Friday, November 29, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 49

Brighton anaota ndoto ya ajabu akiwaona watu waliokufa siku nyingi kwa kujiua wakiwemo mzee Mboma, Patrick, James na Anna. Baada ya ndoto hiyo anazongwa na mwanadada Sharifa anayemsababishia kesi ya mauaji ya mpangaji wake, yaani Kishoka. Kesi inaunguruma mahakamani kisha anajikuta akihukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe kwa kosa la mauaji ya Kishoka, kosa ambalo alikuwa hajalitenda. Akiwa gerezani akisubiri tarehe za kunyongwa anakutana na Mack, jamaa aliyekuwa amenunua nyumba iliyokuwa ya marehemu James, naye Mack anaanza kumhadithia kisa kilichompelekea afungwe jela.
Kwa kusimuliwa na Mack, Brighton anayasikia mengi kuhusu mali alizokuwa amerithi kutoka kwa marehemu kaka yake kwa kila aliyekuwa amemuuzia aliishia kupatwa na matatizo akiwemo Mack mwenyewe. Hatimaye siku ya kunyongwa inafika kweli, hata hivyo anajikuta anakolewa kimiujiza na msichana aliyemsingizia kuua, yaani Sharifa, anatolewa gerezani na kuwa huru kabisa.
Anaporudi kwake anakuta nyumba yake ishauzwa na mtu aliyekuwa amemwachia.  Sasa endelea...................

Wakati nagonga wimbo uliokuwa unakita ulifikia mwisho, hapo hapo na mimi nikagandamizia kuendelea kugonga ili nipate kusikika. Kabla wimbo mwingine haujaanza kusikika niliweza kuona mlango ukifungulia. Ndipo alipotoka kijana ambaye nilikuwa namfahamu; alikuwa akiitwa Benja.
            Hata hivyo hakuonyesha dalili zozote za kuweza kunitambua. Nilikuwa nimebadilika si mchezo. Sikuwa kama Brighton wa kipindi kile, enzi hizo kina Mapara na hao kina Benja walikuwa wanapenda kuniita pedeshee mtoto, jina ambalo nilikuwa nalipinga vikali kwani nilikuwa sipendi majisifu.
            Nilipogundua kwamba hajanifahamu nilianza kujiuliza,
‘Sijui nimkumbushe, sijui nijikaushe tu ili siri yangu izidi kudumu. Lakini nikijikausha atanipa michapo yote kuhusu Mapara?” Nilizidi kuwaza na kuwazua wakati tukisalimiana.
            Suala la kujikausha ndilo lililopitishwa na halmashauri ya ubongo wangu japokuwa kama angekuwa mgumu kunieleza habari nilizokuwa nazihitaji basi ningejifunua kwake.
            Baada ya salamu mazungumzo yaliendelea,
“Karibu bwana!”
“Asante!”
“Karibu pita ndani.”
“Asante lakini nipo haste haste kidogo, namulizia Mapara.”
“Unamuulizia Mapara?”
“Ndiyo!”
“Ni nani yako huyo Mapara?”
“Ni rafiki yangu!”
“Mara ya mwisho kuonana naye ilikuwa ni lini?”
“Ni miaka mingi kidogo lakini sikumbuki”
            Maswali ya Benja aliyokuwa akiuliza mfululizo utadhani naye ni polisi yalianza kunikera. Hata hivyo niliona nikianza kumjibu utumbo sitafanikisha nilichokuwa nakihitaji. Nililazimika kuwa mpole kama simba jike anapozaa ili nifanikishe suala langu, suala la kupata habari za Mapara.
            Niliendelea kjitahidi kumjibu kila swali alilouliza.
“Wewe ni mwenyeji wa wapi?”
“Ni mwenyeji wa mji huu huu ila nilisafiri siku nyingi.”
“Dah! Huyu Mapara ana miaka mingi sana hayupo nchi hii!”
“Yupo nchi gani sasa?”
“Hata mimi sijui ila ninachojua ni kwamba huwezi ukampata mji huu wala nchi hii.”
            Mpaka hapo nilikuwa nimeishiwa maji. Mambo yalizidi kuniwia ugumu baada ya kuambiwa kuwa Mapara alikuwa yupo nchi za ng’ambo.
            Hata hivyo nilijua dhahiri ya kwamba Benja alikuwa ananificha kunieleza habari kamili. Niliamini kabisa kuwa alikuwa anajua mambo mengi sana kuhusu Mapara kwani alikuwa ni mtu wake wa karibu sana.
            Baada ya kuona mambo yamenikaa vibaya sikuwa na budi kunyolewa. Nilimuomba Benja tuingie ndani kwake ili nikamuelezee matatizo yangu kwani nilikuwa na matatizo makubwa.
            Benja hakukataa. Alinikaribisha ndani nami nikaingia. Tulipofika ndani nilimweleza kinaga ubaga bila kumficha kitu chochote kuhusu kesi yangu ilivyoenda, hukumu mpaka kutoroka kwangu siku hiyo ambayo ilikuwa ndiyo siku ya kunyongwa.
            Alistaajabu sana kusikia hivyo.
“Unajua nilikuwa nakufananisha kwa mbaali lakini nikawa najiambia mwenyewe itawezekanaje mtu aliyehukumiwa kunyongwa aonekane tena uraiani? Na ingekuwa kwa msamaha wa rais basi tungesikia kwenye vyombo vya habari.”
            Kabla hatujaanza hata maongezi yetu Benja aliniambia nimsubiri kidogo, alitoka nje na kwenda sehemu ambapo sikukujua. Huku nikiwa ndani niliendelea kusikiliza nyimbo za mziki wa kizazi kipya ambao niliuacha ndiyo kwanza unachipuka.
            Hata hivyo nilihisi mabadiliko makubwa sana kwenye mziki huo kwani nyimbo zilikuwa na ubora wa hali ya juu kushinda enzi zile bado sijafungwa. Kweli kuwa jela ni sawa na kutokuwa kwenye hii dunia kwani unakuwa hujui kinachoendelea uraiani.
            Baada ya muda usiozidi nusu saa niliona mlango ukifunguliwa, ndipo alipotokea Benja akiwa na kifuko kaning’iniza ambamo kulikuwa na chakula.
            Alinitengea nami nikaanza kula. Kusema kweli nilikuwa na njaa ya kufa mtu. Tumbo nilikuwa likisokota kwa njaa si mchezo. Nilianza kula chakula kilichokuwa kimeletwa na Benja kutoka mkahawani.
            Nilipomaliza kula mazungumzo yalianza. Shauku yangu kubwa ilikuwa ni kusikia habari za Mapara. Hata hivyo kwa wakati huo nilikuwa na uhakika wa kusikia habari zote za Mapara kutoka kwa Benja kwani ukaribu wao ulikuwa ni kama pete na chanda.

JE, BRIGHTON ATAAMBIWA HABARI GANI ZA MAPARA NA MWENYEJI WAKE BENJA? JIBU LIPO TOLEO LIJALO.

Wednesday, November 27, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 48


            Brighton anaota ndoto ya ajabu akiwaona watu waliokufa siku nyingi kwa kujiua wakiwemo mzee Mboma, Patrick, James na Anna. Baada ya ndoto hiyo anazongwa na mwanadada Sharifa anayemsababishia kesi ya mauaji ya mpangaji wake, yaani Kishoka. Kesi inaunguruma mahakamani kisha anajikuta akihukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe kwa kosa la mauaji ya Kishoka, kosa ambalo alikuwa hajalitenda. Akiwa gerezani akisubiri tarehe za kunyongwa anakutana na Mack, jamaa aliyekuwa amenunua nyumba iliyokuwa ya marehemu James, naye Mack anaanza kumhadithia kisa kilichompelekea afungwe jela.
Kwa kusimuliwa na Mack, Brighton anayasikia mengi kuhusu mali alizokuwa amerithi kutoka kwa marehemu kaka yake kwa kila aliyekuwa amemuuzia aliishia kupatwa na matatizo akiwemo Mack mwenyewe. Hatimaye siku ya kunyongwa inafika kweli, hata hivyo anajikuta anakolewa kimiujiza na msichana aliyemsingizia kuua, yaani Sharifa, anatolewa gerezani na kuwa huru kabisa.
Anaporudi kwake anakuta nyumba yake ishauzwa na mtu aliyekuwa amemwachia.  Sasa endelea...................

