Monday, October 14, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 28



ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA....
Alisema kuwa siku aliyotoka kuongea na mimi kwenye hospitali ya magereza alikutana na msichana aliyekuwa akitusumbua katika kesi hiyo. Msichana aliyekuwa amenisingizika kuwa nimeua wakati sijaua.
SASA ENDELEA.......
“Nilikutana naye sokoni niliposimama kununua matunda, ndipo akaniita wakati naingia kwenye gari niondoke zangu sokoni hapo. Kusema kweli nilikuwa sijamfahamu ila alipofika kwangu alijitambulisha.” Alieleza wakili Mlyanyama.
“Akakuambia vipi?” Nikamuuliza huku nikikaa makini kusikia alichomwambia wakili wangu.
“Eti kanionya niachane na kesi yako kwa sababu hainihusu, akadai vinginevyo nitapata matatizo makubwa.”
            Taarifa hiyo ilininyong’onyeza na kunifanya niishiwe nguvu.
“Hivyi huyu mwanamke ananitafuta nini mimi?” Nilimaka kwa machungu.
“Hata hivyo nilimwambia sitishiki na nikamtaka ajipange kujibu maswali yangu yangu siku atakayosimama kutoa ushahidi.”
“Lakini yule ni mtu hatari sana kaka, bora uachane tu na kesi yangu nisije nikakusababishia matatizo.” Nilimwambia wakili Mlyanyama.
“Hapana, hayo ni maneno ya vitisho tu, ameona hana hoja za kunikabili na huenda kashaambiwa jinsi ninavyowakaba maswali mashahidi wengini au huwa anakuja kinyemela na kashashuhudia.”
“Kaka mimi nimekuambia, yule msichana ni mchawi, hii kesi achana nayo tu wanihukumu yaishe.” Nilimwambia wakili huyo.
            Hata hivyo wakili huyo alikataa katakata kuiachia njiani kesi yangu. Aliapa kuwa na mimi bege kwa bega mpaka pale ambapo kingeeleweka. Alikuwa na kiu ya haki kwangu mithili ya mzee Toboa katika Kiu ya Haki.
            Tuliagana na kuachana huku tukisubiri kesho yake ifike ili nipande tena kizimbani kuendelea na kesi yangu. Nilizidi kupata wasiwasi juu ya hiyo kesi yangu. Kama mpaka yule wakili alikuwa kapewa vitisho na yule msichana, niliwaza bila kupata jibu ni kipi hasa alichokuwa akikitafuta msichana yule kutoka kwangu.
            Kwa kweli nilikuwa na mtihani, tena mzito. Nilitamani nikutane naye uso kwa macho  kisha nimuulize kinagaubaga ni nini hasa nilichokuwa nimemkosea ama ni kipi alichokuwa anahitaji kutoka kwangu.
            Kesho yake asubuhi tulisombwa tena na karandinga la magereza kuelekea mahakamani. Tulipofika mahakamani mimi nilipelekwa moja kwa moja mpaka ndani kwani kesi yangu ndiyo ilikuwa inaanzia kusikilizwa.
            Jaji alipoingia watu wote walisimama wakati sauti ya “kooort” iliposikika. Baada ya kutoa heshima ya mahakama watu wote waliketi, kesi yangu ikaendelea.
            Upande wa mashtaka uliendelea kuleta mashahidi wake ambapo baadhi ya polisi waliokuwa wamekuja kunikamata nyumbani siku ya tukio walisimama mmoja baada ya mwingine kutoa ushahidi.
