Wednesday, September 11, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 11



ILIPOISHIA........
Nilijaribu kuangaza kwenye njia lakini sikuona mtu. Nikaamua kurudi ndani kuendelea kushambulia boflo zangu na supu yangu ya kuku.
SASA ENDELEA.......
            Wakati namalizia zoezi nililokuwa nalo, zoezi la kupata kifungua kinywa, simu yangu ya mkononi ilianza kuita. Niliangalia namba iliyokuwa inanipigia lakini nilishindwa kuitambua, yaani ilikuwa ni namba ngeni ambayo haijahifadhiwa katika simu yangu. Taratibu nilibofya kitufe cha kupokelea kisha nikapeleka simu sikioni.
            Sauti nyororo ilisikika kwenye spika za simu yangu, sauti iliyokuwa ikijitambulisha kuwa ni mtu niliyeongea naye jana kule ufukweni. Nilipomuuliza yuko wapi aliniambia yupo nyumbani kwao hivyo miadi yetu angependa iwe muda wa jioni.
Nilijaribu kumuuliza kama alikuwa kaja nyumbani kwangu muda mfupi uliopita, naye aliniambia hajaja. Pia aliongezea kuwa mpaka muda huo ananipigia simu alikuwa bado yupo kitandani wala hajaachana na shuka.
            Kwa kweli nilianza kuchanganyikiwa upya, Kishoka alipoenda kufungua geti alimkuta dada aliyedai kuwa nilionana naye jana kule ufukweni, huyo aliyenipigia simu naye alijitambulisha kuwa nilikuwa naye ufukweni siku iliyopita.
            Nilishindwa kuelewa jinsi mambo hayo yalivyokuwa yakienda,
‘ufukweni mimi niliongea na msichana mmoja tu, msichana ambaye alikuwa hataki hata kugeuka kunitazama. Sasa mbona wamefika wasichana wawili wanaodai tumeonana ufukweni?’ Niliendelea kuumiza kichwa nikiwaza juu ya tukio hilo la kushangaza na kustaajabisha.
            Hata hivyo nilishindwa kupata jibu. Niliishia kubetua mabega huku akili yangu ikizidi kuchoka kutokana na maajabu hayo. Niliamua kuachana na suala hilo, nikaingia chumbani kwangu kujiandaa ili nitoke kuelekea katika mizunguko ya kila siku kwani tayari nilikuwa nimeshamaliza kustaftahi.
            Wakati nikiwa chumbani mlango wa chumba changu ulianza kugongwa. Nami nilienda kufungua ili nimuone aliyekuwa anagonga. Nilimkuta Kishoka yupo pale mlangoni.
“Kaka umesema ulipoenda getini hukumuona yule shori, mbona mpaka sasa hivi bado yupo?” Lilikuwa ni swali la Kishoka aliloniuliza baada ya kufungua mlango.
            Taarifa hiyo ilizidi kunishtua, nikaanza kujawa na wasiwasi na hofu fulani. Hata hivyo nilijikaza kiume na kumwambia Kishoka tuende wote mpaka getini tukahakikishe kama kweli kuna mtu.
            Tuliondoka kuelekea getini, tulipofika hatukuona mtu yeyote, tuliangalia njiani lakini hatukuona hata dalili za mtu kuondoka getini muda mfupi uliopita. Tulibaki tukiangaliana bila kuongea chochote. Tukio hilo lilikuwa geni kabisa nyumbani kwetu.
            Pale getini hapakuwa na sehemu ya kusema kwamba labda mtu huyo alikuwa anajificha, palikuwa ni peupe kabisa. Sasa hata Kishoka naye alianza kuigiwa na wasiwasi.
            Kutoka hapo getini sikutaka hata kurudi ndani. Nilimwambia Kishoka akaufunge mlango wa chumbani kwangu kisha anichukulie funguo zangu zilizokuwa zikining’inia kwenye mlango wa chumba changu, naye akaenda.
Punde si punde Kishoka alirudi na kunipa funguo zangu. Aliponikabidhi niliondoka zangu kuelekea mitaani huku nikimuacha yeye yupo hapo nyumbani.
HAYA NDUGU MSOMAJI, MWANADADA ANAZIDI KUWACHANGANYA AKILI BRIGHTON NA KISHOKA, JE NINI KITAENDELEA?
           

No comments:

Post a Comment