Hata hivyo nilijishauri mwenyewe kuwa kama ningeenda kwenye nyumba hiyo basi ningeonekana kwa watu wengi, na hofu yangu ilikuwa ni kuvuja kwa siri ya kutoroka gerezani.
            Nilijua fika dunia haina siri na walimwengu hawana dogo. Kitendo cha kuniona tu basi wangeanza kuhoji kutaka kujua kulikoni. Watu wengi walikuwa wanajua fika kuwa mimi nilihukumiwa kifo, sasa kuonekana pale mtaani kungeweza kuzua gumzo na kuniletea matatizo mengine tena, huenda ningejikuta nakamatwa na vyombo vya dola.
            Hata wakati naenda kwenye nyumba yangu hiyo nilienda kwa kujificha ficha sana ili nisionekane kwa watu wa mtaa ule. Lengo langu lilikuwa ni kwamba nifike kwa Mapara na kumwambia tufanye mipango ya kuhama mji huo kinyemera na kuenda katika mji mwingine ambao ingekuwa vigumu watu kunishtukia.
            Akili yangu ilikuwa imenituma kuuza kila kitu kisha kutimkia mji wa mbali ambako ningeweza kuishi kwa raha zangu bila kushtukiwa mpango wangu wa kutoroka jela.
            Sasa kitendo cha kuambiwa Mapara hakuwa anaishi hapo tena kiliichokesha akili yangu mara dufu. Nikawa nawaza cha kufanya bila kupata majibu.
            Jamaa baada ya kuniona nimekaa kimya kirefu nikiwaza kwa kina huku nikipiga miayo mfululizo isiyo na idadi; aliamua kuzama ndani kisha akafunga geti ‘paa!’ Nilibaki pale nje peke yangu nikiwaza na kuwazua bila kupata muafaka wa mawazo yangu.
            Hatimaye niliamua kuchukua maamuzi ya hatari kwani sikuwa na jinsi.
‘Potelea mbali kifo hakina breki, ngoja niende hapo hapo alipokuwa kapanga Mapara ili nikajaribu kuulizia kama bado kapanga hapo au la!’ Nilijishauri na kuanza kuondoka.
            Kwa jinsi nilivyokuwa nimekonda ilikuwa ni vigumu sana kwa mtu yeyote aliyekuwa akinifahamu kugundua kwa haraka kuwa ndiyo mimi. Ukizingatia miaka mingi sikuwepo mtaani hapo na pia watu walikuwa wameshanifuta hata katika fikra zao kutokana na hukumu niliyokuwa nimepewa, yaani hukumu ya kunyongwa; basi niliweza kupishana nao kama vile hatujuani.
            Nilienda moja kwa moja mpaka kwenye nyumba alimokuwa kapanga Mapara. Nikaingia mpaka ndani ya nyumba hiyo. Moja kwa moja nilienda mpaka kwenye chumba alichokuwa akikaa.
            Nilipogonga ilisikika sauti ya mwanamke ikiniitikia.
‘Huyu jamaa kashavuta jiko nini?’ yalikuwa ni mawazo yangu baada ya kuisikia sauti ya mwanadada huyo.
            Mara mwanamke mrembo alifungua mlango na kutoka kidogo kisha akasimama mlangoni kwa mtindo wa kuegemea mlango. Alikuwa ndani ya kanga tu lakini kanga hizo zilikuwa ni mbili, ya kwanza ilikuwa imeanzia kifuani kuyafunika maziwa na ya pili ilikuwa imeanzia kiunoni.
            Nilimsabahi naye akaitikia. Kilichofuata baada ya salamu ni kumuuliza habari za Mapara.
“Mh! Mapara, mbona simfahamu?” Alijibu mwanamama huyo aliyekuwa na uzuri wa shani.
            Baada ya kujibiwa hivyo moyo wangu ulishtuka utadhani umepigwa shoti ya umeme. Tumbo likawa joto kwani dalili za mambo kuzidi kuniwia ugumu zilikuwa zinajidhihirisha waziwazi. Wahenga walisema dalili ya mvua ni mawingu, pia mwanzo wa ngoma siku zote huwa ni lele.
            “Kwani wewe siyo mpangaji wa siku nyingi hapa?” Nilimhoji  mama huyo.
“Ndiyo sina siku nyingi hapa, nina miezi kama mitano hivi tangu kuhamia kwenye hiki chumba.”
“Ndiyo maana, kwa maana Mapara alikuwa kapanga kwenye chumba hikihiki na  ni muda mrefu umepita tangu nifike kumsabahi.”
“Labda muulize kaka wa kwenye chumba  kinachofuata kwani huwa nasikia yeye ndiyo mkongwe zaidi hapa.”
“Sawa, asante kwa msaada wako.”
“Wala usijali, karibu tena.”
“Nimekaribia.” Nilijibu kisha nikaondoka kwa hatua za taratibu kabisa mpaka kwenye chumba kilichofuata.
            Kwa adabu zote nilianza kuugonga mlango. Sikujibiwa chochote. Mle ndani kulikuwa na mdundo wa redio uliokuwa ukikita kwa sauti utadhani ni ukumbi wa disko.
            Niliamua kugonga tena kwa kuamini kuwa labda nilipogonga kwa mara ya kwanza hawakusikia kutokana na makelele ya redio. Tena safari hii nililazimika kuukaza mkono ili kuwafanya waliokuwemo humo ndani wanisikie.

JE, HICHO CHUMBA ANAISHI NANI? NA JE, BRIGHTON ATAPATA UFUMBUZI WA MASWALI YAKE? USIKOSE KUSOMA TOLEO LIJALO.    

Monday, November 25, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 47

Brighton anaota ndoto ya ajabu akiwaona watu waliokufa siku nyingi kwa kujiua wakiwemo mzee Mboma, Patrick, James na Anna. Baada ya ndoto hiyo anazongwa na mwanadada Sharifa anayemsababishia kesi ya mauaji ya mpangaji wake, yaani Kishoka. Kesi inaunguruma mahakamani kisha anajikuta akihukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe kwa kosa la mauaji ya Kishoka, kosa ambalo alikuwa hajalitenda. Akiwa gerezani akisubiri tarehe za kunyongwa anakutana na Mack, jamaa aliyekuwa amenunua nyumba iliyokuwa ya marehemu James, naye Mack anaanza kumhadithia kisa kilichompelekea afungwe jela.
Kwa kusimuliwa na Mack, Brighton anayasikia mengi kuhusu mali alizokuwa amerithi kutoka kwa marehemu kaka yake kwa kila aliyekuwa amemuuzia aliishia kupatwa na matatizo akiwemo Mack mwenyewe. Hatimaye siku ya kunyongwa inafika kweli, hata hivyo anajikuta anakolewa kimiujiza na msichana aliyemsingizia kuua, yaani Sharifa, anatolewa gerezani na kuwa huru kabisa.  Sasa endelea...................

            ‘Ina maana Mapara keshakuwa mbunge siku hizi, au ndiyo ile tabia ya kujiweka ‘matawi ya juu’ na kulazimisha uheshimiwa pale mtu anapozinyaka.’ Nilizidi kuwaza huku nikitafuta majibu ya kumpatia jamaa huyo aliyekuwa kavimbisha tumbo lake kwenye kimlango kidogo cha geti langu.
            Kwa kweli ilikuwa ikiniwia ugumu jinsi ya kuanza kuuliza kuhusu huyo mhesimiwa aliyekuwa anasemwa yuko nje ya nchi. Wazo la kwamba Mapara keshakuwa mtu mkubwa kiasi kwamba mpaka akafikia hatua ya kuitwa mheshimiwa; lilikuwa haliniijii kabisa akilini.
            Mapara alikuwa hajasoma sana kiasi cha kuweza kugombea hata udiwani. Alikuwa kaishia darasa la saba tu, tena la saba lenyewe alikuwa ni ‘bongo lala’ kitu ambacho asingeweza kugombea kutokana na mabadiliko ya utandawazi tuliyonayo siku hizi.
            Siku hizi udiwani ni kuanzia ‘form four’, tofauti na siku za nyuma ambapo utamkuta diwani darasa la saba. Mambo yamebadilika, watu wameshaupumuzisha uongozi wa kianalogia na sasa hivi ni mwendo digitali mpaka kwenye umwenyekiti wa kitongoji ama umwenyekiti w serikali za mtaa.
            Sababu hiyo ndiyo ilizidi kuweta fukuto ndani ya kichwa changu. Nikawa nashindwa nianze vipi kuuliza habari za huyo Mapara niliyekuwa nimemuachia nyumba yangu pamoja na miradi yangu yote.
            “Kwani hapa ni kwa nani?” Nilijikuta naropoka kuuliza.
Jamaa aliguna kwanza kisha akasema,
“Watu wengine sijui mkoje, kwa hiyo wewe wakati unatoka huko ulikuwa unajua hapa ni kwa nani?” Swali hilo lilielekezwa kangu.
            Akili yangu ilizidi kukorogeka na kuvurugika. Nikajikuta nimeropoka tena,
“Kwani Mapara ndiyo mwenye nyumba hii?”
“Siyo bure wewe ni zuzu, maana tangu umefika sijaelewa hata kimoja unachoniambia. Hebu nenda moja kwa moja kwenye pointi yako ya msingi iliyokuleta hapa.” Alimaka jamaa huyo.
            Nikaona alichokuwa amekiongea ni kitu cha msingi, nikaona niende moja kwa moja kwenye pointi. Hata hivyo nilikuwa naogopa kumwambia kuwa nimeponea chupuchupu kunyongwa nikihofia siri itafichuka.
            “Sikiliza kaka, mimi ni mwenyeji kabisa wa mji huu ila nilitoka miaka kadhaa iliyopita. Sasa wakati natoka aliyekuwa akiishi hapa ni jamaa mmoja Mapara, la sijui mpaka sasa anakaa hapa?”
“Alaaha! Sasa nimekusoma. Hapa haishi huyo Mapara unayemsema, hapa ni kwa mheshimiwa mbunge na ni mwaka wa tatu sasa anaishi hapa, huyo uliyemtaja mimi hata simjui.”
             Kauli hiyo ilinifanya niishiwe nguvu. Nilizidi kuchoka. Mtu pekee ambaye nilikuwa nikitegemea aje awe msaada mkubwa kangu alikuwa ni Mapara, naye nilikuwa nimemkosa. Mtihani uliofuata ni wa kujiuliza pa kumpata.
            Wakati wa sakata la kifo cha Kishoka, Mapara alikuwa ndiyo mtu pekee aliyekuwa anakuja kunisalimia kituo cha polisi pamoja na kuniletea chakula. Hata nilipohamishwa na kupelekwa mahabusu ya magereza aliendelea kuwa anakuja kuniona.
Ndipo nilipomkabidhi funguo za nyumba yangu pamoja na majukumu mengine ya kusimamia miradi yangu.
            Hakuwa rafiki yangu ki vile japokuwa tulikuwa tunafahamiana sana kwa vile yeye ndiye alikuwa mmoja wa watu walionipokea kwenye mtaa huo wakati nahamia.
            Baada ya kuambiwa hivyo nikawa njia panda. Nikaanza kujiuliza sijui niende alipokuwa akiishi kwa kipindi kile ambapo alikuwa amepanga chumba kwenye nyumba moja iliyokuwa na wapangaji lukuki!

