Wednesday, October 30, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 38


ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA...
Baada ya kuwaza kidogo alikumbuka kuwa bastola yake ilikuwa imebakiza risasi moja ndani. Ndipo alipoamua kujimaliza na yeye kwa kujipiga risasi.
SASA ENDELEA.......
Wakati huo nilikuwa namfuatilia kwani machale yangu yalikuwa yamenicheza. Wakati anaondoka nyumbani alikuwa kashaniambia kuwa anaenda kwa mpenzi wake ila alikuwa akienda bila ya taarifa huku akiyavunja masharti aliyokuwa amepewa na mpenzi wake huyo. 
Niliamua kumfuatilia ili nikashuhudie ‘timbwilitimbwili’ nililokuwa nikilitegemea kuibuka baada ya kaka James kufika kwa mpenzi wake huyo. Hata kama yangetokea mapigano kisha kaka yangu akazidiwa basi mimi ningekuwepo nyuma yake kuokoa jahazi.
Hata hivyo aliniacha njiani kwani alikuwa akiendesha gari lake kwa kasi mno. Mimi nilikuwa naogopa ajali hivyo nikawa naendesha mwendo wa kistaarabu.
Kwenda kwangu polepole ndiyo kulinifanya nimkose kaka James katika dunia hii kwani nilichelewa kiduchu mno. Wakati naufikia mlango wa chumba walichokuwamo kina Neila, tayari kaka James alikuwa kashakitekenya kitufe cha kufyatulia risasi huku akiwa amejilenga kwenye kichwa chake.
Nilimshuhudia kaka James akianguka mzima mzima kisha akakata roho. Ndipo nilipopoteza fahamu na kushindwa kuelewa kilichokuwa kikiendelea.
Fahamu zilinijia masaa matano mara baada ya tukio hilo kutokea. Nilijikuta nipo wodini huku nikiwa nimetundikiwa drip ya maji. Nilishangaa sana kujikuta nipo hospitali.
Katika kuvuta kumbukumbu nilikumbuka jinsi mambo yalivyokuwa masaa matano yaliyokuwa yamepita. Nilikumbuka kuwa kaka James hakuwepo tena duniani.
Nilizidi kuchanganyikiwa, akili yangu ikazidi kuvurugika baada ya kukumbuka hilo tukio lililokuwa na tanzia kubwa katika moyo wangu na akili yangu kwa ujumla.
Sikuona kabisa mantiki ya kuendelea kubaki hospitali wakati nyumbani kulikuwa na msiba wa marehemu kaka yangu. Sikujua ni vipi mipango ya mazishi ilikuwa inapangwa huko kwani mimi ndiyo nilikuwa ndugu wa pekee wa marehemu. Kwa kifupi mhusika mkuu wa msiba huo nilkuwa ni mimi.
Nilipojaribu kuangaza angaza niliona karibu wagonjwa wote wamelala kwenye vitanda vyao kila mmoja. Sikuona muuguzi wala dakitari yeyote aliyekuwemo kwenye wodi hiyo.
Bila kuchelewa wala kuduwaa niliichomoa sindano ya drip na kutoka mbio kuelekea nyumbani kuungana na majirani kuomboleza kifo cha kaka James.
Kwa vile James alikuwa mtu mashuhuri sana katika mji huo, tayari taarifa za kifo chake zilikuwa zimeshazagaa mtaani na katika mji wote kwa ujumla.
Nilipofika nyumbani niliwakuta watu wengi wameshakusanyika. Hata hivyo mwili wa marehemu ulikuwa upo hospitali umehifadhiwa kwa uchunguzi zaidi. Nilijumuika na watu waliokuwa wameshafika, maombolezo yakaendelea.
Watu walizidi kumiminika kuja kunipa faraja kwenye msiba huo. James alikuwa ni mtu wa watu, alijua kukaa vizuri na majirani pamoja na watu wengine aliokuwa akifahamiana nao. Hali ya watu kujaa ilinifariji kwa kiasi fulani ingawaje moyo wangu ulikuwa umeghubikwa na majonzi yasiyokuwa kifani.

            ******************************

ITAENDELEA....

No comments:

Post a Comment