Tuesday, October 15, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 29



ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA....
“Hebu tuonyeshe kama mtu huyo yumo humu ndani ya mahakama!”
“Ni yule pale kwenye kizimba.” Aliongea msichana huyo huku akinisonta.
SASA ENDELEA.......
Mwendesha mashtaka aliichukua kamera na kuipeleka kwa jaji kisha akasema amemaliza muongozo wake kwa shahidi.
            Akili yangu ilizidi kuchanganyikiwa. Ushahidi wa picha uliokuwa umetolewa na msichana huyo ulizidi kuivuruga akili yangu. Japokuwa nilikuwa bado sijaziona hizo picha lakini niliamini kabisa kuwa msichana huyo hawezi kupeleka kitu ambacho siyo cha kweli mbele ya mahakama.
“Lazima kweli kuna picha zangu kwenye kamera hiyo, lakini sasa hizo picha kazitoa wapi wakati mimi sikumuua Kishoka?” Niliwaza na kuwazua bila kupata jibu.
Wakati nikiwaza hivyo wakili wangu aliinuka na kuomba auone ushahidi wa vielelezo vya picha uliokuwa umetolewa na shahidi huyo. Alipoletewa kamera hiyo alibaini kuwa picha hizo zilikuwa ni zangu kweli.
Naye alizidi kuchanganyikiwa. Akaomba nionyeshwe na mimi kisha akaruhusiwa. Nilipoonyeshwa nilizidi kupigwa na butwaa baada ya kuona picha zikionyesha namchinja Kishoka. Sikuamini kwa macho yangu.
Zilikuwa ni picha kama saba hivi ambazo zilikuwa katika mapozi tofauti, yote yakiwa yanaonyesha nikiwa katika hekaheka ya kumchinja Kishoka kama kuku. Nilizidi kuchanganyikiwa.
Wakili wangu aliniangalia huku akiwa amenywea kisha akatikisa kichwa. Aliondoka na kwenda karibu kabisa na kizimba cha shahidi kisha akakaa mkao wa kuanza kumhoji maswali shahidi aliyekuwa kizimbani ambaye ni Sharifa.
Hata hivyo alishikwa na kigugumizi ghafla na kushindwa kabisa kuongea. Kila alipojaribu kuongea alijikuta akigugumia na kushindwa kuyatamka maneno waziwazi.
Hali hiyo ilileta taflani kubwa ndani ya mahakama hiyo. Kila mtu akaanza kushangaa ni kwa nini wakili huyo amekuwa namna ile. Hali hiyo ilimfanya jaji aiahirishe tena kesi na kuipangia singu nyingine.
Kwa upande wangu sikushangaa sana kuona vioja hivyo kwani nilikuwa najua fika kuwa mwanamke yule ambaye alikuwa amejitambulisha kwa jina la Sharifa alikuwa anatumia nguvu za giza.
Nilirudishwa mahabusu kama kawaida, rumande sasa ikawa ni makazi yangu ya siku nyingi. Mahabusu wengine walikuwa wananikuta na kuniacha kutokana na kesi zao kufikia muafaka, wengine walikuwa wanahukumiwa vifungo na wengine waliokuwa wakishinda waliachiwa huru.
Kwangu mimi ilikuwa kila siku danadana, limeisha hili linaingia lile. Ilifikia kipindi nikachoka kabisa na maisha ya huko rumande, nikawa natamani hata kujiua lakini niliyakumbuka maneno mazito ya marehemu Anna aliyoniambia nikiwa ndotoni ya kuwa adhabu ya mtu anayejiua ni babu kubwa.
Kabla siku ya kusikilizwa kesi yangu haijafika nililetewa taarifa kuwa wakili wangu kafariki dunia. Tangu alipotoka mahakamani siku ile hakuweza tena kuongea, hata kile kigugumizi alichokuwa akipapatua siku hiyo kilibadilika akawa haongei kabisa. alikuwa ni zaidi ya bubu.
Taarifa hizo ziliendelea kueleza kwamba zilipopita siku mbili alianza kuumwa sana hatimaye akawa ameaga dunia. Habari hizo za tanzia ziliniuma sana; kumpoteza wakili Jonas Mlyanyama, mtu ambaye alikuwa makini katika kazi yake.
‘Nilimwambia aiache kesi yangu naye akang’ang’ania kuendelea kuisimamia, ona sasa yaliyomfika. Laita kama angenisikia na kuachana na hii kesi asingekufa, huyu mwanamke ni hatari sana.’ Nilijiwazia huku moyo wangu ukiwa na simanzi kubwa kutokana na kifo cha wakili Mlyanyama.
Taarifa hizo ambazo zilitoka serikalini ziliendelea kunijuza kuwa kwa wakati huo nilikuwa natafutiwa wakili mwingine tena ambaye angeendelea kunitetea katika kesi yangu hiyo. Hata hivyo niliwaambia wasihangaike kunitafutia wakili mwingine kwani yangeweza kumtokea kama yaliyomtokea Jonas Mlyanyama.
“Hii kesi ina utata mkubwa mno kwani tangu mwanzo wake ni mauzauza matupu. Mimi nawaomba msinitafutie wakili yeyote, nitaimalizia mwenyewe.” Nilimwambia mtu aliyekuwa kaniletea taarifa hizo.
“Lakini una haki kisheria kutafutiwa wakili wa kukutetea?”
“Ndiyo nina haki, lakini kwa hali ilivyo katika kesi hii sioni maana yoyote ya kusababisha watu kupoteza maisha yao kwa ajili yangu, kesi yenyewe haina hata mwelekeo mzuri.”
“Haya bwana wewe wasema, mimi nitapeleka taarifa kama ulivyotaka.” Alimalizia mjumbe huyo na kuondoka zake.
MASKINI, WAKILI WA BRIGHTON ALIONYWA ILA AKAPUUZA, SASA YAMEMKUTA MAKUBWA! NINI HATIMA YA BRIGHTON? NA NI KWA NN MSICHANA HUYO KAMUANDAMA! USIKOSE KUFUATILIA SIMULIZI HII!

No comments:

Post a Comment