JE, NINI KITAFATIA? USIKOSE....

Saturday, November 23, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 46

            
Brighton anaota ndoto ya ajabu akiwaona watu waliokufa siku nyingi kwa kujiua wakiwemo mzee Mboma, Patrick, James na Anna. Baada ya ndoto hiyo anazongwa na mwanadada Sharifa anayemsababishia kesi ya mauaji ya mpangaji wake, yaani Kishoka. Kesi inaunguruma mahakamani kisha anajikuta akihukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe kwa kosa la mauaji ya Kishoka, kosa ambalo alikuwa hajalitenda. Akiwa gerezani akisubiri tarehe za kunyongwa anakutana na Mack, jamaa aliyekuwa amenunua nyumba iliyokuwa ya marehemu James, naye Mack anaanza kumhadithia kisa kilichompelekea afungwe jela.
Kwa kusimuliwa na Mack, Brighton anayasikia mengi kuhusu mali alizokuwa amerithi kutoka kwa marehemu kaka yake kwa kila aliyekuwa amemuuzia aliishia kupatwa na matatizo akiwemo Mack mwenyewe. Hatimaye siku ya kunyongwa inafika kweli, hata hivyo anajikuta anakolewa kimiujiza na msichana aliyemsingizia kuua, yaani Sharifa, anatolewa gerezani na kuwa huru kabisa.  Sasa endelea...................

             Mlango wa chumba kile ulikuwa umefungwa. Nilishangaa kuona tunapenye kwenye ukuta kama vile tunapita sehemu yenye uwazi.
            Tuliendelea kutembea kwa hatua za madaha huku akiwa amenishika mkono. Tulitokezea mpaka nje ya jengo tulilokuwemo. Tukaendelea kutembea kuelekea kwenye lango kuu la kuingilia kwenye magereza hiyo.
            Niliweza kuwashuhudia askari magereza wakizunguka zunguka na wengine wakiwasimamia wafungwa waliokuwa wanafanya kazi kwenye ngome ya gereza hilo.
            Katika fikra zangu nilijua kuwa kila mtu anatuona, nikaona nimuulize Sharifa,
“mbona tunatoka kwa kujiamini hivi? Hao askari wakituona si tutapata tabu?”
“Hapa hatuoni mtu yoyote hata tupite palepale aliposimama, labda ngoja nikupe mfano kwa ofisa yule tunayekutana naye.” Alinijibu huku akinionyesha ofisa mmoja tuliyekuwa tunakutana naye.
            Alipomsogelea alimwasha kibao cha haja. Ofisa huyo aliishia kujipapasa tu na hakujua alikuwa kapigwa na nani. Nilianza kucheka kwa kicheko cha chinichini baada ya kukishuhudia hicho kisanga.
            “Hata ukicheka kwa sauti hamna atakayekusikia. Usiwe na wasiwasi upo kwenye mikono salama kabisa.” Aliniambia baada ya kuniona nacheka kwa chinichini.
            Tulitembea mpaka tukafika kwenye geti kubwa. Tulipita bila ya kubughudhiwa na mtu yeyote. Tulipofika nje akaniambia niende mpaka nyumbani kwangu halafu mambo mengine tutayaongea hapo baadaye.
            Nilipojaribu kumuuliza kuwa yeye anaelekea wapi kwa wakati huo aliniambia sipaswi kujua. Nilimuaga na kumshukuru kwa kuniokoa na adhabu iliyokuwa inanikabili kisha nikaanza mdogomdogo kuchapa lapa kuelekea nyumbani kwangu.
            Wakati namuaga alikuwa kasimama barabarani. Nilitembea kidogo kisha nikageuka nyuma kumwangalia. Lahaula! Sikumuona tena.
            Akili yangu ilibaki kuwa na kazi ya ziada japo kuwa nilikuwa nimetoka jela na nimenusurika na adhabu ya kunyongwa. Kikubwa kilichokuwa kinaniumiza akili ni hayo masharti yake. Mpaka muda huo nilikuwa sijajua ni masharti gani atanipa. Kilikuwa ni kitendawili kigumu sana akilini mwangu.
            Nilifuata barabara nikitembea kwa miguu kwani mifuko yangu ilikuwa imetoboka, yaani sikuwa hata na shilingi. Njiani nilikoma na moshi wa magari. Sikuwa na cha kufanya zaidi ya kuyakenulia meno magari yote yaliyokuwa yakinipita kwa vile sikuwa na nauli.
            Safari ya kutoka lilipokuwa gereza nililokuwa nimefungwa mpaka nyumbani kwangu ni mwendo wa masaa mawili kwa miguu. Kibaya zaidi mambo ya kuombana lifti hayakuwepo kabisa katika mji huo. Niliendelea na ‘ba funika ba funua’ mpaka nikafika.
            Nilifika mpaka kwenye geti la fensi ya nyumba yangu, nikajaribu kulisukuma lakini likawa gumu. Kwa kuwa kulikuwa na swichi ya kengele wala sikuhangaika. Nilipeleka mkono wangu panapo swichi, nikabofya kistaarabu kisha nikakaa pembeni kusubiri majibu.
            Punde si punde geti lilifunguliwa. Akatokea jamaa mmoja akiwa kifua wazi.
“Karibu!” Alisikika jamaa huyo akiniambia.
“Asante! Habari yako kaka?”
“Nzuri! Sijui nikusaidie nini?” Alihoji swali hilo ambalo lilinifanya nimshangae.
            ‘Hivi huyu hajui ya kuwa mimi ndiyo mwenye nyumba hii? Au anavyoniona nimekondeana namna hii basi anajua kuwa mimi ni kapuku?’ Niliwaza huku nikiwa ninamwangali jamaa huyo pasipo kummaliza. .
            “Ndugu, sema shida yako nina mambo kibao ya kufanya huko ndani, ila kama unakuja kupiga kibomu kwa mheshimiwa kasafiri, tena hayupo kabisa ndani ya nchi hii.” Alizidi kueleza jamaa huyo.
            Maelezo hayo yalinishtua na kunifanya nianze kupatwa na wasi wasi fulani. Niliyekuwa nimemkabidhi nyumba pamoja na miradi yangu yote alikuwa ni kijana tu kama mimi. Sasa nilizidi kuumiza kichwa uheshimiwa umetoka wapi kwa kijana kama huyo!

AISEEEH, KWA BRIGHTON SASA PANAITWA KWA MHESHIMIWA, HUYO MHESHIMIWA NI NANI? PIA SHARIFA KAPOTELEA WAPI? JE, NA MAISHA YA BRIGHTON YATAKUWAJE BAADA YA KUTOKA JELA? USIKOSE TOLEO LIJALO!

