Saturday, September 7, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 7



ILIPOISHIA........
Nilipigwa na bumbuwazi baada ya kufumbua macho kwani sikumuona Anna wala lile kundi la wale kina mzee Mboma. Nilishangaa kujiona nipo kitandani kwangu kwenye chumba changu. Kumbe ilikuwa ni ndoto tu.
                                                     ******************

SASA ENDELEA.......
              Nilikukuruka huku nikihema. Kumbe nilikuwa nimepiga yowe kwa nguvu kabla ya kughutuka, yowe hilo nililolitoa bila kujijua lilimfanya mpangaji wangu atoke chumbani kwake na kuja kwenye mlango wa chumba changu kufahamu kulikoni. Nikiwa bado nahema nilisikia mlango ukigongwa, nilijikaza na kuuliza ni nani aliyekuwa anagonga.
Sauti ya Kishoka ilisikika ikinijibu, taratibu niliinuka kwenda kufungua mlango baada ya kung’amua kuwa mgongaji wa mlango ni mpangaji wangu.
            Baada ya kumfungulia aliniuliza,
“kulikoni kaka, mbona umepiga yowe kwa nguvu sana, ni nini kimekusibu?”
“Kaka mimi nilikuwa nimelala, wakati nimelala nikaota ndoto lakini siikumbuki!” Hilo ndilo lilikuwa jibu langu kwa swali la Kishoka.
“Basi utakuwa umeta ndoto ya kutisha sana maana makelele uliyokuwa unapiga yalikuwa siyo ya kawaida.” Aliniambia kwa sauti iliyojaa kila aina ya upole.
            “Ndoto niliyoota ni ya kutisha lakini sikumbuki jinsi ilivyokuwa, isitoshe huwa sina kawaida ya kuota mchana.” Nilimalizia kwa kushusha pumzi huku akili yangu ikijaribu kurudisha kumbukumbu nyuma.
            Kumbukumbu zilianza kunijia kwa mbaali sana, zikawa zinakuja na kuondoka utadhani ‘network’ ya simu zilizochakachuliwa, simu zinazouzwa na matapeli chini ya mnara. Katika kukumbuka nilianza kukumbuka kuwa nimemuona marehemu Anna ndotoni.
            Akili yangu sasa ikawa ‘busy’ zaidi ya ‘customer care’ wa mtandao wa simu wenye wateja lukuki wanavyokuwaga. Nilizidi kuvuta kumbukumbu juu ya ndoto niliyoota, ndoto ya kutisha ambayo nilikuwa nimeiota muda mfupi uliopita nilipokuwa nimelala, ndoto ya mchana.
            Mara nikaikumbuka yote, nikaanza kumsimulia Kishoka ndoto hiyo ilivyokuwa, nilimsimulia mwanzo mpaka mwisho.
Nikamsimulia jinsi ndoto yangu ilivyokuwa imetawaliwa na watu waloikufa kitambo, tena vifo vyao ni vya kujiua kila mmoja. Kipenzi changu Anna, Kaka James, mzee Mboma, Patrick pamoja na watu wengine lukuki ambao sikuweza kuwatambua niliwashuhudia kwenye hiyo ndoto .
            Kishoka akaniambia kuwa hiyo ni ndoto tu kama zilivyo ndoto zingine. Alianza kwa kunifafanulia tafsiri ya neno ndoto; akaniambia ndoto kwa jina jingine huitwa njozi ama ruya.
Aliendelea kuniambia kuwa ndoto ni mkusanyiko wa mawazo makuu yaliyokuwa yametawala katika kichwa cha muotaji kipindi hajalala ama siku za nyuma. Akili inapokuwa imepumzika wakati mtu yupo usingizini kichwa huweza kukumbuka matukio hayo na kuyaundia picha ambayo huwa kama tukio halisi.
            Maelezo ya Kishoka hayakuniingia akilini kabisa, nikamkubalia tu ili turudi kwenye pointi yetu ya msingi, yaani fasiri ya ndoto niliyokuwa nimeota. Nilimuuliza ndoto hiyo ina maana gani?
            Hata hivyo alinijibu kuwa yeye siyo bwana njozi, lakini alivyokuwa anahisi ni kwamba akili yangu itakuwa imetawaliwa sana na kuwawaza watu wawili, watu ambao hata kwenye ndoto hiyo nilikuwa nimewaota, yaani marehemu kaka James pamoja na mpenzi wangu wa zamani marehemu Anna.
            Kuondokewa na watu hawa katika maisha yangu kulikuwa kumeniathiri sana kisaikolojia na ndiyo maana nikawaota. Hivi ndivyo Kishoka alivyoning’amua.
            Nilimuuliza kuhusu mzee Mboma, Patrick na wengineo ambao sikuwatambua; sikuwa na mawazo sana juu yao, wengine nilikuwa sijawahi hata kuwaona. Sasa kwa nini nao waonekane kwenye ndoto yangu? Kweli sikatai kuwa kifo cha mpenzi wangu na kaka yangu kilikuwa kimeniathiri sana kisaikolojia, lakini siyo hao wengine, sasa kwa nini nao niwaone?
            Jibu alilonijibu Kishoka ni kwamba hakuna mechi isiyokuwa na washangiliaji, pia akaongezea kuwa hakuna ‘muvi’ inayochezwa na kinara peke yake, lazima pawepo na wahusika waalikwa. Hivyo wahusika wakuu wa ndoto yangu walikuwa ni Anna na James, wengine wote walikuwa wahusika wadogowadogo. Mpaka hapo nilikuwa nimemuelewa kwa kiasi fulani.
            Aliniacha na kwenda zake, nikiwa bado nipo kwenye kitanda changu cha sita kwa sita, niliendelea kuitafakari ndoto ambayo nilikuwa nimeiota muda mfupi uliopita. Maneno ya Anna yenye ujumbe mzito yalizidi kujirudia kichwani mwangu.
JE, NINI KTATOKEA BAADA YA HAPO? ITAENDELEA.......

No comments:

Post a Comment