Friday, October 18, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 32




ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA....
Baada ya kumwambia hivyo jaji aliutaka upande wa mashtaka kuandaa maelezo ya mashtaka kuonyesha ni kwanini unamuona mshtakiwa anahatia kwa mujbu wa ushahidi uliotolewa. Shauri hilo liliahirishwa tena kwa mwezi mmoja.

                        *************************
SASA ENDELEA.......
Siku zilipita. Tarehe ya kesi iliwadia. Siku hiyo ilikuwa ni siku ambayo upande wa mashtaka ulitakiwa kutoa maelezo ya uchambuzi wa kisheria ya kueleza ni kwa jinsi gani inaniona mshtakiwa nina hatia kwa mujibu wa ushahidi uliotolewa.
Tayari nilikuwa nimeshapandishwa kizimbani. Ndipo nilipomuona mwendesha mashtaka amesimama kisha akaanza kutoa maelezo mbele ya mahakama ya kuwa upande wa mashtaka umeleta mashahidi walioweza kuthibitisha ya kwamba nilikuwa nimetenda kosa la kumuua Kishoka Mpoto kwa kukusudia, kitendo ambacho ni kinyume cha sheria.
Akaendelea kueleza kwamba ushahidi uliotolewa umeonyesha dhahiri kuwa nilimchinja Kishoka kwa mikono yangu nikitumia kisu kilichokutwa karibu na mlango kama ushahidi ulivyokuwa umeeleza.
Akaendelea kusema kuwa licha ya mshtakiwa kudai kuwa aliyetoa taarifa za awali hakutaka kujitokeza kituoni mara baada ya kutoa taarifa hizo, shahidi huyo ambaye alikuwa ni mwanadada huenda aliogopa kwenda kituo cha polisi kutokana na kuchanganyikiwa baada ya kushuhudia ndugu yake akiuawa kikatili ama kutokana na desturi iliyojengeka miongoni mwa waafrika wengi ya kukiogopa kituo cha polisi hata kama hawana hatia.
“Hata hivyo shahidi huyo alifanya jambo kubwa na la maana kwa kutoa taarifa kituo cha polisi.” Alizidi kueleza mwendesha mashtaka huyo ambaye ni bwana Charles Ngonyani.
Halikadhalika kuhusu madai yangu ya kudai kuwa msichana huyo alikuwa ni mshirikina au jini, mwendesha mashtaka huyo alisema kwamba hayo yalikuwa ni madai yasiyokuwa ya msingi na mantiki hivyo shahidi huyo alikuwa na haki ya kunifungulia kesi nyingine kwa kumzushia ya kwamba ni mchawi na ni jini. Pia aliongeza kwa kusema kuwa mahakama huwa haiamini imani potofu za kichawi kama mimi nilivyokuwa nikidai.
Hata kuhusu wakili wangu mwendesha mashtaka alidai kuwa wakili huyo alijaribu kufanya usanii mbele ya mahakama kwa kujifanya kashindwa kuongea  kutokana na uchawi aliokuwa akisingiziwa Sharifa ili kujenga hoja yetu, lakini ukweli ni kwamba shahidi huyo alikuwa ameishiwa hoja za kisheria kutokana na ukweli uliokuwa umetolewa na mashahidi wa upande wa mashtaka.
Suala la wakili wangu kufariki dunia mwendesha mashtaka alisema kuwa hiyo ni mipango ya Mungu hivyo asisingiziwe Sharifa.
“Hivyo kulingana na mashahidi waliotoa ushahidi mbele ya mahakama hii tukufu, ni juu ya mahakama kumuona mshtakiwa ana hatia ya kuua kwa kukusudia na hivyo tunaitaka imuhukumu kifo kwa mujibu wa sheria.” Alimalizia mwendesha mashtaka na kuketi.
Niliumia sana kumsikia mwendesha mashtaka huyo akaniona mharifu na kuiomba mahakama inihukumu kifo wakati maskini wa Mungu nilikuwa sijatenda hiyo dhambi ya mauaji. Hata hivyo sikuweza kumlaumu sana kwa vile wajibu wa waendesha mashtaka ni kuwaona washtakiwa wana hatia hata kama hawajafanya makosa.
Baada ya mwendesha mashtaka kumaliza kutoa maelezo yake, jaji Aneth Mwalukwa alinitazama na kuniuliza,
“Na upande wako mshtakiwa unajibu nini?”
            Nilighutuka na kujikuta mapigo yangu ya moyo yakiongeza kasi. Hata hivyo sikuwa na lolote la kuongea bali nilisema kuwa upande wa mashtaka umeniona na hatia kwa vile mauzauza hayakuwatokea wao. Laiti kama yangewatokea hata mara moja basi wangeamini yote niliyoyasema.
            Pia niliongeza kwa kusema kuwa mimi sijabobea sana katika mambo ya sheria hivyo nisingeweza kutoa mapingamizi ya kishera juu ya maelezo ya upande wa mashtaka. Nilimalizia kwa kusema kuwa ni juu ya jaji kuyapima maelezo yangu na ya upande wa mashtaka.
            Wakati wote huo jaji alikuwa ‘busy’ kuandika maelezo niliyokuwa nikiyatoa. Baada ya kumaliza aliniambia kuwa ninawajika kujitetea kwa kosa lililokuwa linanikabili kwani ushahidi uliokuwa umetolewa ulikuwa unaonyesha ya kwamba nimetenda kosa.
            Nilianza kujitetea palepale. Niliiambia mahakama ya kuwa sikuwa na chuki na Kishoka wala hatukuwa katika mgogoro. Niliendelea kueleza kuwa tukio la kuuawa kwa kifo hicho lilinisikitisha sana kwani siku hiyo asubuhi niliagana naye na nikaenda katika mizunguko yangu.
            “Ndipo aliponipigia simu muda wa jioni akiniambia kuwa kuna mgeni wangu hapo nyumbani, mgeni mwenyewe alikuwa ni yule aliyekuwa anatusumbua toka asubuhi akiwa anagonga geti wakati mimi napata kifungua kinywa.”
              Nilizidi kueleza jinsi mgeni huyo ambaye kwa pale mahakamani nilikuja nikamjua jina lake kuwa ni Sharifa. Nilieleza jinsi nilivyopokea taarifa kutoka kwa Kishoka ya kuwa mgeni huyo alikuwa amekataa kuingia ndani na kunitaka niende hukohuko getini nikaonane naye.
            Niliendelea kuieleza mahakama kuwa baada ya kwenda hapo getini sikukuta mtu. Kwa kirefu kabisa nilieleza mauzauza yote aliyokuwa akinifanyia msichana huyo mpaka ile jioni niliporudi kwangu na kumkuta Kishoka kashauawa chumbani mwangu.
            “Mambo ya ushirikina yapo na yanatokea sana katika jamii zetu hivyo mahakama isinione kama naongea uongo.” Nilizidi kujitetea.
            Mwisho wa utetezi wangu niliitaka mahakama inione sina hatia na iniachie huru kisha nikafunga kinywa changu.
            Baada ya kutoa utetezi huo, jaji Aneth Mwalukwa ambaye alikuwa ni mwanamama alipanga siku ya hukumu yangu baada ya mwezi mmoja.
HAYA SASA, TAREHE YA HUKUMU YA BRIGHTON YATAJWA. JE, ITAKUWAJE? USIKOSE SEHEMU YA 32

No comments:

Post a Comment