Friday, November 22, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 45

KWA WASOMAJI WAPYA.....
            Brighton anaota ndoto ya ajabu akiwaona watu waliokufa siku nyingi kwa kujiua wakiwemo mzee Mboma, Patrick, James na Anna. Baada ya ndoto hiyo anazongwa na mwanadada Sharifa anayemsababishia kesi ya mauaji ya mpangaji wake, yaani Kishoka. Kesi inaunguruma mahakamani kisha anajikuta akihukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe kwa kosa la mauaji ya Kishoka, kosa ambalo alikuwa hajalitenda. Akiwa gerezani akisubiri tarehe za kunyongwa anakutana na Mack, jamaa aliyekuwa amenunua nyumba iliyokuwa ya marehemu James, naye Mack anaanza kumhadithia kisa kilichompelekea afungwe jela.
Kwa kusimuliwa na Mack, Brighton anayasikia mengi kuhusu mali alizokuwa amerithi kutoka kwa marehemu kaka yake kwa kila aliyekuwa amemuuzia aliishia kupatwa na matatizo akiwemo Mack mwenyewe. Hatima siku ya kunyongwa inafika kweli, anaambiwa akafanyishwe maungamo kwa mtumishi wa Mungu. Je, atanyongwa kweli? Sasa endelea...................

            Mara baada ya kuketi mwanamke huyo aliinua kichwa chake, mbona nilizidi kuchoka! Niliweza kumtambua barabara. Huwezi amini ndugu msomaji mwanamke huyo alikuwa ni Sharifa, mwanadada aliyenisingizia kuwa nimeua kisha akaonyesha ushahidi wa picha na kunifanya nihukuniwe kunyongwa.
            Baada ya kumuona hasira zilinijaa ghafla, nikasema potelea pote lolote na liwe, hakuna cha maungamo wala nini. Moyo wa kulipa kisasi ulinijaa mtoto wa kiume, nikatamani nimraruwe mle mle kwenye chumba hicho ili hata kama ninanyongwa na yeye awe ameshakufa.
            Hata hivyo nilipiga moyo konde na kujishauri nitulize munkari na kuzizuia papara zangu ili nimsikilize ananiambia nini.
            Aliniangalia kisha akaachia bonge la tabasamu. Hapo ndiyo niliweza kuuona uzuri wake ulivyokuwa wa shani, mtoto masharah alikuwa kamili kila idara.
            Hata hivyo sikutishika na tabasamu lake hilo kwani nilijua wazi kuwa tabasamu hilo lilikuwa ni la kinafiki. Nikazidi “kumlia buyu” nikisubiri aanzishe yeye mjadala.
Alikuwa katupia suti ya kike rangi nyeusi huku macho yake yakipendezeshwa na miwani midogo iliyokuwa imemkaa kisawasawa.
“Sharifa, leo hii wewe ndiyo mtumishi wa Mungu?” Niliamua kumuuliza bila woga baada ya ukimya mrefu kidogo kutawala.
“Tulia Brighton na unisikilize kwa makini.” Sauti nyororo ya msichana huyo ilipenya kupitia kwenye ngoma za masikio yangu, sauti ambayo ilinikumbusha ufukweni siku niliyoanza kabisa kukutana naye.
            “Hivi unajua ni kwa nini matatizo yote hayo yamekuaandama?” Alinihoji huku nami nikiwa makini kumsikiliza.
“Sijui labda uniambie wewe kwa maana umeonekana kuyasakama sana maisha yangu.” Nilijibu kwa mkato na kukaa kimya.
“Chanzo cha matatizo hayo yote ni mirathi ya kaka yako James.”
“Mirathi ya kaka yangu James! Imefanya nini?”
“Ujio wangu siyo kuja kujadili chanzo cha matatizo yako, ila nilikuwa nakutaarifu tu ili ukae unajua.”
“Kwa hiyo umekuja kufanya nini?” Nilizidi kumtwanga maswali bila woga wowote.
            “Lengo la mimi kuwa hapa ni kuja kukuokoa na adhadu ya kunyongwa kama utakuwa tayari kutekeleza masharti nitakayokuambia.”
“Masharti yapi hayo?” Nilihohoji huku hisia za wokovu wa chupuchupu nikizitazamia.
            Hata hivyo kazi ilikuwa kwenye hayo masharti. Ingawa alikuwa hajaniambia ila nilihisi yangekuwa magumu mno.
“Huhitaji kuyajua kwa sasa hayo masharti, kama upo tayari nikuokoe sema.” Aliongea Sharifa na kuzidi kuniweka katika wakati mgumu.
            Akili yangu ilikuwa ikizunguka kama korona kwa wakati huo huku nikiwaza na kuwazua ni uamuzi gani nichukue, lipi nishike na lipi niache.
            Kibaya zaidi nilikuwa sijaambiwa masharti nitakayopewa, hapo ndiyo nilizidi kuchanganyikiwa. Kuendelea kuishi nako nilikuwa bado nakutamani, isitoshe kufa kwa kunyongwa nako kulikuwa kukinitisha.
            ‘Hii ni bahati ya mtende nisiiachie Brighton mimi. Hayo masharti nitahangaika nayo mbele kwa mbele, kikubwa ni kwamba niwe nimeokoka na adhabu ya kunyongwa. Yakienda kunishinda si nakataa tu, atanifanya nini wakati gerezani tayari kashanitoa?’ Niliwaza kimoyomoyo huku nikionekana kuukubali msaada wa Sharifa.
            Nilitulia kidogo kama nawaza kitu fulani kwa kina, ghafla niligutushwa na sauti ya Sharifa iliyokuwa ikiniambia nifanye maamuzi yangu haraka kwani nilikuwa namchelewesha.
            “Sawa nimekubali niokoe” Nilijikuta najiropokea tu wala nilikuwa sijakamilisha sawasawa.
            Baada ya kuongea hivyo nilimuona Sharifa akitoa tena tabasamu lake la ukweli, tambasamu ambalo nilikuwa nikilifurahia kila alipolitoa. Aliinuka kwenye kiti alichokuwa amekaa kisha kitabu alichokuwa nacho mkononi akakitumbukiza kwenye mkoba wake aliokuwa nao. Akaja upande niliokuwa nimekaa, akaniambia nami niinuke. Nilipoinuka akanishika mkono na kuniambia tuondoke zetu.

HEHEEEH! MAKUBWA.MIRATHI YA JAMES INAMSABABISHIAJE MATATIZO BRIGHTON? PIA WATAFANIKIWA KWELI KUTOKA KWENYE NGOME YA MAGEREZA? NA KAMA WAKITOKA NI MASHARTI YAPI SHARIFA ATAMPA BRIGHTON? USIKOSE TOLEO LIJALO.

Thursday, November 21, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 44

KWA WASOMAJI WAPYA.....
            Brighton anaota ndoto ya ajabu akiwaona watu waliokufa siku nyingi kwa kujiua wakiwemo mzee Mboma, Patrick, James na Anna. Baada ya ndoto hiyo anazongwa na mwanadada Sharifa anayemsababishia kesi ya mauaji ya mpangaji wake, yaani Kishoka. Kesi inaunguruma mahakamani kisha anajikuta akihukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe kwa kosa la mauaji ya Kishoka, kosa ambalo alikuwa hajalitenda. Akiwa gerezani akisubiri tarehe za kunyongwa anakutana na Mack, jamaa aliyekuwa amenunua nyumba iliyokuwa ya marehemu James, naye Mack anaanza kumhadithia kisa kilichompelekea afungwe jela.
Kwa kusimuliwa na Mack, Brighton anayasikia mengi kuhusu mali alizokuwa amerithi kutoka kwa marehemu kaka yake kwa kila aliyekuwa amemuuzia aliishia kupatwa na matatizo akiwemo Mack mwenyewe.  sasa endelea...................

