Friday, September 6, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 6



ILIPOISHIA........
‘Ama kweli leo ndiyo leo, ngoja nisubiri hatima yake.’ Niliwaza kimoyomoyo huku mdomo ukiendelea kuwa wazi, kamasi pamoja na machozi vilianza kunitoka hata sikuwa na muda wa kuviondoa badala yake nilizidi kuviachia vitiririke mpaka basi.

SASA ENDELEA.......
Mrembo Anna, niliyezoea kumuita ‘queen’; msichana aliyekuwa amefanikiwa kuuteka moyo wangu kwa kiasi kikubwa, siku hiyo alikuwepo mbele yangu. Msichana niliyemuamini kiasi kwamba niliapa kumzika endapo asingenizika. Tena aliniahidi kunitunzia zawadi adimu, zawadi ambayo wasichana wengi wa siku hizi wamepungukiwa, zawadi ya usichana wake ama bikira yake. Hakika nilikuwa naingojea kwa hamu kubwa.
Zawadi hiyo alikuja kuipoteza pasipo yeye kutaka; siku ambayo alimsindikiza dada yake kwenye ‘birthday’ ya mpenzi wake. Walipofika huko mambo yalikuwa ndivyo sivyo; alitokea kijana mmoja ambaye alimtaka kimapenzi.
Anna hakuwa tayari kwa vile alikuwa akinipenda na kunithamini pia. Hakutaka kabisa kunisaliti wala kumzawadia kidume mwingine yeyote tunu adimu kama ile. Kikombe kile kilikuwa ni halali yangu kukivunja.
Kwa kuwa mazingira yenyewe yalikuwa hatarishi, msimamo wa Anna haukuzaa matunda yoyote. Kijana huyo aliamua kutumia ubabe baada ya sera zake kugonga mwamba, na kweli alifanikisha. Aliamua kumbaka Anna, kitendo ambacho kiliyavunja maagano yetu.
Baada ya Anna kunieleza habari hizo, habari ambazo zilileta msiba mkubwa ndani ya moyo wangu, nilimuomba anipe muda wa wiki mbili kabla ya kutoa uamuzi wangu juu ya hiyo hujuma ya tunu yangu. Vilevile nilitoa shinikizo la kwenda kupima virusi vya ukimwi baada ya miezi mitatu.
Wakati tukisubiria miezi mitatu ikamilike ili tuende kupima VVU, nilipokea taarifa za kifo cha mpenzi Anna, taarifa ambazo zilionekana kuuchoma moyo wangu mkuki wenye sumu kali.
Anna alipoteza uhai wake baada ya majaribio ya kuitoa mimba aliyoipata siku aliyobakwa. Kabla mauti hayajamfika aliandika ujumbe uliosisitiza kuwa ataendelea  kunipenda hata huko aendako.
Anna sasa alikuwa yupo mbele yangu, nilitaka kumnyoshea mikono nimuite japo kwa ishara. Hata hivyo nilishindwa kutokana na kukosa nguvu katika mikono yangu.
‘Sasa Anna atajuaje kuwa nipo karibu yake, tena nimemuona!’ Nilizidi kuchanganyikiwa huku nikiwaza vile.
Bila kutegemea nilimuona akinisogelea, moyo wangu ulianza kufarijika kidogo kidogo. Nikaanza kujipa matumaini ya kwamba huenda nitapata kuongea na Anna wangu.
Nilimsubiria kwa shauku kubwa. Alinisogelea hadi akanikaribia, sasa alikuwa yupo umbali wa kama mita tatu hivi kutoka nilipokuwa. Alizidi kutoa kilio cha kuomboleza, nikaanza kumuonea huruma mpenzi wangu wa tangu zamani, tulikuwa tukipendana ila kifo ndicho kilichotutenganisha.          
Alifungua kinywa chake na kuanza kunena,
 “mpenzi wangu Brighton, najua nilikukosea sana, na siyo wewe peke yako bali hata jamii kwa ujumla. Huko tuliko tunateseka sana, tena mimi nateseka mara mbili ya wenzangu. Kawaambie binadamu huko duniani kuwa kuua ni dhambi kubwa mno, adhabu yake ni kali kupita maelezo.” Aliongea kwa masikitiko makubwa huku akionekana ni jinsi gani alivyokuwa anaugua moyoni.
Nilitaka kumuuliza swali, tatizo nilikuwa bado siwezi kuongea. Nilibaki nimemwangalia bila ya kupepesa macho. Aliendelea kunihubiria,
“adhabu yangu imekuwa tofauti na za wengine kwa sababu niliua mara mbili, nilikiua kiumbe kilichokuwamo tumboni mwangu kisha na mimi nikajiua. Japokuwa uhai niliupoteza baada ya kupoteza damu nyingi nilipotoa mimba, kitendo hicho kilinifanya nihesabike kuwa nilijiua; kosa ambalo ni la kuua.
Usijaribu kabisa kuua wala kujiua. Yeyote afanyaye hivyo makazi yake ni hii sehemu tuliyopo. Brighton; kazidi kutenda mema duniani ili siku zako zitakapoisha ukapumzike kwa amani na siyo kwa mateso kama tunavyopumzika sisi.”
Ghafla mwanga kama wa radi ulitokea alipokuwa amesimama Anna. Ukali wa mwanga huo ulinifanya nifumbe macho. Nilipigwa na bumbuwazi baada ya kufumbua macho kwani sikumuona Anna wala lile kundi la wale kina mzee Mboma. Nilishangaa kujiona nipo kitandani kwangu kwenye chumba changu. Kumbe ilikuwa ni ndoto tu.
                                      ******************
ITAENDELEA.......

No comments:

Post a Comment