Saturday, September 14, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 13


ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA......    
Mpaka nafika mlangoni sikukutana na mtu, nilifungua mlango na kuingia ndani nikijua kuwa mgeni wangu huyo alikuwa kanielewa na kuamua kunisubiri. Wakati nafungua mlango jicho lilikuwa ‘busy’ kuangalia kwenye sofa ili nimuone mgeni wangu.
SASA ENDELEA.......
Tofauti na matarajio yangu, jicho langu halikuona chochote kwenye sofa, kulikuwa ni kweupe. Hapakuwa na mgeni wala Kishoka lakini tv ilikuwa inawaka na redioni ilikuwa inasikika ZBC radio ikiunguruma kwa mbaali, kituo cha radio ambacho mimi na Kishoka hupenda kukisikiliza kila wakati. Hata kama tv iwe imewashwa, midundo ya ZBC radio ilikuwa ikisikika kwa chini chini.
            Ndivyo ilivyokuwa hapo sebuleni kwa wakati huo, lakini aliyekuwa akisikiliza radio wala kuangalia tv sikumuona. Nilijaribu kumwita Kishoka lakini hakuniitikia, nikaamua kwenda mpaka kwenye chumba chake kumwangalia, niliukuta mlango umefungwa, nikajaribu kugonga lakini sikujibiwa.
            Nilijaribu kuusukuma mlango nao ukafunguka, nikaangalia chumbani humo lakini sikuona mtu, nikaamua kurudi tena sebuleni nikidhani nitakuta mabadiliko, nilipofika nilikuta hali ni ileile kama ya awali, hapakuwa na Kishoka wala mgeni.
            Nilipata wazo la kumpigia simu Kishoka ili nimuulize alipo, nilipopiga simu  ilianza kuita mpaka ikakata. Mlio wa kupokelea wa simu hiyo ulisikika ukiita kwenye chumba changu. Nikabaki nikijiuliza kuwa Kishoka kaenda kufanya nini chumbani kwangu, vilevile kwa nini sasa alikuwa hapokei simu? Nilijiuliza kimoyomoyo baada ya simu kuita bila kupokelewa.
Niliamua kwenda mpaka chumbani kwangu kuona alichokuwa anakifanya Kishoka kiasi kwamba mpaka anaichunia simu yangu. Nilianza kuhisi kuwa huenda alikuwa anafanya kamchezo kachafu na mgeni wangu kwani naye kwa mambo hayo alikuwa hajambo, alikuwa havumi tu lakini yumo. 
Lakini bado kuna kitu kilikuwa kinanichanganya, katika kumbukumbu zangu wakati natoka mlango ulikuwa umefungwa na funguo nilikuwa nazo, hiyo simu ya Kishoka ilifikafikaje chumbani kwangu? Kishoka mwenyewe alikuwa kaingiaje huko chumbani wakati funguo nilikuwa nimeondoka nazo? Au asubuhi nilisahau kuufunga mlango? Nilibaki na maswali ambayo majibu yake yangepatikana baada ya kumhoji Kishoka.
Shauku ya kutaka kujua alichokuwa anakifanya Kishoka humo chumbani kwangu ilinikaa rohoni. Nilikuwa nikiwaza mambo mia kidogo kabla ya kufika mlangoni;
‘huyu Kishoka yuko peke yake au yupo na  huyo mgeni, maana mpaka naingia ndani sijakutana naye wakati mara ya mwisho kuongea naye kwenye simu nilikuwa nimekaribia getini kwangu. Angekuwa ni mtokaji basi ningekutana naye walau karibu na geti kama siyo mlangoni.’
Nilipofika mlangoni nilibaini kuwa mlango ulikuwa haujafungwa bali ulikuwa umerudishiwa tu. Nilizidi kujiuliza kuwa umefunguliwaje wakati kipindi naondoka funguo niliondoka nazo? Nilizidi kuduwaa.
Mara nilikumbuka kuwa wakati natoka mlango sikuufunga mimi bali aliufunga Kishoka.
‘Kama alikuwa amesahau kuufunga au alikuwa ameuacha kwa makusudi basi atakuwa kaingia kiulaini, lakini kaingia kufanya nini chumbani kwangu? Bila shaka Kishoka anafanya matusi na mgeni wangu chumbani kwangu.’ Mawazo yangu yalianza kunituma vile kwa wakati huo.
Ndipo nilipouona mwanga wa taa ikiwaka chumbani, nikazidi kujawa na ghadhabu.
‘Wamewasha hadi taa utadhani ni chumbani kwao, hizi sasa ni dharau. Kwa nini asimpeleke chumbani kwake?’ Nilizidi kujisemea kimoyomoyo.

JE, KISHOKA ANAFANYA NINI CHUMBANI KWA BRIGHTON? NA MGENI BADO YUPO HUMO NDANI AU VIPI? USIKOSE SEHEMU YA 14.

No comments:

Post a Comment