            Wakili wangu hakuwa na maswali mengi sana ya kuwahoji. Yeye alichodai ni kwamba anamsubiri kwa hamu shahidi ambaye alitoa taarifa za tukio hilo kwenye kituo cha polisi. Shahidi huyo hakuwa mwingine bali ni yuleyule msichana mwenye kiinimacho.
            Baada ya polisi hao kuisha wote kutoa ushahidi, msichana huyo ambaye nilikuwa simjui hata jina aliinuka na kwenda kwenye kizimba cha upande wa pili kutoa ushahidi wake.
            Kama ilivyo ada, mwendesha mashtaka alimuongoza kutoa maelezo hatua kwa hatua.
“Mimi naitwa Sharifa Abdul.” Alitaja jina lake baada ya kuulizwa na mwendesha mashtaka.
“Sharifa, hebu ieleze mahakama ulikuwa wapi mnamo tarehe ishirini na moja mwezi wa kumi na moja mwaka jana muda wa jioni?” Ilikuwa ni sauti ya mwendesha mashtaka bwana Charles Ngonyani.
“Nakumbuka siku hiyo nilikuwa nyumbani kwangu Majengo mapya, ndipo nilipoamua kwenda kumtembelea kaka yangu ambaye ni marehemu Kishoka.”
“Endelea..,”
“Nilipofika alipokuwa akiishi kaka yangu huyo nilikuta milango ipo wazi.”
“Huyo kaka yako alikuwa akiishi wapi?” Mwendesha mashtaka aliuliza.
“Alikuwa akiishi mtaa wa Tumaini.”
“Alikuwa akiishi na nani?”
“Alikuwa amepanga na alikuwa akiishi na mmiliki wa nyumba hiyo.”
“Ehe, ulipokuta mlango upo wazi ulichukua uamuzi gani?”
“Kabla sijagonga nilisikia sauti ya kilio na makelele mle ndani ambapo sauti ya mtu aliyekuwa akitoa kilio niliitambua.”
“Ilikuwa ni sauti ya nani?”
“Ilikuwa ni sauti ya kaka yangu Kishoka.”
“Uliposikia hivyo ulifanyaje?”
“Niliamua kuingia mpaka sebuleni, hata hivyo makelele hayo yalikuwa yakitokea chumbani.”
“Chumba hicho kilikuwa ni cha nani?”
“Kilikuwa ni cha mmiliki wa nyumba hiyo.”
“Baada ya hapo ulifanyaje?”
“Baada ya kuuona hata mlango wa chumbani haujafungwa, nilianza kwenda kwa tahadhari kubwa kuchungulia kilichokuwa kinaendelea ndani ya chumba hicho.”
            “Uliweza kuchungulia humo ndani?”
“Ndiyo!”
“Ulipochungulia uliona nini?”
“Nilichokiona sikuamini kwa macho yangu. Nilimuona kijana mwenye nyumba akimchinja Kishoka kama mbuzi wa sherehe achinjwavyo huku kamfunga kamba miguuni na mikononi.”
“Ulipoona hivyo uliamua nini?”
“Kwanza niliongopa kuongea chochote kwa kuhofia usalama wangu. Kwa bahati nzuri nilikuwa na kamera kwenye mkoba wangu, nikaitoa na kuanza kupiga picha.”
“Baada ya hapo afanyaje?”
“Nilitoka na kuondoka mbio kurudi nyumbani, wakati nikiwa njiani nilipiga simu kituoni na kutoa taarifa hizo.”
“Hizo picha ulizozipiga siku ya tukio unazo?”
“Ndiyo zimo kwenye kamera yangu hii.” Aliongea Sharifa huku akiionyesha mahakama kamera ndogo ya digitali.
“Huyo mtu aliyefanya hayo mauaji ukimuona unaweza ukamfahamu?”
“Bila shaka!”
“Hebu tuonyeshe kama mtu huyo yumo humu ndani ya mahakama!”
“Ni yule pale kwenye kizimba.” Aliongea msichana huyo huku akinisonta.
JE, WAKILI WA BRIGHTON ATAWEZA KUMKABILI KWA MASWALI MSICHANA ALIYEMUONYA AACHANE NA HIYO KESI? NA NI MADHARA YAPI ATAYAPATA KWA KUKAIDI ONYO LA MSICHANA HUYO? USIKOSE TOLEO LIJALO!         

No comments:

Post a Comment