Thursday, October 17, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 31



ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA....
“Kwa nini kesho yake asubuhi ulikuwa unatusumbua na Kishoka ukigonga geti na kupotea kimiujiza?”
“Sikuwa mimi?”
“Alikuwa nani?”
“Mimi sijui.”
SASA ENDELEA.......
Baada ya kuona msichana huyo anakikataa kila nilichomuuliza hasira zilianza kuniingia. Ghafla likaniijia swali ambalo nilijikuta namuuliza kwa mtindo wa kuropoka vile.
            “Wewe ni mchawi?”
“Hapana mimi siyo mchawi.”
“Wewe ni jini?”
“Hapana mimi siyo jini.”
“Kama kweli wewe siyo jini hebu apa kwa Mungu ukisema kuwa wewe siyo jini?”
“Sasa niape ili iweje?” Aliongea Sharifa huku naye akionekana kuanza kuhamaki.
“A-aaah! Wewe hebu apa na kama siyo jini kweli hautadhurika na chochote.”
            Huku nikiwa nimechachamaa kumlazimisha Sharifa akiri kwa ulimi wake kuwa yeye siyo jini, nilisikia sauti ya jaji akiingilia kati mahojiano yetu.
“Naona mshtakiwa umekosa maswali ya msingi ya kumuuliza shahidi. Kama huna swali jingine sema ili nimruhusu shahidi atoke kizimbani.”
“Mheshimiwa jaji huyu mwanamke siyo mtu wa kawaida kabisa, na sielewi ni kwa nini kaniandama mimi tu katika dunia hii. Amini nakwambia alianza kunifanyia mauzauza siku moja kabla ya kifo cha Kishoka kutokea, hata wakili aliyekuwa akinitetea kayaona mauzauza na ndiyo maana alishindwa kabisa kuongea siku ile. Alianza kwa kumuonya aachane na kesi hii na kumuonya kuwa atamfanya kitu kibaya lakini wakili huyo hakutishika. Alipoona vile akaamua kumuua kabisa kwa kuona kwamba kakaidi, hebu muache aape kama kweli ni binadamu wa kaida, na endapo atakuwa siyo binadamu wa kawaida Mungu anaenda kumuumbua hapahapa!” Nilijaribu kujitetea kwa jaji.
“Unaswali jingine zaidi ya hilo?”
“Endapo ataapa maswali yatapatikana.”
“Shahidi, unaweza ukashuka kizimbani maana mshtakiwa hana jipya.” Alitamka jaji na kunifanya niishiwe nguvu.
            Nilipotupia jicho kwenye kizimba cha mashahidi nilimuona Sharifa akiondoka kizimbani hapo na kwenda kuketi. Kitendo cha kuondoka msichana huyo bila kufanya nilichokuwa nimemtaka akifanye kiliniumiza sana moyoni.
            Baada ya Sharifa kushuka kizimbani upande wa mashtaka ulimpandisa shahidi mwingine ambaye alikuwa ni miongoni mwa askari waliokuwa wamekuja kunikamata siku ya tukio.
            Mpaka anapanda kizimbani na kuapishwa kisha kutoa ushahidi wake, akili yangu haikuwa katika ushahidi wake bali ilikuwa ikimfikiria Sharifa tu. Tena kichwa changu kilikuwa kimevurugika vibaya vibaya kutokana na jaji kunikatalia ombi langu kwani niliamini kuwa endapo angekuwa ni jini kweli basi angeumbuka.
Alipomaliza kutoa ushahidi wake ambao haukuwa na tofauti kubwa sana na ule uliotolewa na askari wenzake aliokuja nao kwangu siku ya tukio, jaji aliniuliza kama nina swali kwa shahidi.
Kusema kweli nilikuwa sijasikia hata neno moja alilokuwa ameongea shahidi huyo wakati anatoa ushahidi wake kwa vile nilikuwa nimezama katika lindi la mawazo juu ya Sharifa. Sasa ningeuliza nini ilhali nilikuwa sijayanyaka maelezo yake hata kidogo!
Ili kukata mzizi wa fitina nilifumbua kinywa changu na kusema kwa mkato kwamba sina swali lolote kwa shahidi huyo. Ndipo jaji alipomruhusu aende kuketi.     
Baada ya hapo mwendesha mashtaka aliinuka na kumwambia jaji kuwa upande wa mashtaka ulikuwa umekamilisha mashahidi wake. Baada ya jaji kuambiwa hivyo aliniuliza kama nina mashahidi ili baraza lijalo nianze kuwaleta.
Nilichomjibu ni kwamba sina mashahidi kwani kesi yenyewe ilikuwa imeghubikwa na utata mkubwa, pia kutokana na mazingira yake jinsi yalivyokuwa.
 Baada ya kumwambia hivyo jaji aliutaka upande wa mashtaka kuandaa maelezo ya mashtaka kuonyesha ni kwanini unamuona mshtakiwa anahatia kwa mujbu wa ushahidi uliotolewa. Shauri hilo liliahirishwa tena kwa mwezi mmoja.

                        *************************
ITAENDELEA.......

No comments:

Post a Comment