Wednesday, September 18, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 17




ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA......
“Afande, kama vipi richukue maerezo maana tayari rimeshazinduka.” Alisikika afande aliyekuwa ameshikilia bunduki akimwambia mwenzake ambaye alikuwa kashika faili mkononi.
“Hamna tabu afande, hata mimi nilikuwa ninalifikiria hilo kichwani mwangu.” Alijibu afande huyo.
SASA ENDELEA.......
            Mara nilimuona afande huyo aliyekuwa kashikilia faili mkononi akivuta kiti chake na kusogea karibu kabisa na pale nilipokuwa nimelaza kichwa changu. Alifungua faili lake huku akiwa kashikilia kalamu mkononi.
            Alianza kunihoji maswali kuhusiana na tukio zima la mauaji ya Kishoka, kila aliponiuliza nilimjibu, kila nilipomjibu aliandika kwenye karatasi iliyopo kwenye faili lake.
“Mnaishi wangapi katika hiyo nyumba?” lilikuwa ni baadhi tu ya maswali niliyokumbana nayo kutoka kwa kachero huyo. Swali hilo nililijibu kwa kusema kuwa tunaishi wawili tu katika hiyo nyumba, yaani mimi na Kishoka.
Mara aliniuliza uhusiano wangu na Kishoka, nami nilimjibu kuwa Kishoka ni mpangaji wangu katika nyumba yangu niliyorithi kutoka kwa marehemu kaka yangu, kaka James ambaye alikufa kifo cha kujiua mwenyewe kwa kujifyatulia risasi kichwani baada ya kumuua aliyekuwa mpenzi wake pamoja na jamaa aliyemfuma akilamba asali ya mapenzi kwa mpenzi wake huyo..
            “Sasa kwa nini umeamua kumuua Kishoka?” Askari huyo alinifyatulia swali jingine. Nami nilimjibu bila kusita wala kujing’atang’ata kwamba mimi sijaua.
“Kama wewe hujaua, ni nani aliyemchinja Kishoka ilhali mnaishi wawili tu katika hiyo nyumba?”
            Nilijitahidi kuwa makini sana katika maelezo yangu ili nisijikanganyekanganye halafu nikaonekana nimeua kweli. Niliamua kumtaja muuaji, nikasema kuwa ni msichana fulani ambaye alianza kunifanyia vioja tangu juzi nilipokutana naye ufukweni. Nilieleza jinsi mambo yalivyokuwa kati yangu na mwanadada huyo kule ufukweni.
            Nilipoulizwa jina lake na mahali alipokuwa anaishi niliishia kusema sina nijualo juu yake. Nilijaribu kurudia tena kutoa maelezo jinsi nilivyokutana na msichana huyo, sikuwa namfahamu hata kidogo, lakini yeye alidai kuwa ananifahamu na kwa kunithibitishia hilo alinitajia hadi jina langu. Hakuishia hapo tu, aliongeza kuwa mpaka kwangu alikuwa anapajua hivyo akaniahidi atanitembelea kesho yake asubuhi.
            “Ilipofika kesho yake asubuhi kweli alikuja?” Aliendelea kuhoji askari huyo huku akionekana kunisikiliza kwa makini sana.
“Ndiyo alikuja lakini vilikuwa ni vioja vitupu!”
“Uliweza kuonana naye na mkaongea nini?” Aliniuliza afande nami nikaanza kumdadavulia vile ilivyojitokeza tangu msichana huyo anafika pale getini, akakaribishwa na Kishoka lakini akakataa kuingia ndani.
            Niliendelea kueleza jinsi msichana huyo alivyopotea kimazingara tusimuone alikoelekea. Nilizidi kuweka wazi kila kilichojitokeza mpaka wakati nilipokikuta kichwa cha Kishoka kikiwa kimetenganishwa na kiwiliwili chake. Nilimalizia kwa kusema kuwa muuaji si mimi bali ni huyo msichana ambaye kwa vyovyote vile si binadamu wa kawaida.
            Askari huyo aliyakataa katukatu maelezo yangu na kuniambia kuwa mimi ni muongo na hayo maelezo yangu hayawezi yakanifikisha kokote, akasema jeshi la polisi haliamini ushirikina wala mazingazi. Akanitaka nieleze ukweli ili aone ni jinsi gani ataweza kunisaidia. Nilimwambia ukweli wangu ndiyo huo na sikuwa na maelezo mengine zaidi ya hayo.
            Afande huyo nilimuona akifunga faili lake na kuniambia nijiandae kwenda kuozea jela. Alichodai ni kwamba laiti kama ningeeleza ukweli basi angeweza kunisaidia.
                                   
                                        ************************
NINI HATIMA YA BRIGHTON? USIKOSE KUFUATILIA MWENDELEZO WA HADITHI HII TAMU NA YENYE KUSISIMUA!

No comments:

Post a Comment