha machungu ndani ya mtima wangu. Donda lililokuwa limeanza kupona moyoni mwangu sasa lilitoneshwa tena na kitendo cha kumuona mtu huyu, tena lilitoneshwa kwa msumari wa moto.
Niliyasikilizia maumivu hayo yazidiyo maumivu ya mwanamke anayeumwa na uchungu wa kujifungua, hasa uchungu wa mimba ya kwanza.
Marehemu Anna, aliyekuwa kipenzi cha moyo wangu, ndiye niliyemuona kwa wakati huo. Naye alikuwa analia kama walivyokuwa wanafanya wale wengine katika hilo kundi. Nilivuta na kushusha pumzi, nikakodoa macho pima zaidi ya vile nilivyokuwa nimekodoa mwanzo huku mdomo ukiwa wazi!
‘Ama kweli leo ndiyo leo, ngoja nisubiri hatima yake.’ Niliwaza kimoyomoyo huku mdomo ukiendelea kuwa wazi, kamasi pamoja na machozi vilianza kunitoka hata sikuwa na muda wa kuviondoa badala yake nilizidi kuviachia vitiririke mpaka basi.
ITAENDELEA.......

No comments:

Post a Comment