Friday, September 20, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 18



ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA......
Afande huyo nilimuona akifunga faili lake na kuniambia nijiandae kwenda kuozea jela. Alichodai ni kwamba laiti kama ningeeleza ukweli basi angeweza kunisaidia.
                                        ************************
SASA ENDELEA.......
            Nikiwa rumande machozi yalizidi kunitiririka bila kukauka utadhani chemichemi za mto Naili, chemichemi ambazo hutiririka bila kukauka misimu yote; iwe masika ama kiangazi. Mifereji ya machozi ilikuwa inatiririka kutoka machoni ikipitia mashavuni mpaka kwenye kidevu.
            Harufu mbaya ya humo kwenye ‘gheto’ la watuhumiwa ilinifanya nipige chafya mara kwa mara. Nilijaribu kujikaza kiume nijizuie kulia lakini cha ajabu machozi  yalizidi kunitoka. Nilikuwa sijawahi kuswekwa rumande hata siku moja tangu kuumbwa kwa misingi ya dunia.
            Siku niliiona kama haiendi, masaa nayo yalikuwa kama yamesimama. Tangu saa tano za asubuhi baada ya kuruhusiwa hospitali niliingia humo,  mpaka muda huu ambao nilikuwa nauhisi ni kama saa tisa za jioni nilikuwa nimeiva sawasawa. Kwa muda mchache huu ambao nilikuwa nimekaa ndani nilikuwa  najiona kama nimekaa mwezi mzima.
            Mawazo kibao yalikuwa yametawala kichwa changu; niliwaza biashara zangu zitasimamiwa na nani, zaidi ya yote kilichokuwa kinaniumiza kichwa ni hatima ya kesi yangu iliyokuwa inanikabili, kesi ya mauaji.
            Ilipofika usiku nilizidi kuipata freshi, tena ni freshi ya mwaka. Sulubu iliyokuwemo kwenye ‘gheto’ la watuhumiwa haielezeki, yaani ni sulubu ya kufa mtu. Hapo ndiyo nilianza kuamini kuwa kweli rumande siyo kanisani ama msikitini.             
            Mbu walinishambulia si mchezo, nilijaribu kuwaua mmoja baada ya mwingine lakini wakawa hawaishi wala kupungua, suala la kupata usingizi walau dakika moja lilikuwa ni ndoto; tena ndoto yenyewe ni ndoto ya kuota mchana kweupe.
            Siyo mbu peke yao walionipa kero usiku huo, kunguni na viroboto nao walizidi kuleta adha katika mwili wangu.
‘Kama rumande ya polisi tu hali ndiyo hii, kule gerezani sasa hali ikowaje?’ Nilizidi kutafakari huku nikiwa ‘buzy’ kupambana na wadudu hao wasiyokuwa na chembe ya adabu hata kidogo.
            Niliwatumbua kwa hasira kila nilipowabahatisha wakigema damu yangu, lakini nao ndiyo kwanza walizidi kuongezeka utadhani walikuwa wakialikana.
‘Kwa mtindo kama huu kufikia asubuhi nitakuwa nimepoteza lita kadhaa za damu katika mwili wangu. Lakini chanzo cha mateso haya yote ni yule msichana  aliyemuua mpangaji wangu Kishoka.’ Niliendelea kunung’unika peke yangu. Manung’uniko ambayo hayakuzaa matunda ya wokovu wa kesi yangu hata kidogo.
            Hayawi hayawi mwisho yakawa, jogoo la kwanza nililisikia likiruka ‘bonanza’ kuashiria alfajiri inawadia. Mara nilisikia jogoo la pili na hatimaye la tatu. Kulionekana kupambazuka huku nikiumaliza usiku kwa kuutoboa, yaani namaanisha sikusinzia hata sekunde moja zaidi ya kupepesa macho pale ilipobidi.
            Ikawa asubuhi, siku ambayo sikujua itaishaje. Nilitegemea kupandishwa kizimbani kwa mara ya kwanza ili kusomewa shauri lililokuwa linanikabiri. Lakini mambo yakawa sivyo.
Mara mlango ulipofunguliwa niliwaona askari wawili waliokuwa wameshikilia bunduki kila mmoja wamesimama mlangoni kisha wakanitaka nitoke. Nilipotoka walinifunga pingu mikononi kisha wakanitanguliza mbele mpaka kwenye chumba kimoja katika kituo hicho kisha mahojiano yakaanza upya.
ITAENDELEA.....

No comments:

Post a Comment