Wednesday, September 4, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 4



ILIPOISHIA........
Kushindwa kwenda kumkumbatia ndugu yangu huyo wa damu kuliniumiza sana moyoni. Nilishindwa kupata uhakika ya kwamba na yeye alikuwa kaniona au la! Tatizo hata kuongea kwenyewe sikuweza, japo ningemuita kwa sauti natumai angenisikia.

SASA ENDELEA.......
Mtu huyu si mwingine bali alikuwa ni kaka yangu James, ndugu wa damu tumbo moja japokuwa baba tofauti. Mtu aliyeonyesha umuhimu mkubwa sana baada ya wazazi wangu kufariki.
Hakupenda kabisa kuniona nikihangaika ama kusumbuliwa na shida yoyote katika dunia hii, siyo siri alinipenda sana  kaka James.
Upendo ulioshibishwa na udugu wetu ndiyo ulionifanya nimuone mtu muhimu sana chini ya jua. Kila msaada niliomuomba alinisaidia, iwe wa kifedha ama wa kimawazo.
Kwa kuwa hata vikombe hugongana kabatini; siwezi kusema kwamba mimi na James hatukuwa tukikoseana. Pindi tulipokoseana tulisameheana bila kujali ukubwa ama udogo wa kosa jenyewe. Msamaha wetu ulikuwa  wa kweli pindi tuliposameheana. Hakika tuliishi maisha ya amani na furaha siku zote, vicheko na matani ya kawaida vilitawala kila tulipokuwa pamoja.
Hata kilipotokea kifo chake sikuweza kujikaza, niliumia sana moyoni mpaka nikafikia hatua ya kupoteza fahamu. Fahamu ziliniijia baada ya masaa matano, nilipozinduka nikashangaa kujikuta nipo hospitali. Niliangaza huku na huko bila mafanikio ya kumuona nesi wala daktari zaidi ya wagonjwa wenzangu waliokuwa wamelala katika vitanda vyao kila mmoja.
Kumbukumbu za kifo cha kaka James zilinifanya nishindwe kuutambua umuhimu wa drip ya maji niliyokuwa nimetundikiwa na kuanza kukimbia kwenda kumzika kaka yangu mpendwa, ndugu yangu wa pekee aliyekuwa mtegemewa katika maisha yangu.
James alichukua uamuzi wa kujiua kutokana na kusalitiwa na mwanamke ambaye alikuwa ni mchumba wake, mwanamke ambaye alimwamini kupita maelezo; akamnunulia nyumba ya kifahari pia na gari zuri la kifahari. Wakaanza mikakati ya kuoana wakaishi pamoja kwenye hilo jumba la kifahari waendelee kuponda mali wakiamini kabisa kuwa kufa kwaja.
Moyo wa James uligongomewa mwiba wa sumu alipomkuta mwanamke huyo yupo na kibwana kingine.
Kibaya zaidi mwanamke huyo baada ya kufumwa alijibu utumbo kwa  James na kumwambia hamtaki tena wala hana mpango wa kuolewa nayeye.
Mpaka naingia kaburini mwanamke huyo nitakuwa namfananisha na nyoka ndumilakuwili, tena mwenye sumu kali. Hii yote ni kutokana na kupoteza dira ya maisha yangu kwa kuiangusha nguzo niliyokuwa nimeegemea ambayo ni kaka James.
Mwanamama huyo ilibidi amweleze bayana James kuwa hakuwa na mapenzi ya dhati kwake. Pia alizidi kujifaragua kuwa alijifanya anampenda ili amchune kisawasawa. Baada ya kuridhika kuwa amemchuna vya kutosha ; pesa, nyumba pamoja na gari , mwanamke huyo aliamua kusema ‘byebye’ kwa kaka James na kukitangaza rasmi kimjamaa alichokuwa nacho kuwa hicho ndiyo kimume chake kitarajiwa.
Maneno kama yale yenye kejeli za kila namna yalimkasirisha sana James. Hasira ziliuzidi uwezo wake wa kufikiri, na ndipo alipoamua kufanya mauaji ya kinyama kwa  mwanamke huyo pamoja na kimjamaa kile kwa kuwatwanga risasi kila mmoja.
Alipomaliza kufanya tukio hili, moyo wa woga ulimwijia hatiye ukauzidi uwezo wa kuamua. Akaona suluhisho la tatizo lake ni kujimaliza hata yeye pia. Ndipo alipoamua kujifyatua risasi ya kichwa na kufa papo hapo.
Nikiwa bado nimeukodolea macho umati wa watu waliokuwa wamefariki kitambo, akiwemo kaka yangu James, machozi yalizidi kunitiririka mithili ya mto usiokauka kila msimu. Nguvu za kumsogelea nazo sikuwa nazo, nikabaki nikisaga meno na kutikisa kichwa huku niking’ata kidole changu cha shahada na kuendelea kutikisa kichwa. Kufanya hivyo kote hakukusaidia chochote, mambo yalikuwa bado yako palepale, sikuweza kuongea wala kunena chochote.
Nilipumua kwa nguvu, sijakaa sawa nikamtambua mtu mwingine. Nilishindwa kujizuia baada ya kumuona mtu huyo, nikajikuta nikitabasamu.
Kutabasamu kwangu hakukuashiria kuona mlango wa wokovu kwa tatizo lililokuwa likinikabili; tukio lenye maajabu, vitisho na mikikimikiki ya kila aina. Kumuona tena huyo jamaa ndiyo kulinifanya nitabasamu kwani nilikumbuka visa na vituko alivyokuwa akivifanya kipindi cha uhai wake.
ITAENDELEA..........

No comments:

Post a Comment