Monday, November 4, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 39

ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA...
Watu walizidi kumiminika kuja kunipa faraja kwenye msiba huo. James alikuwa ni mtu wa watu, alijua kukaa vizuri na majirani pamoja na watu wengine aliokuwa akifahamiana nao. Hali ya watu kujaa ilinifariji kwa kiasi fulani ingawaje moyo wangu ulikuwa umeghubikwa na majonzi yasiyokuwa kifani.

            ******************************
SASA ENDELEA.......
Pamoja na kwamba ni miezi kadhaa ilikuwa imepita tangu kifo cha kaka James kutokea, akili yangu ilikuwa haijachanganya kabisa. Kila nilichokuwa najaribu kukifanya nilikiona hakifai.
Kifo hicho kilikuwa kimetonesha donda jingine kwenye mtima wangu ambalo lilikuwa bado halijapona. Donda hilo nilikuwa nalifananisha na donda ndugu kwani lilikuwa limechukua muda mrefu sana bila kupona ndani ya moyo wangu.
Usiombe kupata majeraha palipo na donda ndugu mpenzi msomaji. Hebu fikiria maumivu yake yatakavyokuwa. Ni zaidi ya uchungu!
Donda lililotoneshwa na kifo cha kaka James ni lile lililokuwa limeachwa na kipenzi cha roho yangu marehemu Anna pamoja na wazazi wangu, hasa hasa kile cha Anna.
Kuondoka kwa Anna katika dunia hii kuliniathili pakubwa sana kisaikolojia na athari yake hiyo ilikuwa bado haijaisha moyoni mwangu.
Mpaka leo huwa sipati jibu ukiwa wanaoupata wale wanaoondokewa na wenzi wao wa ndoa wanaowapenda kwa dhati. Ikiwa mimi niliipata freshi kwa mpenzi tu ambaye tulikuwa hata bado hatujaoana, wao sasa inakuwaje ukizingatia tayari wameshaonja tamu ya ndoa?
Marehemu Anna alikuwa ni msichana wa pekee ambaye nilitokea kumpenda kipindi nasoma. Mimi nilikuwa nasoma elimu ya sekondari yeye alikuwa bado yupo shule ya msingi.
Uzuri wa sura yake, umbo pamoja na tabia ndivyo vilikuwa vimenichengua mtoto wa kiumi mpaka nikawa sijiwezi, nikafa na kuoza kwake kama vijana wa kileo wasemavyo. Mtoto alikuwa yupo kamili gado, kamili kila idara.
Mpaka wa leo huwa natafutia msichana mwenye sifa kama zake lakini naambulia hola! Wasichana wa namna hiyo ni adimu sana kuwapata, yaani ni sawa na kumsaka bikira uswahilini kwani unaweza ukakesha bila hata ya kumpata.
Mapenzi yetu hayakuwa kama mapenzi yale yanayofanywa na vijana wa siku hizi, mapenzi ya kuanza kuzini kabla hata hamjafunga ndoa. Eti wao husema huwezi ukauziwa mbuzi kwenye gunia; wapi ndugu zangu hizo ni roho za pepo wachafu tu, pepo wa uzinzi.
Ndiyo zao vijana wa siku hizi, hasa wavulana. Utakuta wanakwambia kumuoa mwanamke huku hujafanya naye mapenzi ni kosa la jinai kwani unaweza ukakuta hayawezi ‘mahabati’,mwenye kutulia kama gogo kwenye mambo fulani. Wanasema yote hayo ni tisa, kumi ukute bwawa na siyo kisima, au ukutane na ile timu ya Songea; unaweza ukatangaza taraka. Hiyo ndiyo mitazamo yao.
Mimi hayo sikujali kwani niliona ni upuuzi na ulimbukeni mkubwa unaotokana na utumwa wa mapepo ya uzinzi. Kutokana na misingi mizuri ya kidini niliyokuwa nimefundishwa tangu utotoni niliamini kuwa hakuna linaloshindikana mbele ya Mwenyezi Mungu.
Kama yeye huwatakasa mpaka wenye ukoma, kwa nini asikibadilishe kitu chochote kinacholeta kikwazo kwako kilichopo kwenye mwili wa mwenzi wako wa ndoa uliyemuoa kwa ndoa halali kabisa? Yote yanawazekana.  
Hivyo ndivyo mitazamo wetu ilivyokuwa. Bahati nzuri ni kwamba Anna alikuwa bado hajaupoteza usichana wake na mimi nilikuwa sijaupoteza uvulana wangu. Wote tulikuwa safi kabisa.
Pamoja na kupendana kwetu lakini tulikubaliana kutofanya mapenzi mpaka tuje kufunge ndoa kwani kinyume na hapo ni dhambi kwa Mungu, dhambi ya kuzini ambayo inawatafuna vijana wengi wa siku hizi.
Huo ndiyo huitwa upendo wa kweli, mapenzi yasiochuja mpaka uzeeni. Siyo mapenzi feki ambayo leo mko pamoja halafu kesho mnazinguana na kushika hamsini zake kila mmoja.
Kifo cha Anna ndiyo kilizima taa za upendo moyoni mwangu na kuacha giza totoro ambalo mpaka leo ni athari kubwa kwangu.
Alikuwa anajipenda, alikuwa anajiheshimu, wala hakuwa mapepe na ndio maana vijana wengi wa mtaani walitamani sana awe wao matokeo yake waliishia kula ‘vibuti’ vya uso.
Amini usiamini siku zote mti wenye matunda ndiyo hupigwa mawe. Kutokana na usemi huo, kipenzi Anna nilimfananisha na mti wa mnazi ambao hata ukiupopoa kwa mawe huwezi kuangusha nazi wala dafu. Kumbe nilikuwa najidanganya kwani kuna wakwezi ambao hupanda mpaka matunda yaliko kisha huanza kuyasanifu kwa vyovyote vile wanavyotaka.
Hicho ndicho kilichotokea kwa marehemu Anna. Pamoja na kuwa na msimamo zaidi ya binti wa kilokole, ilifika siku maagano yetu yakavunjika japokuwa siyo kwa ridhaa na utashi wake.
Ilikuwa ni siku ngumu sana kwake; siku aliyorubuniwa na dada yake kisha wakaenda kwenye sherehe ya kuzaliwa ya mpenzi wa huyo dada yake. Kumbe kulikuwa na mipango kabambe ya kumwingiza kipenzi changu kwenye jaribu zito lililokuja kupelekea kifo chake.

ITAENDELEA.....

No comments:

Post a Comment