             Suala la kuandika barua kwa rais ndiyo lilikuwa limetawala katika kichwa changu. Hiyo ndiyo fursa pekeee iliyokuwa imebakia ya kujaribu kujitetea, si unajua tena mfa maji haishi kutapatapa.
            Rais anao uwezo wa kumsamehe mfungwa wa mauaji endapo ataandika barua kuelezea ambavyo haki haikutendeka katika hukumu yake kwa mujibu wa sheria za nchi yetu naye akajiridhisha na sababu hizo.
            Wazo hilo alinipa Mack, akaniambia unaweza ukamwandikia barua rais na kumweleza jinsi mazingira ya kesi yako yalivyokuwa. Kama akiridhika na maelezo yako anaweza akakuachia ukawa huru.
            Wazo hilo nililiafiki na kulipokea kwa mikono miwili. Nikaandika barua na kuikabidhi kwa mhusika gerezani hapo ambaye alifanya harakati za kuipeleka kwa mheshimiwa rais. Nilijipa matumaini kuwa huenda mheshimiwa ataridhika na malalamiko yangu na kuniachia huru.
            Siku zilizidi kukatika bila kupata majibu yoyote. Miaka kadhaa ilipita nikiwa gerezani kusubiri siku za adhabu yangu ya kunyongwa. Ilibidi nikubaliane na hali halisi ya kwamba kifo changu kitakuwa cha kupigwa kitanzi.
            Hayawi hayawi hatimaye yalikuwa. Siku moja nikiwa sina hili wala lile niliitwa na kuambiwa masaa yangu yalikuwa yanahesabika. Yaani namaanisha siku yangu ya kupigwa kitanzi ilikuwa ndiyo hiyo.
            Nilipelekwa kwenye chumba kimoja ambako niliambiwa nitakutana na mtumishi wa Mungu ili anihubiri na kuniombea pia. Kama ningetaka kutubu dhambi zangu huo ndiyo ulikuwa ni muda muafaka.
Nilijikuta mwili ukinyong’onyea ghafla kwa hofu ya kifo. Usiombe kuijua siku na saa unayokufa.
            Wakati naukanyaga mlango wa chumba hicho nilimuona mwanamke aliyekuwa kainama chini akisomasoma kitabu. Niliambiwa huyo ndiye mtumishi wa Mungu na nilipewa masaa kadhaa ya kuongea naye kabla sijapelekwa kwenye chumba cha kunyongea.
            Mwanamke huyo alionekana kuwa bado yungali msichana. Hata hivyo mpaka nakaa nilikuwa bado sijaiona sura yake kutokana na sababu kuu mbili; sababu ya kwanza ni kutokana na yeye kuwa ‘busy’ na kusoma kitabu na sababu ya pili ni kutokana na machozi kunifumba macho kwani nilikuwa nikilia kilio cha kimya kimya. Hicho huitwa kilio cha ng’ombe; kilio cha kutoa machozi bila ya kutoa sauti.

HAYA SASA, HAYAWI HAYAWI MWISHO YAMEKUWA, KWELI  BRIGHTON ATANYONGWA? USIKOSE TOLEO LIJALO! 

Tuesday, November 19, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 43

KWA WASOMAJI WAPYA.....
            Brighton anaota ndoto ya ajabu akiwaona watu waliokufa siku nyingi kwa kujiua wakiwemo mzee Mboma, Patrick, James na Anna. Baada ya ndoto hiyo anazongwa na mwanadada Sharifa anayemsababishia kesi ya mauaji ya mpangaji wake, yaani Kishoka. Kesi inaunguruma mahakamani kisha anajikuta akihukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe kwa kosa la mauaji ya Kishoka, kosa ambalo alikuwa hajalitenda. Akiwa gerezani akisubiri tarehe za kunyongwa anakutana na Mack, jamaa aliyekuwa amenunua nyumba iliyokuwa ya marehemu James, naye Mack anaanza kumhadithia kisa kilichompelekea afungwe jela.
Kwa kusimuliwa na Mack, Brighton anayasikia mengi kuhusu mali alizokuwa amerithi kutoka kwa marehemu kaka yake kwa kila aliyekuwa amemuuzia aliishia kupatwa na matatizo akiwemo Mack mwenyewe.  sasa endelea...................

Alipopandishwa kizimbani kwa mara ya kwanza alisomewa mashtaka kisha akatakiwa kutojibu chochote kwani mahakama hiyo ilikuwa haina uwezo wa kusikiliza kesi kama hiyo, yaani kesi ya mauaji.
Aliendelea kukaa rumande wakati taratibu za upelelezi wa kesi yake zikiwa bado hazijakamilika. Jalada lake lilipokamilika kesi yake ilihamishiwa kwenye mahaka kuu.
Kesi iliendelea kurindima. Kitu kilichomuacha hoi Mack ni yule shahidi namba moja wa kesi hiyo ambaye alijitambulisha kuwa ni mume  wake na Sada, yaani mwanadada aliyekuwa ameuawa.
Mack alishangaa kumuona shahidi huyo ndiye jamaa aliyekuwa ameuliwa na kaka James kwa kupigwa risasi baada ya kumkuta na Neila ambaye alikuwa ni mpenzi wake (yaani kaka James). Kijasho chembamba kilianza kumtoka.
Jamaa alitoa ushahidi wake akidai kuwa siku ya tukio alikuwepo na alimshuhudia Mack wakati anafanya mauaji.
Kilichozidi kumchanganya Mack na ndiyo hicho hicho kilichokuwa kinazifanya kesi zetu ziwe mapacha ni ushahidi wa ule mkanda uliorekodiwa na kamera maalum za nyumba hiyo ukionyesha mwanzo mpaka mwisho wa tukio.
Mack hakuua. Tena maskini wa Mungu alikuwa haijui hata hiyo nyumba aliyokuwa akiishi mwanamke huyo. Ni sawa kweli alikuwa na wenyeji kidogo kwenye mtaa wa Matopeni, lakini alipokuwa akikaa Sada alikuwa hapajui na ndiyo maana alichemsha kumpata siku alipoenda kumtafuta.
Yale yale kama yaliyotokea kwangu, kuonekana alama za vidole vyangu kwenye mwili wa Kishoka na kwenye kisu wakati sikuwahi hata kuvigusa. Tena hiyo ni tisa, kumi kuonekana picha zangu kwenye kamera nikimchinja Kishoka wakati sikuhusika abadani!
Mwisho wa siku Mack alihukumiwa kunyongwa mpaka afe kwa kosa la kumuua Sada kwa kukusudia. Hivyo ndivyo stori ilivyoenda kwa mujibu wa maelezo yake.
Nilivuta pumzi ndeefu kisha nikaishusha baada ya kumaliza kusimuliwa simulizi hiyo na Mack mwenyewe.
“Mbona kama kuna zengwe fulani hivi kwenye mirathi ya kaka James? Maana mambo yanayotokea siyaelewielewi!” Nilitamka maneno hayo nikimwambia Mack.
“Na hayo matatizo siyo kwetu sisi peke yetu tu, takribani watu wote uliowauzia mali za huyo marehemu kaka yako wamepatwa na matatizo!” Alisikika Mack na kuzidi kunipa mpasuko wa moyo.
            Sasa moyo wangu haukuwa na amani tena. Niliishiwa nguvu mithili ya mtu anapoletewa msiba wa mtu ampendaye kwa dhati. Hata hivyo hamu ya kutaka kujua kilichojiri kwa wateja wangu hao ilizidi kunifukuta.
            “Mungu wangu! Ni matatizo gani yaliyowapata?” Nilijikuta nikiuliza kwa mshangao mkubwa.
“Yule jamaa uliyemuuzia ile kampuni ya usafirishaji hayupo tena duniani.”
“Wewe! Kunesa alishafariki? Ilikuwaje?” Nilijikuta nikizidi kuchanganyikiwa huku nikiuliza maswali dabodabo.
            Mack alianza kunieleza yaliyojiri huko moja baada ya jingine. Alianza na habari za huyo Kunesa, jamaa niliyekuwa nimemuuzia kampuni ya usafirishaji niliyokuwa nimerithi kutoka kwa kaka yangu.
            Alinieleza jinsi kifo cha Kunesa kilivyokuwa. Japokuwa hata yeye hakuwepo huko wakati kifo hicho kinatokea ila alisimuliwa na baadhi ya ndugu na jamaa zake waliokuwa wakienda kumuona pale gerezani.
            Alieleza kuwa Kunesa alikutwa kafa kwenye ofisi yake. Alikuwa kachinjwa huku kichwa kikiwa mbali na kiwiliwili chake. Aliyefanya tukio hilo hajajulikana mpaka wa leo.
            Nilipouliza watu wengine waliokumbwa na matatizo nikaambiwa ni wale jamaa waliokuwa wameyanunua yale magari. Waliyakuta magari yanawaka moto yenyewe kwa nyakati tofauti na chanzo cha moto huo wala hakikujulikana. Habari hizo zilizidi kunipa wasiwasi mkubwa juu ya mali za kaka James. Nikazida kujiuliza kulikoni kuhusu hizo mali.
            Walionunua maduka walifilisika wote, maduka yaliisha na kubakia matupu kabisa. Nilianza kuwaza endapo watu hao wangeamua kunitafuta sijui wangenifanya nini!
            “Na wewe umefikaje kwenye gereza hili wakati hata huko mahakama kuu ipo pamoja na magereza ya kutosha kabisa.” Niliona nimuulize Mack swali hilo lililokuwa linanitatiza tangu nilipomuona tu.
“Afya yangu ilianza kuwa mgogoro mara baada ya kufungwa. Ndipo daktari wa hospitali ya gereza hilo akashauri kwamba nihamishiwe gereza jingine akidai kuwa hali ya hewa ya pale ilikuwa imenikataa. Ndipo nilipoletwa huku.”
            Kwa kweli zilikuwa ni habari nzito za kutisha na kusikitisha. Nilianza kujiona kuwa ni muuaji kwani mtu kama Kunesa nilihisi kuwa nina mchango mkubwa mno juu ya kifo chake, ukizingatia nilimbembeleza kuinunua hiyo kampuni baada ya kukosa mtu wa kuinunua.
            Hiyo ilikuwa ni siku ya kwanza kukutana na Mack, siku ambayo ndiyo kwanza nilikuwa nimetoka mahakamani kuhukumiwa.

