Thursday, September 26, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu 22



ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA....
Baada ya mahabusu wengine kumaliza kusomewa mashtaka yao tulirudishwa rumande ya magereza huku gari tulilokuwa tumepakizwa likikimbia kwa kasi.
SASA ENDELEA.......
            Tukiwa njiani moyo wangu ulizidi kuumia kwa kupotezewa muda kwa kesi ambayo sijashiriki wala kuifanya. Akili yangu yote ilikuwa kwenye hatima ya hiyo kesi. Mpaka tunafika kwenye ngome ya gereza nilikuwa nimezama kwenye mawazo mazito. Nilighutushwa na sauti ya mlango wa karandinga ulipokuwa ukifunguliwa ili tushuke. Tulishuka na kuswekwa kwenye gheto la watuhumiwa kuendelea na msoto.
            Wiki mbili zilikatika nikiwa rumande, niliziona ni nyingi sana. Hali yangu kiafya ilizidi kuwa mgogoro kila siku iliyoenda kwa Mungu. Kudhoofu huko hakukutokana na ugonjwa bali mawazo, aiseeeh! Acha kabisa kitu mawazo, tena mawazo ya kesi ya mauaji ambayo hukushiriki hata kuitenda. Kila wakati nilijikuta nikichoka kabisa.
            Wakili wangu alinitembelea tena siku moja kabla ya siku ya kwenda mahakamani. Tuliongea mawili matatu huku akinipa moyo kwa kuniambia nitashinda tu na haki itatendeka kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu.
            “Halafu mbona umekonda sana?” Lilikuwa ni swali la Jonas Mlyanyama baada ya kuongea mambo yetu muhimu yaliyokuwa yanahusiana na hiyo kesi yangu.
“Mawazo kaka, unajua kesi hii inanipa wakati mgumu sana katika kichwa changu.” Nami nilimjibu.
“Acha kuwaza sana ndugu yangu, kwanza hii kesi mimi hainipi presha hata kidogo. Hapo tutashinda tu.” Alisikika wakili Jonas akiniambia.
            Maneno yake hayo niliyaona kama ya kunifariji tu ili niache kuwaza, lakini hatari iliyokuwa mbele yangu ilikuwa kubwa mno. Piga ua kifo cha kunyongwa kilikuwa kinaninyemelea. Suala la kuokoka lilikuwa adimu kama kaburi la baniani.
            “Najaribu kujikaza lakini najikuta nikiwaza tu, kila nikikaa mawazo yananijia, hata usingizi nashindwa kupata, chakula nacho hakipandi hata kama kwa kukilazimisha.”
“Usijali ndugu yangu, amini nakwambia Mungu yupo na atakusaidia.” Ilikuwa ni sentensi ya mwisho kutoka kinywani kwa wakili Jonas Mlyanyama.
            Bila ya muda kupotea tayari nilikuwa mbele ya askari aliyekuwa akilalama kuwa tumetumia muda mwingi kwa kupiga soga kama tumekutana sokoni.
            Alinipeleka moja kwa moja kwenye ‘gheto’ la watuhumiwa lililokuwepo gerezani hapo. Nikawakuta mahabusu wenzangu ambao tulikuwa tumeshaanza kuzoeana.
Tuliendelea kupiga stori za hapa na pale. Hata hivyo mimi mawazo yangu yote hayakuwa pale hata kidogo. Nilikuwa nikiwaza mambo lukuki kwa awamu, mara namuwaza Kishoka, mara nawaza kesi yangu itakavyokuwa.
Wakati mwingine taswira ya msichana aliyenisababishia matatizo hayo ilinijia kichwani mwangu; msichana ambaye mimi ndiyo nilikuwa nikiamini kwa asilimia mia tano kuwa ndiye alihusika na kifo cha Kishoka.
            Hali ya rumande ndugu yangu wee acha tu. Hata kama kungekuwa na masofa pamoja na runinga mimi nisingeweza kuyafurahia kwani uhuru hamna.
            Ilipofika mida ya jioni vijana wawili waliletwa kwenye ‘sello’ tuliyokuwemo. Mahabusu mmoja akaninong’oneza kuwa vijana hao walikuwa wameifanya rumande kuwa ni maskani yao.
            Kukatisha mwezi hawajaswekwa humo ilikuwa ni vigumu kwao. Kila waliporudi uraiani baada ya kumaliza kutumikia adhabu za vifungo walizokuwa wakipewa, vijana hao walifanya makosa tena na kurudishwa rumande.
            Niliwashangaa sana baada ya kuambiwa kuwa walikuwa na kasumba hiyo. Sehemu mbaya kama ile wao walikuwa wakiifurahia! Ama kweli kila shetani na mbuyu wake. Nilipojaribu kuuliza kipi hasa ambacho huwafanya waione rumande kama maskani niliambiwa kuwa ni ugumu wa maisha.
            Kumbe huo ndiyo ulikuwa ni mfumo wao wa maisha, si unajua tena huko kula ni bure na kulala ni bure! Kwao siku zilisonga kwa mtindo ule.
            Hata hivyo mimi niliona ni ujinga na umbumbumbu uliokuwa ukiwasumbua. Mbona kuna shughuli kibao huko uraiani ambazo wangefanya zingewapatia riziki ya halali.
            Vijana hao niliwafananisha na mazuzu ambao mishipa ya fikra ilishakatika kichwani mwao. Rumande siyo sehemu ya kukimbilia kama una akili yako timamu.

                                    *************************
ITAENDELEA........

No comments:

Post a Comment