Thursday, September 12, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 12



ILIPOISHIA........
Punde si punde Kishoka alirudi na kunipa funguo zangu. Aliponikabidhi niliondoka zangu kuelekea mitaani huku nikimuacha yeye yupo hapo nyumbani.
SASA ENDELEA.......
Wakati wa jioni nikiwa narudi nyumbani nilipitia sokoni kununua matunda, nikiwa sokoni nilimuona msichana mmoja, msichana huyo alikuwa anafanana sana na yule niliyemuona  kule ufukweni. Siyo kwa sura tu, bali mpaka mavazi aliyokuwa amevaa siku ile ufukweni.
            Nilimsogelea na kumwambia dada mambo naye akanijibu poa. Baada ya kuisikia sauti yake nilibaini kitu, sauti hiyo haikuwa na tofauti na sauti ya msichana aliyekuwa akinizingua kule ufukweni, yaani sauti ileile ya mwanadada niliyekutana naye nikaanza kumuita asikubali hata kunisubiri.
Sauti yake hiyo iliyokuwa nyororo kiasi kwamba hata kama ulikuwa na homa ukiisikia tu unapata afueni. Sauti ambayo husemekana inauwezo wa kumtoa chura mtoni aisikiapo.
            Nilijikakamua na kumuuliza kama alikuwepo ufukweni jana yake. Akakanusha kanu na kusema yeye huwa hana kawaida ya kwenda ufukweni. Nilimuuliza tena kama ananifahamu mimi naye akasema ilikuwa ndiyo mara yake ya kwanza kuniona. Niliamua kuachana naye baada ya kukumbuka usemi wa wahenga usemao kuwa duniani wawili wawili.
            Lakini sura yake, nguo alizokuwa amevaa pamoja na sauti yake havikuwa na tofauti hata kidogo na yule msichana  wa ufukweni. Nilibaki kuwaza huku nikiendelea na safari yangu ya kurudi nyumbani.
            Nikiwa njiani simu yangu ya kiganjani ilianza kuita, nikaitoa mfukoni na kuangalia namba ya aliyekuwa ananipigia. Nilibaini kuwa kumbe alikuwa ni Kishoka, nilibonyeza kitufe cha kupokelea kisha nikamsikiliza alichokuwa anasema.
            “Kaka uko wapi?” Aliniuliza nami nikamjibu nipo njiani kuelekea nyumbani. Baada ya kumjibu hivyo aliniambia kuwa msichana aliyezuru kwetu asubuhi alikuwa kaja tena na alikuwa ananisubiri. Nilimwambia nipo karibu kufika kisha nikakata simu na kuirudisha mfukoni.
            Nililazimika kuongeza mwendo kama si kuanza ‘kutroti’ ili nimuwahi mgeni wangu niliyeambia ananisubiria, mgeni ambaye tangu jana alikuwa ananizingua kule ufukweni. Wakati mwingine woga flani ulianza kuniingia kutokana na maajabu aliyokuwa ananionyeshea tangu asubuhi.
            Nilipofika mita chache kutoka kwenye geti la nyumba yangu simu yangu ilianza kuita tena, nilipoiangalia namba niliikumbuka. Namba hiyo ndiyo iliyokuwa imetumiwa na msichana huyo kunipigia asubuhi akidai miadi yetu iwe jioni.
            Niliipokea na kusikiliza kilichokuwa kinasemwa, mwanadada huyo alilalamika sana akidai nimechelewa. Nilimwambia avute subira kidogo kwani mimi nilikuwa tayari nipo getini kwa wakati huo.
Msichana huyo alikataa katakata kuningoja akidai kwamba nimechelewa, muda aliokuwa ameutenga kwa ajili ya miadi yetu ulikuwa umeisha.
            Huku nikifungua geti nilijitahidi kumsihi anisubiri japo kwa muda wa dakika sifuri kwani nilikuwa nipo getini, hata hivyo aliendelea kushikilia msimamo wake akidai ndiyo anaondoka ndani na hawezi kurudi tena.
Kauli hiyo ndiyo aliyomalizia kuongea kisha akakata simu. Huku nimeshikilia simu mkononi nilifunga geti na kuelekea ndani haraka haraka kumwahi mgeni wangu ambaye alikuwa kacharuka kuondoka.
            Nilijipa matumaini kwamba ningekutana naye nje ya nyumba akielekea getini ama ningekutana naye mlangoni. Na kama ningekutana naye basi ningejaribu kumbembeleza ili arudi tena ndani japo dakika tatu ndipo aende zake, lengo langu ni kutaka kumuona kwenye mwanga ili nimfaidi, nikishamuona basi hata aende zake.
            Mpaka nafika mlangoni sikukutana na mtu, nilifungua mlango na kuingia ndani nikijua kuwa mgeni wangu huyo alikuwa kanielewa na kuamua kunisubiri. Wakati nafungua mlango jicho lilikuwa ‘busy’ kuangalia kwenye sofa ili nimuone mgeni wangu.
HAHAAAA! HAPO PATAMU MPENZI MSOMAJI, BRIGHTON ATAMKUTA HUMO NDANI HUYO MGENI WAKE? USIKOSE SEHEMU YA 13

No comments:

Post a Comment