                        ***************************

DUH! HIZO MALI ZA URITHI WA BRIGHTON KUTOKA KWA KAKA YAKE ZINA NINI? MBONA KILA ALIYEZINUNUA ANAPATA MATATIZO? USIACHE KUFUATILIA SIKU SI NYINGI UTALIPATA JIBU!

Sunday, November 17, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 42

KWA WASOMAJI WAPYA.....
            Brighton anaota ndoto ya ajabu akiwaona watu waliokufa siku nyingi kwa kujiua wakiwemo mzee Mboma, Patrick, James na Anna. Baada ya ndoto hiyo anazongwa na mwanadada Sharifa anayemsababishia kesi ya mauaji ya mpangaji wake, yaani Kishoka. Kesi inaunguruma mahakamani kisha anajikuta akihukumiwa adhabu ya kunyongwa mpaka afe kwa kosa la mauaji ya Kishoka, kosa ambalo alikuwa hajalitenda. Akiwa gerezani akisubiri tarehe za kunyongwa anakutana na Mack, jamaa aliyekuwa amenunua nyumba iliyokuwa ya marehemu James, naye Mack anaanza kumhadithia kisa kilichompelekea afungwe jela, sasa endelea...................

            Pale pale nikajishauri kuwa nimkatishe Mack kwa kumuuliza swali tena kwani kuuliza ilikuwa siyo dhambi na nilikuwa sijakatazwa. Ndipo nilipomuuliza kuwa msichana huyo alijitambulisha kwa jina gani.
            “Alisema kuwa anaitwa Sada, mwenyeji na mzaliwa wa Matopeni ila wazazi wake walikuwa wameshafariki kwa kipindi hicho.” Hilo ndilo lilikuwa jibu la Mack kwa swali nililokuwa nimemuuliza, jibu ambalo lilianza kunitoa katika hisia zangu juu ya msichana huyo.
            “Alikuwa yukoje yukoje kimuonekano?” Nilizidi kudodosa nikidhani ya kuwa huenda alikuwa kabadilisha tu majina.
“Alikuwa ni mwembamba halafu kaenda hewani kimtindo, mweupe na mwenye mwanya. Akiwa anaongea sauti yake ilikuwa nzito kiana.” Alidadavua Mack.
Jibu hilo pekee lilitosha kuitengua hoja iliyokuwa imejengeka akilini mwangu ya kwamba mwanamke huyo alikuwa ndiyo Sharifa. Nilimuacha Mack aendelee kunipa michapo labda kwa baadaye ningeweza kung’amua kitu kuhusu mwanadada huyo.
Aliendelea kunielezea. Akasema kuwa baada ya siku mbili kupita mwanamke huyo alijileta mwenyewe kwa Mack akija kumwambia anampa onyo la mwisho, kama hatahama vitendo vingefuata.
Mack alitaka sana kuumaliza mgogoro huo kwa njia ya amani akiamini kabisa kuwa yote yanawezekana kwa nguvu ya hoja. Alimsihi mwanadada huyo waende kwenye ofisi za serikali ya mtaa ili wakaliongelee shauri hilo.
Hata hivyo mwanamke huyo alimjibu kwa nyodo nyingi akisema kuwa hana muda mchafu wa kwenda kuonana na hao viongozi wa serikali za mtaa. Siyo muda peke yake, hata hadhi yake ilikuwa siyo ya kwenda kuvimbisha tumbo lake mbele ya watu kama hao aliowaita majuha.
Mack aliyapeleka majibu hayo kwa hao viongozi, nao wakamwambia ya kuwa asubiri hatua atakayochukua mwanamke huyo huku wakiahidi kuwa mstari wa mbele kumtetea.
Wiki moja baada ya hapo kioja kilitokea nyumbani kwa Mack. Wakati anatoka kwenye mihangaiko yake ya kila siku, alikutana na askari polisi waliokuwa wakimsaka kwa udi na uvumba. Walipompata walimweka chini ya ulinzi wakimwambia ametoka kuua mtaa wa Matopeni.
Alishangaa sana kusikia hivyo, akawaambia kuwa yeye hajaua. Wakamwambia kuwa ameua kwani nyumba aliyokuwa ameenda kufanya tukio hilo ilikuwa na kamera maalum za kunasa wezi na wahalifu mbalimbali.
Alipouliza kamuua nani akaambiwa kuwa kamuua mwanadada mmoja aliyekuwa akijulikana kwa jina la Sada, mwanamke aliyekuwa akiishi katika mtaa wa Matopeni.
Mack aliendelea kubisha. Askari hao wakaanza kupekua kwenye gari lake. Katika pekua pekua waliona bastola ndani ya gari la lake, kitu ambacho kilikuwa ni kigeni kabisa kwake.
Kiukweli alikuwa hana bastola na alikuwa hajawahi kumiliki siraha kama hiyo katika maisha yake, hata kule kuishika masikini wa Mungu alikuwa hajawahi. Cha ajabu sasa ilipatikana, tena ndani ya gari lake. Alizidi kuchanganyikiwa.
Askari waliendelea kueleza kuwa kwenye kamera hizo Mack alianza kuonekana tangu anafika kwenye nyumba ya Sada na zilikuwa zimerekodi tukio zima.
Kati ya askari waliokuwa wamemkamata mmoja alikuwa akimfahamu, hivyo baada ya kuiona picha yake kwenye kamera hizo akawa amemtambua.
Habari hiyo ilikuwa ni ngeni kabisa kwa Mack. Aliwaeleza askari hao kuwa yeye hakuua ingawaje kweli alikuwa katika mgogoro wa nyumba na huyo Sada. Alizidi kujitetea kuwa hata nyumbani kwake (yaani kwa Sada) alikuwa hapafahamu kwani siku moja alienda kumtafuta ili waende kwenye ofisi za serikali ya mtaa kuuongelea mgogoro wao lakini hakufanikiwa kumpata msichana huyo.
Pamoja na kujitetea kote huko, Mack aliambulia kuwekwa chini ya ulinzi na kupelekwa kwenye kituo cha polisi cha kati. Alikaa hapo kwa siku moja na nusu kisha jalada la kesi yake likapelekwa kwenye mahakama ya hakimu mkazi.

DAH! MAUZAUZA YANAHAMIA KWA MACK. HUYO SADA NI NANI NA ANAUHUSIANO WOWOTE NA SHARIFA ALIYEKUWA AKIMSUMBUA BRIGHTON? USICHOKE KUFUATLIA MWISHO WA SIKU MAJIBU YOTE UTAYAPATA. 

