Monday, September 16, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 15



ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA......
Pumzi zilianza kuniishia, nikajikuta nikipumua kwa shida huku kifua changu kikianza kubana. Sijakaa sawa nikaanza kuhisi kama kizunguzungu na kuhisi kama nataka kuanguka. Mpaka hapo nilipoteza ‘network’ na kujikuta sijitambui hata kidogo.
                                    **********************   

SASA ENDELEA.......
Fahamu zilinijia kama mtu aamkapo kutoka usingizini. Kitanda nilichokuwa nimelalia si kile nilichokizoea, kitanda chenye godoro la Dodoma ambacho ni futi sita kwa sita.
Kitanda nilichokuwa nimekilalia kwa wakati huo kilikuwa ni tatu kwa sita,  
‘piga ua hiki siyo kitanda changu.’ Nilijikuta nashikilia msimamo huo.
            Huku nikipepesa macho niligundua kitu kingine, humo ndani kulikuwa na vitanda lukuki vilivyokuwa vinafanana. Harufu ya dawa nilianza kuisikia, hapo ndipo nilipong’amua ya kuwa nipo hospitali.
            Huku nikipiga miayo, nilitaka kupeleka mkono wangu wa kuume usoni kujaribu kupangusa tongotongo endapo zipo, mkono uligoma kwenda. Nikaanza kujiuliza ni kwa nini mkono wangu unang’ang’ania kwenye chuma cha kitanda?
            Kabla sijaangalia kilichokuwa kinakwamisha mkono wangu wa kulia kunyanyuka, nilitaka kutumia mkono wangu wa pili kusafisha macho yangu, nao ulikuwa mzito kiaina.
Huku maruweruwe yakififia kwenye mboni za macho yangu, niliinua kidogo kichwa changu kuangalia kilichokuwa kinaufanya mkono wangu wa kushoto uwe mzito kunyanyuka. Ndipo nilipojionea sindano kubwa ikiwa imeunganishwa na mrija wa plastiki ambao unaelekea kwenye nguzo ya chuma iliyokuwepo karibu na kitanda nilichokuwa nimelazwa.
            Nilipoufuatilia mrija huo mpaka ulipoishia nilijionea drip ya maji imetundikwa, huku maji hayo yakitoja taratibu na kuingia kwenye mrija huo kisha kuteremka mpaka kwenye mkono wangu.
            ‘Nimetundikiwa drip ya maji, ni nini kimenisibu mpaka nikafikishwa hapa?’ Nilibaki nikijiuliza bila kupata majibu ya swali langu hilo.
            Wazo la kuangalia kilichokuwa kinaufanya mkono wangu wa kulia ung’ang’nie huko kwenye chuma cha kitanda lilinijia, nikageuza shingo yangu kiasi kwamba mpaka nikaweza kuona kwenye chuma cha kitanda nilichokuwa nimelalia. Moyo uliruka baada ya kukiona kilichokuwa kimeufanya mkono wangu ugande  kwenye chuma hicho.
            ‘Nimefungwa pingu! Ni kosa gani nililofanya mimi mpaka nikafikia hatua ya kulazwa hospitali huku nikiwa nimefungwa pingu. Mimi siyo jambazi na wala huwa sina fikra za kuja kuwa, sasa iweje leo nifungwe pingu mithili ya jambazi aliyeshindikana kisha akakamatwa kwa bahati mbaya?’ Fukuto la maswali mengi lilizidi kukisumbua kichwa changu na akili yangu kwa ujumla.
            Katika kuangaza angaza niliwaona askari wawili waliokuwa wamekaa karibu yangu huku mmoja akiwa ameshikilia mtutu.
 ‘Ama kweli huu ‘msala’ si wa kitoto, nimewekwa chini ya ulizi kwa silaha za moto, hivi nimefanya kitu gani mimi?’ Nilijaribu kuwaza na kuwazua ili nifahamu kilichokuwa kimenisibu lakini ikawa ‘holla’.
            Nilijikakamua na kuamua kuwauliza hao hao waliokuwa wameniweka chini ya ulizi.
“Samahani afande, hivi ni tukio gani nililofanya mpaka mmeniwekwa chini ya ulinzi ndani ya hospitali?” Nililibwaga swali hilo kwa maafande hao ambao sura zao zilikuwa zimekunja ndita si mchezo.
            “Unajifanya hujui urichokitenda? Acha kuuriza maswari yasiyokuwa na tumbo wara mgongo mura.” Alisikika askari ambaye alikuwa kashikilia cha moto huku rafudhi yake ikinidhihirishia waziwazi kuwa ni mtu wa Mara, yaani mkurya. Tena alinijibu kwa sauti ya ukali utadhani kanishika ugoni kwa mkewe.
Niliamua kujinyamazia kwa kuhofia kupewa mikong’oto na maafande hao walioonekana kupinda kuzidi maelezo. Alama za mia moja kumi na moja zilizokuwa zimejichora kwenye mapaji ya nyuso zao kwa kukunja ndita zilikuwa zinanitisha.
NINI KITAENDELEA! SEHEMU YA 16 SI YA KUKOSA!

No comments:

Post a Comment