Friday, November 8, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 41


ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA...
Nilizidi kuchanganyikiwa kwa kuona maisha yangu yakiandamwa na mikasa, mikosi na ndege mbaya kila wakati. Kichwa kilizidi kuuma.
SASA ENDELEA.......
Maisha ya gerezani yalizidi kusonga huku nikiwa nasubiri siku yangu ya kutundikwa kwenye kitanzi ifike, siku ambayo nilikuwa sijui tarehe yake, mwezi wala mwaka wake.
Huko gerezani nilishangaa sana kumkuta jamaa mmoja ambaye nilikuwa namfahamu. Jamaa huyo ni yule niliyekuwa nimemuuzia nyumba aliyokuwa kahongwa Neila, mwanamke aliyeuliwa na James baada ya kumuonyeshea utapeli wa mapenzi na nyodo za kila aina.
Nilishangaa sana kumkuta jamaa huyo aliyekuwa anajulikana kwa jina la Mack. Alikuwa kakaa gerezani kwa muda mrefu kiasi kwani alikuwa kashapewa mpaka unyapara wa humo gerezani.
“Kulikoni tena ndugu yangu na wewe umeletwa huku?” Lilikuwa ni swali la Mack siku ya kwanza kabisa kuingia jela mara baada ya kuniona.
“Matatizo makubwa ndugu yangu, hapa nilipo sina hata hamu! Na wewe lini tena humu na kipi kilichopelekea kuletwa sehemu hii isiyofaa?” nilimuuliza nikiwa na shauku kubwa ya kujua kilichokuwa kimemsibu.
Kabla ya kunijibu aliguna kisha akavuta pumzi ndefu na kisha  kuzishusha.
“Ni stori ndefu mdogo wangu, hebu anza kwanza wewe kunieleza mkasa uliokusibu mpaka ukaletwa humu.”
Niliamua kuanza kumsimulia jinsi mambo yalivyokuwa. Nikamweleza kinaga ubaga, hatua kwa hatua tangu kipindi nahama mji tuliokuwa tunaishi na kaka James.
Wakati namsimulia alikuwa katulia tulii huku akinisikiliza kwa umakini mkubwa. Nilipomaliza nikamuachia naye aweze kufunguka. Alianza kwa kusema,
“Kisanga chako hakina tofauti sana na kile kilichonitokea mimi.” Alitulia kidogo kumeza mate.
            Nilishtuka sana baada ya kusikia hivyo. Nikawa na hamu ya kusikia mambo yalivyokuwa huko. Aliendelea kuniambia kuwa mara baada ya kumuuzia nyumba ile alihamia. Akawa anaishi pale yeye na familia yake ambayo ilikuwa na jumla ya watu watatu, yaani yeye mwenyewe, mke wake na mtoto wake mmoja.
            Kabla hajamaliza hata mwezi kuna msichana alijitokeza na kumtaka ahame pale akidai kuwa nyumba ile ni yake. Baada ya kuambiwa hivyo hakutishika kwani ushahidi wote wa kuonyesha kuwa nyumba ile ni mali yake ya halali alikuwa nao.
            Mwanadada huyo alizidi kumwandama kwa kumtisha na vitisho kedekede. Pamoja na vitisho hivyo Mack aliendelea kukaidi madai ya mwanadada huyo.
            “Huyo msichana ulikuwa unamfahamu kabla?” Nilimtwanga swali hilo nikiwa najaribu kudadisi juu ya msichana huyo.
“Hapana! Nilikuwa sijawahi hata kumuona kabla ya hapo.” Mack alinijibu kama hivyo.
“Alisema yeye ni mwenyeji wa wapi?” Niliuliza tena.
“Alidai kuwa ni mwenyeji wa palepale mjini mtaa wa Matopeni. Lakini mimi niliona ni muongo kwani Matopeni nilikuwa mwenyeji kidogo na nilikuwa sijawahi kuona sura kama yake.”
            Niliona niachane na kuuliza uliza maswali kwani yalikuwa yanakatisha uhondo wa stori yenyewe. Nikamuacha Mack aendelee kunipa michapo hatua kwa hatua.
Aliendelea kueleza kuwa baada ya kukaidi mwanamke huyo hakuchoka kumghasi akimwambia ahame katika nyumba ile.
Baada ya Mack kuona kero imezidi aliamua kulipeleka shauri hilo kwenye uongozi wa serikali za mtaa ili wamsaidie kuipata suluhu. Alipowaeleza viongozi hao walimwambia aende na mlalamikaji huyo ili wakapate kuyasikiliza malalamiko yake.
“Nikaenda kumtafuta mtaa wa Matopeni lakini sikufanikiwa kumuona. Kila niliyemuuliza alisema hamfahamu.” Alisikika Mack akiniambia.
Sikutaka kutia swali katika maelezo yake, nikachombeza tu kwa kumwambia aendelee, naye akaendelea.
“Baada ya kumkosa nilirudi nyumbani. Nikaamua kumsubiri atakapokuja nimkamatishe na kumpeleka kwenye ofisi za serikani za mtaa.”
            Huku nikimsikiliza lakini kwenye ubongo wangu kulikuwa na mjadala mzito uliokuwa ukiendelea. Suala la kulifahamu jina la msichana huyo ndiyo lilikuwa nimetawala kwenye akili yangu. Mawazo yangu yote yalikuwa yananituma kuwa piga ua galagaza yule msichana alikuwa ni Sharifa, msichana aliyenisababishia matatizo ya kupatikana na hatia ya kuua wakati sijaua.

JE, MSICHANA HUYO NI NANI NA KWA NINI ANAMSUMBUA MACK? USIKOSE TOLEO LIJALO.

Wednesday, November 6, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 40

ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA...
Kumbe kulikuwa na mipango kabambe ya kumwingiza kipenzi changu kwenye jaribu zito lililokuja kupelekea kifo chake.
SASA ENDELEA.......

Kuna kijana mmoja ambaye alikuwa akimtaka Anna kimapenzi siku nyingi lakini ikashindikana. Kwenye hicho kisherehe naye alikuwepo.
Baada ya kumuona Anna kijana kijana huyo akasema kuwa lazima lengo lake litimie, ndipo alipomchanganyia dawa za kulewesha kwenye soda na hatimaye akalewa na akawa hajielewi.
Baada ya kufanya hivyo kijana huyo alijichukulia mzigo kiulaini na kwenda kuutumia jinsi alivyotaka. Lengo lake lilikuwa ni kufanya mapenzi na Anna, kweli alifanikiwa japokuwa Anna alikuwa hajitambui.
Tukio hilo lilimuumiza sana kipenzi changu. Hata hivyo wakati huo mimi nilikuwa masomoni hivyo hakuweza hata kupata faraja kutoka kwangu. Miezi miwili baadaye tulifunga shule. Ndipo niliporudi nyumbani na kukuta habari za kubakwa kwa Anna ambazo ziliurarua moyo wangu.
Tunu ya usichana wa Anna ambayo alikuwa ameitunza kwa ajali yangu ilikuwa tayari imeshahujumiwa. Hakuwa bikira tena. Iliniuma sana kusikia hivyo. Hata hivyo sikutaka kuukatisha uhusiano wetu kwa sababu ya hilo, nilimwambia kuwa tutakuwa pamoja licha ya kwamba tunu yangu ilikuwa imeshahujumiwa.
Ndipo nilipomshauri aende kuangalia afya yake huenda siku hiyo alipata maambukizi ya virusi vya UKIMWI. Naye bila ubishi alienda, hata hivyo majibu yalikuwa safi.
Siku kadhaa zilipita. Nikiwa sijui hili wala lile nilipokea taarifa za kifo cha Anna, taarifa ambazo zilizidi kuuchoma moyo wangu.
Taarifa hizo zilisema kwamba Anna alikuwa amekufa baada ya kufanya jaribio la kutoa mimba. Niliposikia hivyo nilijua moja kwa moja mimba hiyo iliingia siku ile alipobakwa na yule kijana.
Ndipo nilipozidi kuumia na kujihisi mpweke zaidi ya kinda lililoachwa na mama likabaki peke yake kwenye kiota. Huo ndiyo ulikuwa mwisho wa maisha ya Anna kwa hapa duniani ingawa mpaka leo moyoni mwangu yu hai.
Tukio hilo liliniacha na kidonda kikubwa sana ndani ya moyo wangu. Mpaka nakuja kuondokewa na kaka yangu kidonda hicho kilikuwa hakijapata hata dalili za kupona, kikawa kimegongomewa msumari mwingine tena mkubwa zaidi.
Aliyekuwa mstari wa mbele kunifariji juu ya machungu ya kuondokewa na Anna naye alinitoka, tena kwa kifo cha ghafla ghafla huku nikimshuhudia wakati roho inaachana na mwili wake. Hakika lilikuwa ni pigo mjaarabu.
Huku nikiwa na majonzi yangu tele moyoni niliendelea kulisongesha huku nikipata faraja kutoka kwa majirani na rafiki zangu wa karibu, faraja ambayo hata haikukidhi mahitaji ya upweke uliokuwepo ndani ya moyo wangu.
Kitu kingine ambacho kilianza kuniacha hoi ni hizo mali zilizokuwa zimeachwa na kaka James. Nilizidi kuchanganyikiwa kwa jinsi zilivyokuwa zikipukutika na kuisha bila kuelewa zinaishaje.
Biashara zote zikawa haziendi. Nikienda kwenye maduka mauzo yalikuwa mabovu, kampuni ya usafirishaji nayo ikazidi kufilisika siku hadi siku. Ajali za mara kwa mara zikawa zinatokea kwenye malori ya kusafirisha mizigo kwanye kampuni hiyo. Nilizidi kuchoka.      
Baada ya kuona mambo yanazidi kwenda kombo niliamua kuanza kupiga bei mali moja baada ya nyingine. Nilianzia kuuza nyumba aliyokuwa kahongwa Neila, mwanamke aliyepigwa risasi na kaka James.
Mara baada ya kuiuza nyumba hiyo, niliyatangazia dau magari mawili ya kifahari yaliyokuwa yameachwa na kaka James. Gari moja ni lile alilohongwa Neila; mwanamke aliyekuwa akijidai ana mapenzi ya kweli kwa kaka James kumbe hamna chochote. Mwanamke ambaye alisababisha kifo cha kaka yangu huyo.
Gari la pili ni lile alilokuwa akitumia kaka James. Yote yalikuwa ni magari ya kifahari. Nilibakiza gari moja ambalo nilikuwa nalitumia mimi. Hilo sikutaka kuliuza.
Ndani ya miezi sita nilikuwa nimeshauza kila kitu; maduka, nyumba pamoja na kampuni ya usafirishaji. Lengo langu lilikuwa ni kuhama kabisa mji huo.
  Nilipomaliza michakato yote nilihama mji huo na kuhamia mji mwingine ambako nilienda kununua nyumba na kuendelea na maisha kama kawaida. Nilianza kufanya biashara zangu huko.
Nyumba hiyo ilikuwa kubwa mno kukaa peke yangu kwani nilikuwa bado nahisi upweke kutokana na kuondokewa na nguzo yangu muhimu katika dunia hii.
Ndipo nilipoamua kukipangisha chumba kimoja na mpangaji aliyekuja kupanga alikuwa ni marehemu Kishoka. Alikuwa ni kijana mstaarabu sana ambaye hakuwa na makuu.
Maisha yetu yalizidi kuwa ya furaha kadri siku zilivyozidi kusonga. Tukawa tunaishi kama ndugu wa damu ilhali tulikuwa tumekutana ukubwani tu kila mmoja akiwa na meno thelethini na mbili.
Kiumri tulikuwa hatupishani sana japokuwa alikuwa ananizidi miaka mitatu. Nilipomuita kaka naye aliniita kaka. Pamoja na kunizidi umri lakini na mimi nilikuwa mwenye nyumba wake.
Ilifikia wakati nikamwambia asiwe ananilipa kodi ya nyumba kwani urafiki wetu ulikuwa umefikia hatua nyingine. Akawa anaishi bila kulipa kodi ya pango siku zote.
Mpaka matatizo ya kifo chake yanatokea tulikuwa tunaishi naye kama ndugu, kifo ambacho kilikuja kikanigharimu hukumu ya kunyongwa nikisingiziwa kuwa mimi ndiye niliyemchinja.
Nilizidi kuchanganyikiwa kwa kuona maisha yangu yakiandamwa na mikasa, mikosi na ndege mbaya kila wakati. Kichwa kilizidi kuuma.

                        ********************
ITAENDELEA.....


Monday, November 4, 2013

MIRATHI YA KAKA sehemu ya 39

ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA...
Watu walizidi kumiminika kuja kunipa faraja kwenye msiba huo. James alikuwa ni mtu wa watu, alijua kukaa vizuri na majirani pamoja na watu wengine aliokuwa akifahamiana nao. Hali ya watu kujaa ilinifariji kwa kiasi fulani ingawaje moyo wangu ulikuwa umeghubikwa na majonzi yasiyokuwa kifani.

            ******************************
SASA ENDELEA.......
Pamoja na kwamba ni miezi kadhaa ilikuwa imepita tangu kifo cha kaka James kutokea, akili yangu ilikuwa haijachanganya kabisa. Kila nilichokuwa najaribu kukifanya nilikiona hakifai.
Kifo hicho kilikuwa kimetonesha donda jingine kwenye mtima wangu ambalo lilikuwa bado halijapona. Donda hilo nilikuwa nalifananisha na donda ndugu kwani lilikuwa limechukua muda mrefu sana bila kupona ndani ya moyo wangu.
Usiombe kupata majeraha palipo na donda ndugu mpenzi msomaji. Hebu fikiria maumivu yake yatakavyokuwa. Ni zaidi ya uchungu!
Donda lililotoneshwa na kifo cha kaka James ni lile lililokuwa limeachwa na kipenzi cha roho yangu marehemu Anna pamoja na wazazi wangu, hasa hasa kile cha Anna.
Kuondoka kwa Anna katika dunia hii kuliniathili pakubwa sana kisaikolojia na athari yake hiyo ilikuwa bado haijaisha moyoni mwangu.
Mpaka leo huwa sipati jibu ukiwa wanaoupata wale wanaoondokewa na wenzi wao wa ndoa wanaowapenda kwa dhati. Ikiwa mimi niliipata freshi kwa mpenzi tu ambaye tulikuwa hata bado hatujaoana, wao sasa inakuwaje ukizingatia tayari wameshaonja tamu ya ndoa?
Marehemu Anna alikuwa ni msichana wa pekee ambaye nilitokea kumpenda kipindi nasoma. Mimi nilikuwa nasoma elimu ya sekondari yeye alikuwa bado yupo shule ya msingi.
Uzuri wa sura yake, umbo pamoja na tabia ndivyo vilikuwa vimenichengua mtoto wa kiumi mpaka nikawa sijiwezi, nikafa na kuoza kwake kama vijana wa kileo wasemavyo. Mtoto alikuwa yupo kamili gado, kamili kila idara.
Mpaka wa leo huwa natafutia msichana mwenye sifa kama zake lakini naambulia hola! Wasichana wa namna hiyo ni adimu sana kuwapata, yaani ni sawa na kumsaka bikira uswahilini kwani unaweza ukakesha bila hata ya kumpata.
Mapenzi yetu hayakuwa kama mapenzi yale yanayofanywa na vijana wa siku hizi, mapenzi ya kuanza kuzini kabla hata hamjafunga ndoa. Eti wao husema huwezi ukauziwa mbuzi kwenye gunia; wapi ndugu zangu hizo ni roho za pepo wachafu tu, pepo wa uzinzi.
Ndiyo zao vijana wa siku hizi, hasa wavulana. Utakuta wanakwambia kumuoa mwanamke huku hujafanya naye mapenzi ni kosa la jinai kwani unaweza ukakuta hayawezi ‘mahabati’,mwenye kutulia kama gogo kwenye mambo fulani. Wanasema yote hayo ni tisa, kumi ukute bwawa na siyo kisima, au ukutane na ile timu ya Songea; unaweza ukatangaza taraka. Hiyo ndiyo mitazamo yao.
Mimi hayo sikujali kwani niliona ni upuuzi na ulimbukeni mkubwa unaotokana na utumwa wa mapepo ya uzinzi. Kutokana na misingi mizuri ya kidini niliyokuwa nimefundishwa tangu utotoni niliamini kuwa hakuna linaloshindikana mbele ya Mwenyezi Mungu.
Kama yeye huwatakasa mpaka wenye ukoma, kwa nini asikibadilishe kitu chochote kinacholeta kikwazo kwako kilichopo kwenye mwili wa mwenzi wako wa ndoa uliyemuoa kwa ndoa halali kabisa? Yote yanawazekana.  
Hivyo ndivyo mitazamo wetu ilivyokuwa. Bahati nzuri ni kwamba Anna alikuwa bado hajaupoteza usichana wake na mimi nilikuwa sijaupoteza uvulana wangu. Wote tulikuwa safi kabisa.
Pamoja na kupendana kwetu lakini tulikubaliana kutofanya mapenzi mpaka tuje kufunge ndoa kwani kinyume na hapo ni dhambi kwa Mungu, dhambi ya kuzini ambayo inawatafuna vijana wengi wa siku hizi.
Huo ndiyo huitwa upendo wa kweli, mapenzi yasiochuja mpaka uzeeni. Siyo mapenzi feki ambayo leo mko pamoja halafu kesho mnazinguana na kushika hamsini zake kila mmoja.
Kifo cha Anna ndiyo kilizima taa za upendo moyoni mwangu na kuacha giza totoro ambalo mpaka leo ni athari kubwa kwangu.
Alikuwa anajipenda, alikuwa anajiheshimu, wala hakuwa mapepe na ndio maana vijana wengi wa mtaani walitamani sana awe wao matokeo yake waliishia kula ‘vibuti’ vya uso.
Amini usiamini siku zote mti wenye matunda ndiyo hupigwa mawe. Kutokana na usemi huo, kipenzi Anna nilimfananisha na mti wa mnazi ambao hata ukiupopoa kwa mawe huwezi kuangusha nazi wala dafu. Kumbe nilikuwa najidanganya kwani kuna wakwezi ambao hupanda mpaka matunda yaliko kisha huanza kuyasanifu kwa vyovyote vile wanavyotaka.
Hicho ndicho kilichotokea kwa marehemu Anna. Pamoja na kuwa na msimamo zaidi ya binti wa kilokole, ilifika siku maagano yetu yakavunjika japokuwa siyo kwa ridhaa na utashi wake.
Ilikuwa ni siku ngumu sana kwake; siku aliyorubuniwa na dada yake kisha wakaenda kwenye sherehe ya kuzaliwa ya mpenzi wa huyo dada yake. Kumbe kulikuwa na mipango kabambe ya kumwingiza kipenzi changu kwenye jaribu zito lililokuja kupelekea kifo chake.

ITAENDELEA.....